Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Kwa nini Biblia inajirudia-rudia?

PINDI kwa pindi waandikaji wa Biblia walirudia misemo ileile neno kwa neno. Fikiria sababu tatu ambazo huenda ziliwachochoea waandikaji hao kufanya hivyo:

Kipindi cha wakati maneno hayo yalipoandikwa. Katika Israeli la kale, watu wengi hawakuwa na nakala za kibinafsi za ile Sheria. Mara nyingi walisikia Sheria hiyo ikisomwa wakati taifa lilipokusanyika pamoja kwenye hema la ibada. (Kum. 31:​10-12) Kuna uwezekano mkubwa kwamba kulikuwa na mambo yaliyowakengeusha fikira walipokuwa wakisikiliza na kusimama kwa saa kadhaa katika umati mkubwa. (Neh. 8:​2, 3, 7) Katika nyakati hizo, kurudia misemo muhimu kungefanya iwe rahisi kwa watu kukumbuka maandiko na kuyatumia. Kurudia maneno fulani kungewasaidia kukumbuka hasa habari zenye mambo mengi, kama vile, masharti na sheria za Mungu.—Law. 18:​4-22; Kum. 5:1.

Aina ya uandikaji. Asilimia 10 hivi ya Biblia ni nyimbo—kama vile kitabu cha Zaburi, Wimbo wa Sulemani, na Maombolezo. Wakati mwingine nyimbo zilitia ndani maneno yaliyorudiwa, yaliyounganisha utunzi wa wimbo na kuwasaidia wasikilizaji wakariri maneno ya wimbo huo. Kwa mfano, ona maneno yaliyo kwenye Zaburi 115:​9-11: “Ee Israeli, mtumainini Yehova—Yeye ndiye msaada wenu na ngao yenu. Ee nyumba ya Haruni, mtumainini Yehova—Yeye ndiye msaada wenu na ngao yenu. Ninyi mnaomwogopa Yehova, mtumainini Yehova—Yeye ndiye msaada wenu na ngao yenu.” Je, unaona jinsi ambavyo kurudia maneno hayo kungewasaidia waimbaji kukumbuka kweli hizo zenye thamani na kuziweka moyoni na akilini?

Uhitaji wa kukazia mambo muhimu. Wakati mwingine waandikaji wa Biblia walirudia misemo muhimu. Kwa mfano, Yehova alipowaamuru Waisraeli wasile damu, Yehova alimwongoza Musa arudie sababu ya kutokula damu mara nyingi. Mungu alitaka kukazia kwamba uhai wa kiumbe umo katika damu, yaani, damu inawakilisha uhai. (Law. 17:​11, 14) Baadaye, mitume na wazee huko Yerusalemu waliorodhesha njia muhimu za kuepuka kumchukiza Mungu, walikazia tena umuhimu wa kujiepusha na damu.—Mdo. 15:​20, 29.

Yehova hakukusudia kurudiwa kwa misemo ya Kimaandiko kuwe desturi fulani. Kwa mfano, Yesu alisema: “Mnaposali msiseme mambo yaleyale tena na tena.” (Mt. 6:7) Kisha akatupatia habari zinazofaa kutajwa katika sala zinazopatana na mapenzi ya Mungu. (Mt. 6:​9-13) Basi, ingawa tunaepuka kurudia maneno yaleyale tena na tena katika sala, tuna uhuru wa kurudia habari zilezile tena na tena.—Mt. 7:​7-11.

Hivyo, kuna sababu nzuri kwa nini Neno la Mungu lililoongozwa na roho linarudia maneno au misemo fulani. Ni njia mojawapo kati ya nyingi ambazo Mfundishaji wetu Mkuu anatufundisha jinsi ya kujinufaisha wenyewe.—Isa. 48:​17, 18.