Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 14

WIMBO 56 Fanya Kweli Iwe Njia Yako ya Maisha

‘Songa Mbele Kuelekea Ukomavu’

‘Songa Mbele Kuelekea Ukomavu’

“Na tusonge mbele kuelekea ukomavu.”EBR. 6:1.

JAMBO KUU

Jifunze jinsi Mkristo mkomavu anavyofikiri na kutenda kupatana na mapenzi ya Mungu na anavyofanya maamuzi ya hekima.

1. Yehova anataka tufanye nini?

 MOJAWAPO ya pindi zenye shangwe zaidi kwa wenzi wa ndoa ni wakati mtoto wao anapozaliwa. Ingawa wazazi wanampenda mtoto wao aliyezaliwa, hawangependa abaki akiwa mchanga. Kwa kweli, wazazi wanaweza kuwa na wasiwasi sana ikiwa mtoto wao hakui. Vivyo hivyo, Yehova anafurahi sana anapoona tunachukua hatua ya kwanza ya kuwa wafuasi wa Yesu, lakini hataki tuendelee kuwa watoto kiroho. (1 Kor. 3:1) Badala yake, anataka tuwe Wakristo walio “watu wazima.”—1 Kor. 14:20.

2. Tutachunguza nini katika makala hii?

2 Inamaanisha nini kuwa Wakristo walio watu wazima? Tunahitaji kufanya nini ili tuwe Wakristo wakomavu? Chakula kigumu cha kiroho kinatusaidiaje kukua kiroho? Na kwa nini tunapaswa kuepuka kujiamini kupita kiasi? Katika makala hii, tutachunguza majibu ya maswali hayo.

KUWA MKRISTO MKOMAVU KUNAMAANISHA NINI?

3. Kuwa Mkristo aliye mtu mzima kunamaanisha nini?

3 Katika Biblia, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “watu wazima” linaweza pia kumaanisha, “wakomavu,” “wakamilifu,” na “kamili.” a (1 Kor. 2:6) Tunakuwa Wakristo walio watu wazima, au wakomavu tunapoendelea kukua kutoka kuwa watoto kiroho hadi kuwa wanaume au wanawake wa kiroho. Bila shaka, hata tunapofikia lengo hilo, hatupaswi kamwe kuacha kuendelea kukua kiroho. (1 Tim. 4:15) Sisi sote, kutia ndani vijana, tunaweza kuwa wakomavu kiroho. Lakini ni nini kinachoonyesha kwamba Mkristo amekuwa mkomavu?

4. Mkristo mkomavu yukoje?

4 Mkristo mkomavu ni yule anayeishi kulingana na matakwa yote ya Mungu, hachagui matakwa ambayo atafuata na yale ambayo hatayafuata. Bila shaka, atafanya makosa kwa kuwa yeye si mkamilifu. Hata hivyo, anaonyesha kupitia maisha yake ya kila siku kwamba anafikiri na kutenda kupatana na mapenzi ya Mungu. Amevaa utu mpya na anaendelea kujitahidi kupatanisha njia yake ya kufikiri na njia ya kufikiri ya Mungu. (Efe. 4:​22-24) Amejizoeza kufanya maamuzi ya hekima kwa kutegemea sheria na kanuni za Yehova, hivyo hahitaji orodha ndefu ya amri za kumwongoza. Anapofanya uamuzi, anajitahidi sana kutenda kupatana na uamuzi wake.—1 Kor. 9:​26, 27.

5. Mkristo asiye mkomavu anakabili hatari zipi? (Waefeso 4:​14, 15)

5 Kwa upande mwingine, Mkristo ambaye si mkomavu anaweza kudanganywa kwa urahisi kupitia “udanganyifu” na “njia za hila” na anaweza kuwaamini waasi-imani na wale wanaoeneza fununu zisizo na msingi. b (Soma Waefeso 4:​14, 15.) Huenda akawaonea wivu wengine, akasababisha mizozo, au akakasirika haraka. Na anaweza kufanya jambo baya anaposhawishiwa.—1 Kor. 3:3.

6. Kwa nini tunaweza kulinganisha kufikia ukomavu wa kiroho na ukuaji wa mtoto? (Tazama pia picha.)

6 Kama ilivyotajwa mwanzoni, Maandiko yanalinganisha hatua za kukua kiroho na hatua za ukuaji wa mtoto hadi kuwa mtu mzima. Mtoto hajui mambo mengi, hivyo anahitaji ulinzi na mwongozo wa mtu mzima. Kwa mfano, huenda mama akamwambia binti yake amshike mkono wanapovuka barabara. Binti huyo anapokua, huenda mama yake akamruhusu avuke barabara mwenyewe, lakini atamkumbusha kwamba kabla ya kuvuka, ahakikishe hakuna gari lolote lililo karibu. Msichana huyo anapokuwa mtu mzima, atajua jinsi ya kuepuka hatari kama hizo. Kama watoto wadogo wanavyohitaji msaada wa watu wazima ili waepuke hatari, ndivyo Wakristo wasio wakomavu wanavyohitaji msaada wa mara kwa mara kutoka kwa Wakristo wakomavu ili waepuke hatari za kiroho na kufanya maamuzi ya hekima. Kwa upande mwingine, Wakristo wakomavu wanapofanya uamuzi, wanafikiria kwa makini sana kanuni za Biblia kuhusu jambo hilo na kisha wanatenda kulingana na mambo waliyojifunza.

Wakristo wasio wakomavu wanahitaji kujifunza jinsi ya kufanya maamuzi ya hekima kwa kutumia kanuni za Biblia (Tazama fungu la 6)


7. Je, Wakristo wakomavu wanahitaji msaada wa wengine?

7 Je, hilo linamaanisha kwamba Mkristo mkomavu hahitaji kamwe msaada wa mtu yeyote? Hapana. Wakati mwingine, Mkristo mkomavu anahitaji kuomba msaada kutoka kwa wengine. Lakini mtu ambaye si mkomavu huenda akatarajia wengine wamwambie jambo la kufanya au wamfanyie uamuzi ambao yeye mwenyewe angepaswa kufanya. Kwa upande mwingine, Mkristo mkomavu hutafuta msaada kutoka kwa watu wengine wenye hekima na uzoefu kuliko yeye huku akitambua kuwa Yehova anatarajia kwamba “ataubeba mzigo wake mwenyewe.”—Gal. 6:5.

8. Wakristo wakomavu hutofautiana katika njia zipi?

8 Sifa za Wakristo wakomavu hutofautiana kama tu mwonekano wa watu wazima unavyotofautiana. Kwa mfano, baadhi ya Wakristo wakomavu wanaweza kuwa na hekima sana, wengine wakawa na ujasiri sana, na wengine wakawa wakarimu sana, au wenye huruma sana. Isitoshe, Wakristo wawili wakomavu wanapokabili hali zinazofanana, wanaweza kufanya maamuzi tofauti, lakini maamuzi yao yakapatana na kanuni za Biblia. Mara nyingi jambo hilo hutokea Wakristo wanapofanya uamuzi unaotegemea dhamiri zao. Kwa sababu wanatambua jambo hilo, kila mmoja anaepuka kumhukumu mwenzake kwa sababu ya tofauti zao. Badala yake, wanakazia fikira kuendelea kuwa na umoja.—Rom. 14:10; 1 Kor. 1:10.

TUNAHITAJI KUFANYA NINI ILI TUWE WAKRISTO WAKOMAVU?

9. Je, ukuaji wetu wa kiroho unajitokeza wenyewe tu? Fafanua.

9 Kadiri muda unavyopita, ndivyo mtoto anavyokua, lakini ili tukue kiroho tunahitaji kufanya jitihada. Kwa mfano, ndugu na dada katika kutaniko la Korintho walikubali habari njema, wakabatizwa, wakapokea roho takatifu, na kunufaika kutokana na mambo ambayo mtume Paulo aliwafundisha. (Mdo. 18:​8-11) Hata hivyo, miaka kadhaa baada ya ubatizo wao, wengi walikuwa bado hawajakomaa kiroho. (1 Kor. 3:2) Tunawezaje kuhakikisha kwamba hatupatwi na jambo kama hilo?

10. Ni lazima tufanye nini ili tufikie ukomavu? (Yuda 20)

10 Ili kufikia ukomavu, ni lazima kwanza tusitawishe tamaa ya kutaka kuwa wakomavu. Wale ‘wanaoupenda ujinga,’ wanaopenda kuendelea kuwa watoto kiroho, hawatafanya maendeleo. (Met. 1:22) Hatungependa kuwa kama wale ambao tayari ni watu wazima lakini wanaendelea kuwategemea wazazi wao wawafanyie maamuzi. Badala yake, tunatimiza wajibu wetu na kuhakikisha kwamba uhusiano wetu na Yehova unaendelea kukua. (Soma Yuda 20.) Ikiwa bado unajitahidi kufikia ukomavu, sali kwa Yehova akupatie “hamu na nguvu za kutenda.”—Flp. 2:13.

11. Yehova anatusaidiaje ili tufikie ukomavu? (Waefeso 4:​11-13)

11 Yehova hatarajii tujitegemee wenyewe tunapojitahidi kukua kiroho. Wale wanaotumikia wakiwa wachungaji na walimu katika kutaniko la Kikristo wametayarishwa ili kutusaidia ‘tukomae kabisa’ kiroho “na kufikia kiwango cha kimo kamili cha Kristo.” (Soma Waefeso 4:​11-13.) Pia, Yehova anatupatia roho yake takatifu ili itusaidie kuwa na “akili ya Kristo.” (1 Kor. 2:​14-16) Zaidi ya hayo, kupitia roho yake Mungu aliongoza vitabu vinne vya Injili viandikwe ili kutuonyesha jinsi Yesu alivyofikiri, alivyosema, na kutenda alipokuwa katika huduma yake duniani. Kwa kuiga njia ya Yesu ya kufikiri na kutenda, unaweza kufikia lengo lako la kuwa Mkristo mkomavu.

CHAKULA KIGUMU CHA KIROHO KINATUSAIDIA KUKUA KIROHO

12. “Fundisho la msingi kumhusu Kristo” ni nini?

12 Ili kufikia ukomavu wa kiroho, ni lazima “[tuliache] nyuma fundisho la msingi kumhusu Kristo,” yaani, tujifunze mengi zaidi ya mafundisho ya msingi ya Kikristo. Kwa mfano, mafundisho hayo ya msingi yanatia ndani toba, imani, ubatizo, na ufufuo. (Ebr. 6:​1, 2) Hayo ni baadhi ya mafundisho ya msingi ambayo Wakristo wote huamini. Ndiyo sababu mtume Petro alizungumzia mafundisho hayo ya msingi alipouhubiria umati wa watu katika siku ya Pentekoste. (Mdo. 2:​32-35, 38) Ni lazima tukubali mafundisho hayo ya msingi ili tuwe wanafunzi wa Kristo. Kwa mfano, Paulo alionya kwamba yeyote anayekataa fundisho la ufufuo anakataa imani yote ya Kikristo. (1 Kor. 15:​12-14) Hata hivyo, hatupaswi kuridhika tu na mafundisho ya msingi ya kweli.

13. Ni lazima tufanye nini ili tunufaike na chakula kigumu cha kiroho kinachotajwa kwenye Waebrania 5:14? (Tazama pia picha.)

13 Tofauti na fundisho hilo la msingi, chakula kigumu cha kiroho kinahusisha sheria na pia kanuni za Yehova, ambazo zinatusaidia kuelewa njia yake ya kufikiri. Ili tunufaike na chakula hicho kigumu cha kiroho, ni lazima tujifunze kwa makini Neno la Mungu, tulitafakari, na kutumia mambo tunayojifunza. Tunapofanya hivyo, tunajizoeza kufanya maamuzi yanayomfurahisha Yehova. cSoma Waebrania 5:14.

Chakula kigumu cha kiroho kinatufundisha jinsi ya kufanya maamuzi yanayomfurahisha Yehova (Tazama fungu la 13) d


14. Paulo aliwasaidiaje Wakorintho wakue kiroho?

14 Mara nyingi ni vigumu kwa Wakristo wasio wakomavu kufanya maamuzi mazuri ikiwa hakuna sheria hususa katika Biblia, yaani, wanapohitaji kutumia kanuni za Biblia. Huenda baadhi ya watu wakahisi kwamba wanaweza kufanya chochote wanachotaka ikiwa hakuna sheria hususa inayotajwa katika Biblia. Na wengine wanaweza kuweka sheria kuhusu mambo ambayo hayahitaji sheria. Kwa mfano, inaonekana Wakristo jijini Korintho walimwomba Paulo awawekee sheria kuhusu ikiwa wangeweza kula chakula kilichotolewa kwa sanamu, au la. Badala ya kuwaambia jambo la kufanya, Paulo alionyesha kwamba kila mmoja wao alikuwa na ‘haki ya kuchagua’ kwa kutegemea kile ambacho dhamiri yake ilimruhusu kufanya. Alitaja baadhi ya kanuni za Biblia ambazo zingewasaidia kufanya uamuzi ambao haungeumiza dhamiri zao na wakati huohuo wasiwakwaze wengine. (1 Kor. 8:​4, 7-9) Hivyo, Paulo alikuwa akiwasaidia Wakorintho wakue kiroho ili waweze kutumia nguvu zao za utambuzi badala ya kumtegemea mtu mwingine au kutafuta tu sheria.

15. Paulo aliwasaidiaje Wakristo Waebrania wafanye maendeleo ya kiroho?

15 Tunajifunza somo muhimu sana kutokana na mambo ambayo Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania. Baadhi yao hawakuwa wameendelea kukua kiroho; kwa kweli ‘walihitaji tena maziwa, bali si chakula kigumu cha kiroho.’ (Ebr. 5:12) Hawakujifunza na kukubali kweli mpya ambazo Yehova alikuwa akizifunua hatua kwa hatua kupitia kutaniko. (Met. 4:18) Kwa mfano, Wakristo wengi Wayahudi bado waliendelea kushika Sheria ya Musa hata ingawa miaka 30 ilikuwa imepita tangu Sheria hiyo iondolewe kwa msingi wa dhabihu ya Kristo. (Rom. 10:4; Tito 1:10) Kwa kweli, miaka hiyo 30 iliwapa Wakristo Wayahudi wakati wa kutosha wa kuelewa kwamba hawakuhitaji tena kuifuata Sheria. Mtu yeyote ambaye amesoma barua iliyoongozwa na roho ambayo Paulo aliwaandikia Waebrania, anaweza kuthibitisha kwamba kitabu hicho kina chakula kigumu cha kiroho. Wakristo hao walihitaji kitia moyo hicho ili kuimarisha imani yao katika ubora wa mpango wa ibada ya Kikristo na ili kuwapa ujasiri wa kuendelea kuhubiri licha ya upinzani kutoka kwa Wayahudi.—Ebr. 10:​19-23.

EPUKA KUJIAMINI KUPITA KIASI

16. Zaidi ya kujitahidi kufikia ukomavu, ni lazima tufanye nini?

16 Ni lazima tujitahidi sana ili kufikia ukomavu wa kiroho na pia kuudumisha. Ili tufanikiwe tunahitaji kuepuka kujiamini kupita kiasi. (1 Kor. 10:12) Tunapaswa ‘kuendelea kujijaribu’ ili kuhakikisha kwamba tunaendelea kufanya maendeleo.—2 Kor. 13:5.

17. Barua ya Paulo kwa Wakolosai inaonyeshaje umuhimu wa kuendelea kuwa wakomavu?

17 Katika barua yake kwa Wakolosai, Paulo anaonyesha tena kwamba tunahitaji kuendelea kuwa wakomavu. Ingawa Wakristo hao walikuwa wakomavu, Paulo aliwaonya wawe makini ili wasinaswe na njia ya kufikiri ya ulimwengu. (Kol. 2:​6-10) Na Epafra, ambaye inawezekana aliwajua vizuri ndugu na dada kutanikoni, alisali bila kuacha kwamba ‘mwishowe wasimame wakiwa kamili,’ au wakomavu. (Kol. 4:12) Tunaweza kujifunza somo gani? Paulo na Epafra walijua kwamba ili tuendelee kuwa wakomavu tunahitaji kufanya jitihada nyingi na kupata msaada wa Mungu. Walitaka Wakristo Wakolosai waendelee kuwa wakomavu licha ya changamoto walizokuwa wakikabili.

18. Ni nini kinachoweza kumpata Mkristo mkomavu? (Tazama pia picha.)

18 Paulo aliwaonya Waebrania kwamba Mkristo mkomavu anaweza kupoteza kibali cha Yehova milele. Moyo wa Mkristo unaweza kuwa mgumu sana hivi kwamba anakosa kutubu na kupata msamaha wa Mungu. Inapendeza kwamba Waebrania hawakuwa wamefikia hatua hiyo. (Ebr. 6:​4-9) Namna gani wale ambao ni wahubiri wasiotenda au wametengwa na ushirika lakini baadaye wanatubu? Wanapotubu kwa unyenyekevu wanaonyesha kwamba wao ni tofauti na wale ambao Paulo aliandika kuwahusu. Hata hivyo, wanapomrudia Yehova, wanahitaji msaada ambao Yehova huandaa. (Eze. 34:​15, 16) Huenda wazee wakapanga Mkristo mkomavu awasaidie warudie tena uhusiano wao mzuri na Yehova.

Yehova huandaa msaada kwa ajili ya wale wote wanaohitaji kurudia tena hali yao nzuri ya kiroho (Tazama fungu la 18)


19. Tunapaswa kuwa na lengo gani?

19 Ikiwa unasonga mbele kuelekea ukomavu, unaweza kufikia lengo lako! Endelea kujilisha chakula kigumu cha kiroho na kupatanisha njia yako ya kufikiri na ile ya Yehova. Na ikiwa tayari wewe ni Mkristo mkomavu, endelea kuwa hivyo sasa na milele.

UNGEJIBUJE?

  • Kuwa Mkristo mkomavu kunamaanisha nini?

  • Tunaweza kufanya nini ili tuwe Wakristo wakomavu?

  • Kwa nini tunapaswa kuepuka kujiamini kupita kiasi?

WIMBO 65 Songa Mbele!

a Maandiko ya Kiebrania hayataji moja kwa moja maneno “mkomavu” au “asiye mkomavu,” lakini yanazungumzia wazo lililo katika maneno hayo. Kwa mfano, kitabu cha Methali kinamtofautisha mtu ambaye ni kijana na ambaye ni mjinga na yule mwenye hekima na uelewaji.—Met. 1:​4, 5.

b Tazama makala “Jilinde Dhidi ya Habari za Uwongo” katika mfululizo wa makala wa “Habari Zaidi” kwenye jw.org na JW Library.®

c Tazama makala yenye kichwa “Mradi wa Kujifunza” katika gazeti hili.

d MAELEZO YA PICHA: Ndugu akitumia kanuni za Biblia alizojifunza kutoka katika Neno la Mungu anapochagua burudani.