Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Nguvu za Mungu Zimeonekana Wazi Kupitia Udhaifu Wangu

Nguvu za Mungu Zimeonekana Wazi Kupitia Udhaifu Wangu

MIMI na mke wangu tulipofika nchini Kolombia mwaka wa 1985, tulipata nchi hiyo ikikabiliana na vitendo vingi sana vya ukatili. Serikali ilikuwa ikikabiliana na vikundi vyenye nguvu vya walanguzi wa dawa za kulevya jijini na vikundi vya wapiganaji walioishi milimani. Katika eneo la Medellín, ambapo tulitumikia baadaye, vikundi vya vijana wahalifu waliokuwa na silaha walikuwa wakizunguka-zunguka mitaani. Waliuza madawa ya kulevya, waliwalazimisha watu wawalipe pesa ili wasiwadhuru, na walilipwa pesa ili wawaue watu. Hakuna hata mmoja wao aliyeishi kwa muda mrefu. Tulihisi ni kana kwamba tupo katika dunia tofauti.

Tukiwa watu wawili wa kawaida kutoka Finland, mojawapo ya nchi za kaskazini kabisa mwa dunia, tulifikaje Amerika Kusini? Na nimejifunza mambo gani katika miaka hiyo mingi?

MAISHA YANGU YA UJANA NCHINI FINLAND

Nilizaliwa mwaka wa 1955, nikiwa wa mwisho katika familia ya wavulana watatu. Nililelewa karibu na pwani ya kusini ya Finland, katika eneo ambalo sasa linajulikana kuwa jiji la Vantaa.

Mama yangu alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova miaka michache kabla sijazaliwa. Hata hivyo, baba yangu alipinga kweli na hakumruhusu mama yangu ajifunze na sisi watoto au kutupeleka katika mikutano ya kutaniko. Kwa hiyo, alitufundisha kweli za msingi za Biblia wakati baba hakuwepo.

Nilichukua msimamo upande wa Yehova nikiwa na umri wa miaka saba

Tangu nilipokuwa mtoto, niliazimia kumtii Yehova. Kwa mfano, pindi fulani nilipokuwa na umri wa miaka saba, mwalimu wangu alinikasirikia sana kwa sababu nilikataa kula verilättyjä (chapati za maji za Finland zilizochanganywa na damu). Alitumia mkono mmoja kubana mashavu yangu ili nifungue mdomo, na kwenye mkono mwingine alikuwa ameshika uma uliokuwa na kipande cha chapati hiyo na alilazimisha kuiingiza mdomoni mwangu ili niile. Nilifanikiwa kuusukuma uma huo, nao ukaanguka kutoka mkononi mwake.

Nilipokuwa na umri wa miaka 12, baba yangu alikufa. Baada ya hapo, ningeweza kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Akina ndugu katika kutaniko walinionyesha fadhili na walipendezwa nami, na hilo lilinichochea kufanya maendeleo ya kiroho. Nilianza kusoma Biblia kila siku na kujifunza machapisho yetu ya Kikristo kwa bidii. Kwa sababu nilikuwa na mazoea hayo mazuri ya kujifunza, nilibatizwa Agosti 8, 1969, nikiwa na umri wa miaka 14.

Baada tu ya kumaliza shule, nilianza upainia. Baada ya majuma machache, nilihamia kwenye eneo lenye uhitaji mkubwa la Pielavesi, karibu na eneo la katikati ya Finland.

Nilipokuwa Pielavesi, nilikutana na msichana ambaye alikuja kuwa mke wangu mpendwa, Sirkka. Nilivutiwa naye kwa sababu ni mwenye kiasi na alimpenda sana Yehova. Hakutafuta umashuhuri au vitu vya kimwili. Sote tulitamani kufanya yote tunayoweza katika utumishi wetu kwa Yehova na tulikuwa tayari kutimiza mgawo wowote tuliopewa. Tulifunga ndoa Machi 23, 1974. Badala ya kwenda fungate, tulienda kutumikia katika mji wa Karttula, ambapo kulikuwa na uhitaji zaidi wa wahubiri wa Ufalme.

Nyumba tuliyoishi Karttula, Finland

YEHOVA ALITUTUNZA

Gari tulilopewa na ndugu yangu

Tangu mwanzoni mwa ndoa yetu, Yehova alionyesha kwamba angetutunza ikiwa tungetanguliza Ufalme wake maishani. (Mt. 6:33) Kwa mfano, tulipokuwa Karttula, hatukuwa na gari. Mwanzoni, tulisafiri kwa baiskeli. Hata hivyo, katika msimu wa baridi kulikuwa na baridi kali sana. Ili tuweze kuwahubiria watu katika eneo hilo kubwa tulihitaji kuwa na gari. Lakini hatukuwa na pesa za kununua gari.

Bila kutarajia, ndugu yangu mkubwa alikuja kututembelea. Kwa fadhili alitupatia gari lake ambalo lilikuwa limelipiwa bima. Tulihitaji tu kununua mafuta. Na baada ya hapo, tukawa na gari tulilohitaji.

Yehova alituonyesha kwamba angetimiza jukumu lake la kutupatia mahitaji yetu ya kimwili. Kazi yetu ilikuwa kutanguliza masilahi ya Ufalme.

SHULE YA GILEADI

Darasa letu la Shule ya Utumishi wa Painia la 1978

Tulipokuwa tukihudhuria Shule ya Utumishi wa Painia mwaka wa 1978, Raimo Kuokkanen, a mmoja wa walimu wetu, alitutia moyo tujaze ombi la kuhudhuria Shule ya Gileadi. Hivyo, tulianza kujifunza Kiingereza tukiwa na lengo la kustahili kuhudhuria. Hata hivyo, mwaka wa 1980, kabla hatujajaza ombi hilo, tulialikwa tutumikie katika ofisi ya tawi ya Finland. Wakati huo, Wanabetheli hawangeweza kutuma ombi la kuhudhuria Shule ya Gileadi. Lakini tulitaka kutumikia mahali popote ambapo Yehova aliona palitufaa, na si pale ambapo sisi tuliona kuwa panafaa. Hivyo, tulikubali mwaliko huo. Hata hivyo, tuliendelea kujifunza Kiingereza ili tuwe tayari kujaza ombi la Shule ya Gileadi ikiwa nafasi ingetokea.

Miaka michache baadaye, Baraza Linaloongoza liliwapa Wanabetheli nafasi ya kujaza ombi la kuhudhuria Shule ya Gileadi. Tulijaza ombi hilo mara moja, lakini si kwa sababu hatukufurahia kuwa Betheli. Badala yake, tulitaka kuonyesha tuko tayari kutumikia mahali popote penye uhitaji mkubwa ikiwa tungestahili. Tulialikwa katika darasa la 79 la Shule ya Gileadi na tulihitimu Septemba 1985. Tulipata mgawo wa kwenda nchini Kolombia.

MGAWO WETU WA KWANZA WA UMISHONARI

Mgawo wetu wa kwanza nchini Kolombia, ulikuwa katika ofisi ya tawi. Nilijitahidi kufanya yote niliyoweza katika mgawo wangu, lakini baada ya mwaka mmoja katika ofisi ya tawi, nilihisi tulihitaji kufanya mabadiliko. Kwa mara ya kwanza na ya pekee maishani mwangu, niliomba kubadilishiwa mgawo. Baadaye, tulipata mgawo wa kuwa wamishonari katika jiji la Neiva, kwenye eneo la Huila.

Sikuzote nimefurahia utumishi wa shambani. Nikiwa painia mseja nchini Finland, wakati mwingine ningehubiri mapema asubuhi hadi jioni sana. Pia, tukiwa wenzi wapya wa ndoa, kuna siku ambazo mimi na Sirkka tulihubiri siku nzima. Nyakati nyingine tulilala kwenye gari tulipohubiri katika maeneo ya mbali. Kufanya hivyo kulitusaidia kupunguza saa tulizotumia kusafiri na kuanza safari mapema siku iliyofuata.

Tukiwa wamishonari, tulihisi tena shauku ileile katika huduma ambayo tulikuwa nayo awali. Tulikuwa na ongezeko katika kutaniko letu, na ndugu na dada wa Kolombia walikuwa wenye heshima, upendo, na shukrani.

NGUVU YA SALA

Umbali mfupi kutoka kwenye mgawo wetu jijini Neiva, kulikuwa na miji ambayo haikuwa na Mashahidi. Nilihangaishwa sana na jinsi ambavyo habari njema ingefika katika maeneo hayo. Hata hivyo, kwa sababu kwenye maeneo hayo kulikuwa na vikundi vilivyokuwa vikipigana, hakukuwa salama kwa wageni. Hivyo, nilisali kwamba mtu mmoja kutoka katika miji hiyo awe Shahidi. Nilifikiri mtu huyo angepaswa kuishi Neiva ili ajifunze kweli. Hivyo, nilisali kwamba baada ya ubatizo awe mkomavu kiroho na arudi katika mji wao ili ahubiri. Nilipaswa kujua kwamba Yehova alikuwa na suluhisho bora kuliko langu.

Muda mfupi baadaye, nilianza kujifunza Biblia pamoja na mwanamume kijana anayeitwa Fernando González. Aliishi Algeciras, mojawapo ya miji ambayo hakukuwa na Mashahidi. Fernando angesafiri umbali wa kilomita 50 ili kuja Neiva kufanya kazi. Alijitayarisha vizuri kwa ajili ya kila kipindi cha funzo na mara moja alianza kuhudhuria mikutano yote. Tangu juma la kwanza alipoanza kujifunza, Fernando angewakusanya watu wengine katika mji wao wa nyumbani na kuwafundisha mambo ambayo alikuwa amejifunza katika funzo lake la Biblia.

Pamoja na Fernando mwaka wa 1993

Fernando alibatizwa Januari 1990, miezi sita baada ya kuanza kujifunza. Baadaye, akawa painia wa kawaida. Kwa kuwa sasa kulikuwa na Shahidi aliye mwenyeji katika mji wa Algeciras, kwa kadiri fulani ilikuwa salama kwa ofisi ya tawi kutuma mapainia wa pekee katika eneo hilo. Na Februari 1992, kutaniko lilianzishwa katika mji huo.

Je, Fernando alihubiri tu katika mji wao wa nyumbani? Hapana! Baada ya kufunga ndoa, yeye na mke wake walihamia San Vicente del Caguán, mji mwingine ambao pia haukuwa na Mashahidi. Na walisaidia kuanzisha kutaniko katika mji huo. Mwaka wa 2002, Fernando aliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko. Yeye na Olga, mke wake, wanaendelea na kazi ya kuzungukia makutaniko hadi leo.

Kupitia kisa hicho, nilijifunza umuhimu wa kusali kuhusu mambo hususa yanayohusiana na migawo yetu ya kitheokrasi. Yehova anatimiza mambo ambayo sisi hatuwezi. Isitoshe, mavuno ni yake, na si yetu.—Mt. 9:38.

YEHOVA HUTUPATIA“HAMU NA NGUVU ZA KUTENDA”

Mwaka wa 1990 tulipata mgawo wa kuzungukia makutaniko. Mzunguko wetu wa kwanza ulikuwa katika mji mkuu, Bogotá. Tulikuwa na wasiwasi sana. Mimi na mke wangu ni watu wa kawaida na hatuna vipawa vyovyote vya pekee. Na hatukuwa tumezoea kuishi kwenye jiji kubwa lenye shughuli nyingi. Hata hivyo, Yehova alitimiza ahadi yake inayopatikana kwenye Wafilipi 2:13: “Mungu ndiye ambaye kwa mapenzi yake mema anawachochea, na kuwapa hamu na nguvu za kutenda.”

Baadaye, tulitumwa kwenye mzunguko mwingine katika eneo la Medellín, ambalo nililitaja awali. Watu katika eneo hilo walizoea kuona watu wakitendewa vitendo vya kikatili mitaani hivi kwamba waliliona kuwa jambo lisiloshtua. Kwa mfano, pindi moja nilipokuwa nikiongoza funzo la Biblia, watu walianza kurushiana risasi nje ya nyumba niliyotembelea. Nilikuwa karibu kulala chini sakafuni, lakini mwanafunzi wa Biblia aliendelea kusoma fungu bila wasiwasi wowote. Alipomaliza kusoma fungu hilo, aliniambia anatoka nje kwa muda mfupi. Baada ya muda, alirudi akiwa na watoto wadogo wawili na kwa utulivu alisema, “Samahani, nilihitaji kwenda kuwachukua watoto wangu.”

Pia, kuna pindi nyingine ambazo tulikuwa hatarini. Wakati fulani tulipokuwa katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba, mke wangu alinikimbilia akiwa na wasiwasi sana. Aliniambia kwamba mtu mmoja alijaribu kumpiga risasi. Nilishtuka sana. Hata hivyo, baadaye tulitambua kwamba mwanamume huyo mwenye bunduki alikuwa akimlenga mtu aliyekuwa akipita karibu kabisa na Sirkka.

Baada ya muda, hatukuogopa sana vitendo vya ukatili vilivyotokea mitaani. Tulitiwa moyo na uthabiti wa Mashahidi katika eneo hilo ambao walikabili hali kama hizo au mbaya zaidi ya hizo. Tulifikia mkataa kwamba ikiwa Yehova alikuwa akiwasaidia wao, angetusaidia sisi pia. Sikuzote tulifuata ushauri wa wazee wa kutaniko katika eneo hilo, tulichukua tahadhari, na kuacha mambo mengine mikononi mwa Yehova.

Bila shaka, baadhi ya hali hazikuwa hatari sana kama tulivyofikiria. Pindi moja, nilisikia sauti kama ya wanawake wawili wakitupiana maneno nje ya nyumba niliyokuwa nimetembelea. Sikutaka kutazama watu wakibishana, lakini mwenye nyumba aliniambia twende kwenye eneo la mbele ya nyumba. Badala ya kukuta watu “wakibishana,” tulikuta kasuku wawili wakiiga sauti za majirani.

MAPENDELEO MENGINE NA CHANGAMOTO

Mwaka wa 1997, niliwekwa rasmi kuwa mwalimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. b Sikuzote nilifurahia kuhudhuria shule za kitheokrasi, lakini sikuwahi kamwe kuwazia kwamba ningepata pendeleo la kufundisha mojawapo ya shule hizo.

Baadaye, nilitumikia nikiwa mwangalizi wa wilaya. Mpango huo ulipositishwa, nilianza tena kazi ya kuzungukia makutaniko. Kwa zaidi ya miaka 30, nimefurahia kutumikia nikiwa mwalimu wa shule za kitheokrasi na mwangalizi wa mzunguko. Migawo hiyo imeniletea baraka nyingi. Hata hivyo, mambo hayakuwa rahisi sikuzote. Acheni niwasimulie.

Mimi ni mtu anayechukua hatua mara moja kwa uthabiti. Hilo limenisaidia kukabiliana na hali ngumu. Hata hivyo, mara nyingine nimekuwa na bidii iliyopita kiasi ilipohusu kurekebisha mambo katika makutaniko. Pindi fulani, kwa shauku niliwahimiza baadhi ya watu wawaonyeshe upendo na usawaziko wengine. Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kwamba pindi hizohizo, mimi pia sikuonyesha sifa hizo.—Rom. 7:​21-23.

Nyakati fulani, nilivunjika moyo sana kwa sababu ya udhaifu wangu mbalimbali. (Rom. 7:24) Pindi moja, nilimwambia Yehova katika sala kwamba ingefaa zaidi ikiwa ningeacha umishonari na kurudi nchini Finland. Jioni hiyo, nilihudhuria mkutano wa kutaniko. Kitia moyo nilichopata kilinisadikisha kwamba nilipaswa kubaki katika mgawo wangu na kuendelea kufanyia kazi udhaifu wangu. Hadi leo, ninashukuru sana jinsi Yehova alivyojibu waziwazi sala hiyo. Pia, ninathamini sana jinsi ambavyo kwa fadhili amenisaidia kushinda udhaifu wangu mbalimbali.

KUTAZAMIA WAKATI UJAO KWA UHAKIKA

Mimi na Sirkka tunamshukuru sana Yehova kwa pendeleo la kutumia sehemu kubwa ya maisha yetu katika utumishi wa wakati wote. Pia, ninamshukuru sana Yehova kwa kunipatia mke mwenye upendo na mwaminifu kwa miaka hiyo yote.

Hivi karibuni, nitatimiza umri wa miaka 70 na nitaacha kutumikia nikiwa mwalimu wa shule za kitheokrasi na mwangalizi wa mzunguko. Hata hivyo, hilo halinivunji moyo. Kwa nini? Kwa sababu ninaamini kabisa kwamba jambo linalomletea heshima zaidi Yehova ni tukimtumikia kwa kiasi na kumsifu kutoka katika moyo uliojaa upendo na shukrani. (Mika 6:8; Marko 12:​32-34) Hatuhitaji kuwa na mgawo unaoonekana kuwa muhimu ili kumheshimu Yehova.

Ninapokumbuka migawo niliyofurahia, ninatambua kwamba sikuipata kwa sababu mimi ni bora kuliko wengine; wala kwa sababu ya uwezo fulani wa pekee. Badala yake, Yehova alinipatia migawo hiyo kwa sababu ya fadhili zake zisizostahiliwa. Alinipatia mapendeleo hayo licha ya udhaifu wangu. Ninajua kwamba nimefaulu kutimiza migawo hiyo kwa sababu tu ya msaada wa Yehova. Kwa njia hiyo, nguvu za Mungu zimeonekana wazi kupitia udhaifu wangu.—2 Kor. 12:9.

a Simulizi la maisha la Raimo Kuokkanen, “Tuliazimia Kumtumikia Yehova,” lilichapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 2006.

b Sasa ni Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme.