Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 19

WIMBO 22 Ufalme Unatawala​—Tunasali Ukuye!

Tunajua Nini Juu ya Namna Yehova Atahukumu Watu?

Tunajua Nini Juu ya Namna Yehova Atahukumu Watu?

“Yehova . . . hataki mutu yeyote aharibiwe.”2 PE. 3:9.

WAZO KUBWA

Tunaweza kuwa hakika kama wakati Yehova atahukumu watu hivi karibuni, atafanya vile mu njia yenye kufaa na kwa haki.

1. Juu ya nini tunaweza kusema kama tuko naishi mu kipindi ya ajabu sana?

 TUNAISHI mu kipindi ya ajabu sana! Kila siku, tuko najionea namna unabii wa Biblia uko natimia. Kwa mufano, tuko naona namna “mufalme wa kaskazini” na “mufalme wa kusini” wako napigania utawala wa ulimwengu. (Da. 11:40, na maelezo ya chini.) Tuko naona namna habari njema iko nahubiriwa sana vile haiyahubiriwaka, na mamilioni ya watu wako nakubali kweli. (Isa. 60:22; Mt. 24:14) Na tuko napata chakula mingi ya kiroho “kwa wakati wenye kufaa.”—Mt. 24:45-47.

2. Tunaweza kuwa hakika na jambo gani, lakini tunapaswa kukubali nini?

2 Yehova anaendelea kutusaidia kuelewa muzuri zaidi matukio makubwa yenye kuwa mbele yetu. (Mez. 4:18; Da. 2:28) Tunaweza kuwa hakika kama, mbele taabu kubwa ianze, tutajua mambo yote yenye tuko nayo lazima ili tuendelee kuvumilia kwa uaminifu na tuendelee kuwa na umoja mu ile kipindi ya nguvu sana. Lakini, tunapaswa kukubali kama kuko mambo fulani yenye hatujue kuhusu mambo yenye itatokea hivi karibuni. Mu hii habari, tutazungumuzia kwanza juu ya nini tumebadilisha mambo yenye tulikuwa nasema kuhusu matukio fulani. Kisha tutarudilia mambo fulani yenye tunajua kuhusu wakati wenye kuya na namna Baba yetu wa mbinguni atatenda.

MAMBO YENYE HATUJUE

3. Zamani tulisema ni wakati gani njo Yehova hatapatia tena watu nafasi ya kujiunga na siye, na juu ya nini tulisema vile?

3 Zamani, tulisema kama wakati tu taabu kubwa itaanza, watu hawatapata tena nafasi ya kuwa upande wa Yehova na kuokoka Armagedoni. Tulisema vile juu tulielewa kama habari kuhusu Garika ilifananisha mambo yenye itatokea mu wakati wenye kuya. Kwa mufano, tuliwaza kama sawa vile tu Yehova alifunga mulango wa safina mbele Garika ianze, ku mwanzo wa taabu kubwa, Yehova “atafungia mulango” ulimwengu wa Shetani na ile itafanya watu wengine wasikuwe na nafasi ya kuwa upande wa Yehova na kuokolewa.—Mt. 24:37-39.

4. Habari kuhusu Garika ilikuwa na maana fulani ya kiunabii? Fasiria.

4 Habari kuhusu garika ilifananisha jambo fulani yenye itatokea mu wakati wenye kuya? Hapana. Juu ya nini? Juu Biblia haiseme vile. a Yesu alilinganisha “siku za Noa” na wakati wa kuwapo kwake, lakini hakusema kama kila tukio yenye ilitokea mu siku za Noa ilifananisha jambo fulani yenye itatokea mu wakati wenye kuya; hakusema kama kufunga mulango wa safina kulikuwa na maana fulani ya kiunabii. Lakini ile haimaanishe kama, habari kuhusu Noa na Garika haiwezi kutufundisha jambo fulani.

5. (a)  Noa alifanya nini mbele Garika ifike? (Waebrania 11:7; 1 Petro 3:20) (b) Kuhusu kazi ya kuhubiri, namna gani hali yetu inafanana na siku za Noa?

5 Juu Noa alisikia onyo yenye Yehova alimupatia, alionyesha kama alikuwa na imani kwa kujenga safina. (Soma Waebrania 11:7; 1 Petro 3:20.) Vilevile, wale wenye wanasikia habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu wanapaswa kutenda kulingana na mambo yenye wanasikia. (Mdo. 3:17-20) Petro alimuita Noa kuwa “muhubiri wa haki.” (2 Pe. 2:5) Lakini, vile tuliona mu habari yenye ilitangulia, hatujue ikiwa Noa alihubiria kila mutu ku dunia mbele Garika ifike. Leo tuko nafanya kazi ya kuhubiria watu mu dunia yote, na tunajikaza kuifanya kwa bidii. Lakini, hata tujikaze namna gani, hatuwezi kutangazia kila mutu ku dunia habari njema mbele mwisho ufike. Juu ya nini tunasema vile?

6-7. Juu ya nini tunaweza kusema kama hatutaweza kuhubiria kila mutu habari njema mbele mwisho ufike? Fasiria.

6 Fikiria mambo yenye Yesu alisema juu ya kazi ya kuhubiri. Alitabiri kama habari njema ingehubiriwa “katika dunia yote yenye kuikaliwa na watu ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14) Ule unabii uko natimia kabisa-kabisa leo. Ujumbe wa Ufalme uko nahubiriwa mu luga zaidi ya 1000, na kupitia site yetu jw.org, watu wengi mu dunia wanaweza kusikia ule ujumbe.

7 Lakini, Yesu aliambia pia wanafunzi wake kama ‘hawatamaliza kuzunguka miji,’ ao kuhubiria watu wote mbele akuje. (Mt. 10:23; 25:31-33) Mambo yenye Yesu alisema inaonekana pia leo. Mamilioni ya watu wanaishi mu maeneo yenye kazi ya kuhubiri imetiliwa vizuizi. Zaidi ya ile, kila dakika mamia ya watoto wanazaliwa. Tunafanya yetu yote ili kutangazia habari njema “kila taifa na kabila na luga na watu.” (Ufu. 14:6) Lakini hata tufanye nini hatutaweza kutangazia kila mutu habari njema mbele mwisho ufike.

8. Tunaweza kujiuliza ulizo gani juu ya namna Yehova atahukumu watu wakati wenye kuya? (Ona pia picha.)

8 Ile inatokeza hii ulizo: Itakuwa namna gani juu ya wale wenye hawatapata nafasi ya kusikia habari njema mbele taabu kubwa ianze? Yehova na Mwana wake, mwenye amepatia kazi ya kuhukumu, watawatendea namna gani? (Yoh. 5:19, 22, 27; Mdo. 17:31) Andiko ya musingi ya hii habari inasema kama Yehova “hataki mutu yeyote aharibiwe.” Lakini anataka “wote wafikie kutubu.” (2 Pe. 3:9; 1 Ti. 2:4) Hata kama tunajua ile yote, Yehova hayatufunulia namna atahukumu wale wenye hawakupata nafasi ya kusikia habari njema. Kwa kweli, halazimike kutuambia mambo yote yenye alishafanya na yenye atafanya.

Yehova atatendea namna gani wale wenye pengine hawakupata nafasi ya kusikia habari njema mbele taabu kubwa ianze? (Ona fungu ya 8) c


9. Yehova ametufunulia nini mu Biblia?

9 Mu Neno yake Biblia, Yehova ametufunulia mambo fulani yenye atafanya. Kwa mufano, Biblia inatuambia kama Yehova atafufua “wenye hawako wenye haki” wenye hawakupata nafasi ya kusikia habari njema na kubadilika. (Mdo. 24:15; Lu. 23:42, 43) Ile inatokeza maulizo ingine ya maana.

10. Tunaweza kujiuliza maulizo gani ingine?

10 Wote wenye watakufa wakati wa taabu kubwa hawatakuwa na tumaini ya kufufuliwa? Biblia inaonyesha kama wapinzani wenye Yehova na majeshi yake wataharibu ku vita ya Armagedoni, hawatafufuliwa. (2 Te. 1:6-10) Lakini, tuseme nini juu ya watu wengine, kwa mufano, wale wenye inawezekana watakufa kwa sababu ya magonjwa, uzee, aksida, ao wenye watauawa na wanadamu wenzao? (Muh. 9:11; Zek. 14:13) Wamoja wao wanaweza kuwa kati ya “wenye hawako wenye haki” wenye watafufuliwa mu dunia mupya? Hatujue.

MAMBO YENYE TUNAJUA

11. Wakati wa Armagedoni, hukumu itategemea nini?

11 Tunajua mambo mbalimbali kuhusu matukio ya wakati wenye kuya. Kwa mufano, tunajua kama ku Armagedoni, watu watahukumiwa kulingana na namna walitendea ndugu za Kristo. (Mt. 25:40) Wale wenye watahukumiwa kuwa kondoo, ni wale wenye waliunga mukono Wakristo watiwa-mafuta na Kristo. Tunajua pia kama ndugu fulani za Kristo watakuwa wangali ku dunia kisha taabu kubwa kuanza na wataenda mbinguni muda kidogo tu mbele ya Armagedoni. Muda wote wenye ndugu za Kristo watakuwa wangali ku dunia, itawezekana watu wenye moyo muzuri wapate nafasi ya kuwaunga mukono na kuunga mukono kazi yenye wako nafanya. (Mt. 25:31, 32; Ufu. 12:17) Juu ya nini ni jambo ya maana kujua vile?

12-13. Watu fulani wanaweza kutenda namna gani kisha kuona uharibifu wa “Babiloni Mukubwa”? (Ona pia picha.)

12 Hata kisha taabu kubwa kuanza, inawezekana kama watu fulani wenye wataona uharibifu wa “Babiloni Mukubwa” watakumbuka kama Mashahidi wa Yehova walizungumuzia ile tukio kwa muda murefu. Inawezekana wamoja kati ya wenye wataona ile matukio wabadilike?—Ufu. 17:5; Eze. 33:33.

13 Kama ile jambo inatokea itafanana na mambo yenye ilitokea mu Misri wakati wa Musa. Kumbuka kama “kikundi kikubwa cha watu wenye kuchangamana” kilijiunga na Waisraeli wakati walikuwa wanatoka Misri. Inawezekana wamoja kati ya wale watu walianza kuwa na imani wakati waliona mapigo kumi yenye Musa alitabiri. (Kut. 12:38) Kama jambo ya vile inatokea kisha uharibifu wa Babiloni Mukubwa, tutakasirika juu watu wanajiunga na siye wakati kidogo tu mbele mwisho ufike? Hapana! Tunapenda kuonyesha sifa za Baba yetu wa mbinguni, “Mungu mwenye rehema na huruma, hakasirike haraka na ni mwenye upendo mwingi mushikamanifu na kweli.” bKut. 34:6.

Watu fulani wenye wataona uharibifu wa “Babiloni Mukubwa” watakumbuka kama Mashahidi wa Yehova walizungumuzia ile tukio kwa muda murefu (Ona fungu ya 12-13) d


14-15. Uzima wa milele wa mutu unategemea kipindi yenye anakufa ao fasi kwenye anaishi? Fasiria. (Zaburi 33:4, 5)

14 Wakati fulani, tunasikiaka mutu anasema: “Itakuwa muzuri zaidi kama mutu wa familia yangu anakufa mbele taabu kubwa ianze juu kukuwe tumaini ya kumuona tena wakati wa ufufuo.” Wakati wanasema vile, hawakuwake na nia ya mubaya. Lakini kupata uzima wa milele haitegemee ni mu kipindi gani mutu anakufa. Yehova ni muamuzi mukamilifu, maamuzi yake ni yenye haki na yenye kuwa sawa. (Soma Zaburi 33:4, 5.) Tunaweza kuwa hakika kama “Muamuzi wa dunia yote” atafanya mambo yenye kuwa sawa.—Mwa. 18:25.

15 Inapatana pia na akili kusema kama kupata uzima wa milele ao hapana haitegemee fasi kwenye mutu anaishi. Mamilioni ya watu wanaishi mu maeneo kwenye hawapate nafasi ya kujifunza juu ya Ufalme, hatuwezi kuwazia kama Yehova atahukumu tu wale watu wote kuwa “mbuzi.” (Mt. 25:46) Muamuzi mwenye haki wa dunia yote anahangaikia sana wale watu kupita namna tunawahangaikia. Hatujue namna Yehova ataongoza matukio wakati wa taabu kubwa. Pengine watu fulani kati yao, watapata nafasi ya kujifunza juu ya Yehova, kumuamini na kuwa upande wake wakati atajitakasa mbele ya mataifa yote.—Eze. 38:16.

Kisha taabu kubwa kuanza, . . . inawezekana wamoja kati ya wenye wataona ile matukio wabadilike?

16. Kujifunza Biblia kumetusaidia kujua nini juu ya Yehova? (Ona pia picha.)

16 Kujifunza Biblia kumetusaidia kujua kama Yehova anaona uzima wa wanadamu kuwa wa maana sana. Alitoa Mwana wake ili siye wote tukuwe na tumaini ya kuishi milele. (Yoh. 3:16) Tumejionea siye wote namna Yehova ni mwenye upendo mwingi. (Isa. 49:15) Anajua kila mumoja wetu kwa jina. Anatujua muzuri sana, njo maana hata tukikufa anaweza kutufufua juu anakumbuka kila kitu juu yetu na mawazo yenye tulikuwa nayo! (Mt. 10:29-31) Bila shaka, tuko na sababu ya muzuri ya kuwa hakika kama Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo atahukumu kila mutu kwa njia kamilifu, juu ni mwenye hekima, mwenye haki na mwenye rehema.—Yak. 2:13.

Tunaweza kuwa hakika kama Yehova atahukumu kwa njia kamilifu kila mutu, juu ni mwenye hekima, mwenye haki na mwenye rehema (Ona fungu ya 16)


17. Tutazungumuzia nini mu habari yenye kufuata?

17 Hii mafasirio ya mupya inafanya kazi yetu ya kuhubiri ikuwe ya haraka sana kuliko wakati ingine yoyote. Juu ya nini tunasema vile? Na nini njo inatuchochea tuendelee kuhubiri habari njema bila kuacha? Tutazungumuzia majibu ya ile maulizo mu habari yenye kufuata.

WIMBO 76 Sema Vile Unajisikiaka

a Ili kujua juu ya nini tumefanya hii mabadiliko, soma habari “Hii ‘Ndiyo Njia Iliyokubaliwa Nawe’” mu Munara wa Mulinzi wa tarehe 15, Mwezi wa 3, 2015, uku. 7-11.

b Kisha Babiloni Mukubwa kuharibiwa, watumishi wote wa Yehova watajaribiwa wakati wa shambulio ya Gogu wa Magogu. Mutu yeyote mwenye atajiunga na watu wa Mungu kisha uharibifu wa Babiloni Mukubwa, atajaribiwa pia.

c MAFASIRIO YA PICHA: Hali tatu zenye kuonyesha sababu zenye pengine zinafanya watu fulani wasipate nafasi ya kuhubiriwa: (1) Mwanamuke mwenye kuishi mu eneo kwenye dini inafanya isikuwe salama kuhubiri, (2) bibi na bwana wenye kuishi mu eneo kwenye serikali inakataza kazi ya kuhubiri na ile inafanya ikuwe hatari kuhubiri, na (3) mwanaume mwenye kuishi mu eneo ya mbali sana kwenye ni nguvu sana kufika.

d MAFASIRIO YA PICHA: Kijana mwanamuke mwenye aliacha kweli anakumbuka mambo yenye alijifunza kuhusu uharibifu wa “Babiloni Mukubwa.” Anabadilika na anarudia kwa wazazi wake Wakristo. Kama mambo ya vile inatokea, tunaweza kufikiria sifa ya rehema na huruma ya Baba yetu wa mbinguni na kufurahi juu mutenda zambi amerudia.