Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Kwa nini wanaume ambao si Waisraeli walitumikia katika jeshi la Mfalme Daudi?

KATIKA jeshi la Daudi kulikuwa na wanaume ambao hawakuwa Waisraeli kama vile Seleki Mwamoni, Uria Mhiti, na Ithma Mmoabu. a (1 Nya. 11:​39, 41, 46) Jeshi la Daudi lilitia ndani pia “Wakerethi, Wapelethi, na Wagathi.” (2 Sam. 15:18) Inaonekana kwamba Wakerethi na Wapelethi walikuwa na uhusiano wa karibu na Wafilisti. (Eze. 25:16) Wagathi walikuwa wakaaji wa jiji la Gathi lililokuwa katika eneo la Wafilisti.—Yos. 13:​2, 3; 1 Sam. 6:​17, 18.

Kwa nini Daudi aliruhusu wanaume ambao si Waisraeli watumikie katika jeshi lake? Alikuwa na uhakika kwamba walikuwa washikamanifu kwake, na jambo muhimu zaidi kwa Yehova. Kwa mfano, kamusi moja ya Biblia, The New Interpreter’s Dictionary of the Bible, inasema hivi inapozungumza kuhusu Wakerethi na Wapelethi: “Walidumisha ushikamanifu wao kwa Daudi hata katika pindi ngumu sana katika utawala wake.” Jinsi gani? Wakati “wanaume wote wa Israeli” walipomwacha Mfalme Daudi na kumfuata “mfanya fujo fulani aliyeitwa Sheba,” Wakerethi na Wapelethi walidumisha ushikamanifu wao kwa Daudi na wakamsaidia kukomesha uasi ambao Sheba alianzisha. (2 Sam. 20:​1, 2, 7) Katika pindi nyingine, Adoniya, mwana wa Mfalme Daudi alijaribu kunyakua ufalme. Hata hivyo, Wakerethi na Wapelethi walibaki wakiwa washikamanifu kwa Daudi na kumsaidia kumfanya Sulemani, ambaye Yehova alikuwa amemchagua atawale baada ya Daudi, awe mfalme.—1 Fal. 1:​24-27, 38, 39.

Mwanamume mwingine ambaye hakuwa Mwisraeli aliyebaki mshikamanifu sana kwa Daudi alikuwa Itai Mgathi. Itai na mashujaa wake 600 walimuunga mkono Mfalme Daudi wakati Absalomu, mwana wa Daudi, alipoasi na kugeuza mioyo ya wanaume wa Israeli dhidi ya mfalme. Mwanzoni, Daudi alimwambia Itai kwamba kwa sababu yeye si mwanamume Mwisraeli, hakupaswa kujihusisha katika mapigano hayo. Lakini Itai akasema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi na kwa hakika kama bwana wangu mfalme anavyoishi, mahali popote utakapokuwa wewe bwana wangu mfalme, ukiwa hai au ukiwa umekufa, mimi mtumishi wako nitakuwa mahali hapo!”—2 Sam. 15:​6, 18-21.

Itai alikuwa mshikamanifu kwa Daudi, mfalme mtiwa-mafuta wa Yehova

Ingawa Wakerethi, Wapelethi, na Wagathi hawakuwa Waisraeli, walimtambua Yehova kuwa Mungu wa kweli na Daudi kuwa mtiwa-mafuta wa Yehova. Ni lazima Daudi alithamini sana kuwa na wanaume hao washikamanifu waliomuunga mkono!

a Sheria ya Mungu iliyorekodiwa katika Kumbukumbu la Torati 23:​3-6 iliwakataza Waamoni na Wamoabu kuingia katika kutaniko la Israeli. Hata hivyo, inaonekana sheria hiyo ilikuwa ikirejelea mtu kuwa raia kamili kisheria katika taifa hilo na haikuwakataza wanaume hao ambao si Waisraeli kushirikiana au kuishi pamoja na watu wa Mungu. Tazama Insight on the Scriptures, Buku la 1, uku. 95.