MAKALA YA 19

WIMBO 22 Ufalme Umesimamishwa—Na Uje!

Tunajua Nini Kuhusu Hukumu za Yehova za Wakati Ujao?

Tunajua Nini Kuhusu Hukumu za Yehova za Wakati Ujao?

“Yehova . . . hataki yeyote aangamizwe.”2 PET. 3:9.

JAMBO KUU

Tunaweza kuwa na uhakika kwamba hukumu za Yehova za wakati ujao zitakuwa za uadilifu na haki.

1. Kwa nini tunaweza kusema kwamba tunaishi katika kipindi chenye kusisimua?

 TUNAISHI katika kipindi chenye kusisimua! Kila siku, tunajionea unabii wa Biblia ukitimizwa. Kwa mfano, tunajionea “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” wakishindana kwa sababu kila mmoja anataka kuutawala ulimwengu. (Dan. 11:​40, maelezo ya chini) Tunajionea habari njema ya Ufalme wa Mungu ikihubiriwa sasa kuliko wakati mwingine wowote, na mamilioni ya watu wanaitikia vizuri. (Isa. 60:22; Mt. 24:14) Na tunapata chakula kingi cha kiroho “kwa wakati unaofaa.”—Mt. 24:​45-47.

2. Tunaweza kuwa na uhakika kuhusu nini, lakini ni lazima tutambue nini?

2 Yehova anaendelea kutusaidia kuelewa vizuri zaidi kuhusu matukio makubwa ambayo yatatokea hivi karibuni. (Met. 4:18; Dan. 2:28) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba kufikia wakati ambapo dhiki kuu itaanza, tutajua kila kitu tunachohitaji kujua ili tuvumilie kwa uaminifu na hata tuendelee kuwa na umoja katika kipindi hicho kigumu. Hata hivyo, ni lazima tutambue kwamba kuna baadhi ya mambo kuhusu wakati ujao ambayo hatuyajui. Katika makala hii, kwanza tutazungumzia kwa nini tumerekebisha uelewaji wetu kuhusu baadhi ya matukio hayo. Kisha, tutachunguza upya baadhi ya mambo ambayo tunajua kuhusu wakati ujao na jinsi Baba yetu wa mbinguni atakavyotenda.

MAMBO AMBAYO HATUJUI

3. Zamani tulisema nini kuhusu wakati ambapo Yehova angeondoa fursa ya watu kujiunga nasi, na kwa nini tulifikia mkataa huo?

3 Zamani, tulisema kwamba mara tu dhiki kuu itakapoanza, watu wote wasioamini hawatakuwa tena na fursa ya kuchukua msimamo upande wa Yehova na kuokoka Har–​Magedoni. Tulifikia mkataa huo kwa sababu tulielewa kwamba simulizi la Gharika lilikuwa mfano au ufananisho wa kinabii. Kwa mfano, tulifikiri kwamba kama tu ambavyo Yehova alifunga mlango wa safina kabla ya Gharika kuanza, ndivyo ambavyo ‘ataufungia mlango’ mfumo wa mambo wa Shetani mwanzoni mwa dhiki kuu, na hivyo kuzuia watu wengine zaidi kuokolewa.—Mt. 24:​37-39.

4. Je, sasa tunaona simulizi la Gharika kuwa ufananisho wa kinabii? Eleza.

4 Je, tunapaswa kuona simulizi la Gharika kuwa ufananisho wa kinabii? Jibu ni hapana. Kwa nini? Kwa sababu hakuna msingi wa Kimaandiko wa kuunga mkono jambo hilo. a Yesu alilinganisha “siku za Noa” na wakati wa kuwapo kwake, lakini hakumaanisha kwamba simulizi la Gharika lilikuwa ufananisho wa kinabii, yaani, kila mtu na kila tukio katika Gharika lingekuwa ufananisho wa jambo ambalo lingekuja kutimizwa; wala hakusema kwamba kufungwa kwa mlango wa safina kulikuwa na maana yoyote ya kinabii. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba hatuwezi kujifunza jambo lolote kutokana na simulizi la Noa na Gharika.

5. (a) Noa alifanya nini kabla ya Gharika? (Waebrania 11:7; 1 Petro 3:20) (b) Inapohusu kazi ya kuhubiri, hali zetu leo zinafananaje na zile za siku za Noa?

5 Noa aliposikia ujumbe wa onyo kutoka kwa Yehova, alithibitisha kwamba ana imani kwa kujenga safina. (Soma Waebrania 11:7; 1 Petro 3:20.) Vivyo hivyo, watu wanaosikia habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu wanapaswa kutenda kulingana na mambo wanayosikia. (Mdo. 3:​17-20) Petro alimwita Noa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Pet. 2:5) Hata hivyo, kama tulivyozungumzia kwenye makala iliyotangulia, hatujui ikiwa Noa alipanga kampeni ya kuhubiri ili kuwafikia watu wote duniani kabla ya Gharika kuja. Leo, tunashiriki katika kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote, na tunajitahidi kufanya hivyo kwa bidii. Ingawa hivyo, hata tujitahidi kadiri gani, hatuwezi kumfikia kila mtu duniani na kumhubiria habari njema kabla ya mwisho kuja. Kwa nini?

6-7. Kwa nini tunaweza kufikia mkataa kwamba hatutaweza kumfikia kila mtu duniani ili kumhubiria habari njema kabla ya mwisho kuja? Eleza.

6 Fikiria kile ambacho Yesu alisema kuhusu ukubwa wa kazi yetu ya kuhubiri. Alitabiri kwamba habari njema ingehubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14) Unabii huo unatimizwa leo kuliko wakati mwingine wowote. Ujumbe wa Ufalme unapatikana katika lugha zaidi ya 1,000, na kupitia tovuti ya jw.org, idadi kubwa ya watu duniani wanaweza kupata ujumbe huo.

7 Hata hivyo, Yesu aliwaambia wanafunzi wake pia kwamba “hawangemaliza kuzunguka majiji” au kumhubiria kila mtu kabla ya kufika kwake. (Mt. 10:23; 25:​31-33) Hivyo, hatutamhubiria kila mtu kibinafsi kabla ya kufika kwa Yesu ili kuwahukumu wanadamu. Leo, mamilioni ya watu wanaishi katika maeneo ambayo hatuwezi kuhubiri kwa uhuru. Kwa kuongezea, kila dakika mamia ya watoto wanazaliwa. Tunajitahidi kadiri tuwezavyo kuwahubiria habari njema watu katika “kila taifa na kabila na lugha.” (Ufu. 14:6) Lakini ukweli ni kwamba hatutaweza kumhubiria habari njema kila mtu kibinafsi kabla ya mwisho kuja.

8. Ni swali gani ambalo huenda tukajiuliza kuhusu hukumu za Yehova za wakati ujao? (Tazama pia picha.)

8 Hivyo, huenda tukajiuliza: Namna gani kuhusu watu ambao huenda hawatapata nafasi ya kusikia habari njema kabla ya dhiki kuu kuanza? Yehova na Mwana wake ambaye amemweka rasmi afanye kazi ya kuhukumu, watashughulikaje na kila mmoja wao? (Yoh. 5:​19, 22, 27; Mdo. 17:31) Andiko la msingi la makala hii linasema kwamba Yehova “hataki yeyote aangamizwe.” Badala yake, anataka “wote wafikie toba.” (2 Pet. 3:9; 1 Tim. 2:4) Ingawa tunajua jambo hilo kumhusu Yehova, ni lazima tutambue kwamba bado Yehova hajafunua jinsi atakavyowahukumu watu ambao hawakupata nafasi ya kusikia habari njema kabla ya dhiki kuu kuanza. Bila shaka, Yehova hawajibiki kutueleza kuhusu kila kitu ambacho amefanya au atakachofanya.

Yehova atashughulikaje na watu ambao huenda hawatapata nafasi ya kusikia habari njema kabla ya dhiki kuu kuanza? (Tazama fungu la 8) c


9. Yehova ametufunulia nini katika Biblia?

9 Yehova amefunua katika Neno lake baadhi ya mambo ambayo atafanya. Kwa mfano, Biblia inatueleza kwamba Yehova atawafufua watu “wasio waadilifu” ambao hawakupata nafasi ya kuhubiriwa habari njema na kubadili njia zao kabla ya kufa. (Mdo. 24:15; Luka 23:​42, 43) Hilo linatokeza maswali mengine muhimu.

10. Ni maswali gani mengine yanayojitokeza?

10 Je, watu wote watakaokufa wakati wa matukio ya dhiki kuu wataangamizwa milele bila kuwa na tumaini la ufufuo? Maandiko yanaonyesha wazi kwamba wale wanaompinga Yehova moja kwa moja na ambao yeye na majeshi yake watawaangamiza katika Har–​Magedoni hawatafufuliwa. (2 The. 1:​6-10) Lakini vipi kuhusu watu wengine, kwa mfano, wale ambao huenda watakufa kwa sababu ya magonjwa au uzee, au kutokana na aksidenti, au wale watakaouawa na wanadamu wengine? (Mhu. 9:11; Zek. 14:13) Je, inawezekana kwamba baadhi ya watu hao watakuwa miongoni mwa watu “wasio waadilifu” ambao watafufuliwa katika dunia mpya? Hatujui.

MAMBO AMBAYO TUNAJUA

11. Watu watahukumiwa kwa msingi gani wakati wa Har–​Magedoni?

11 Tunajua mambo kadhaa kuhusu matukio ya wakati ujao. Kwa mfano, tunajua kwamba wakati wa Har–​Magedoni watu watahukumiwa kwa kutegemea jinsi walivyowatendea ndugu za Kristo. (Mt. 25:40) Wale watakaohukumiwa kuwa kondoo watakuwa wameonyesha kwamba wanawaunga mkono watiwa-mafuta na Kristo. Pia, tunajua kwamba baadhi ya ndugu za Kristo bado watakuwa duniani baada ya dhiki kuu kuanza na hawatachukuliwa kwenda mbinguni hadi muda mfupi kabla ya vita vya Har–​Magedoni kuanza. Maadamu ndugu za Kristo bado wako duniani, kuna uwezekano kwamba watu wenye mioyo minyoofu watapata nafasi ya kuwaunga mkono na kuunga mkono kazi wanayofanya. (Mt. 25:​31, 32; Ufu. 12:17) Kwa nini habari hizo ni muhimu?

12-13. Huenda baadhi ya watu watatendaje watakapoona “Babiloni Mkubwa” akiharibiwa? (Tazama pia picha.)

12 Hata baada ya dhiki kuu kuanza, inawezekana kwamba baadhi ya watu watakaoona kuharibiwa kwa “Babiloni Mkubwa” watakumbuka kuwa Mashahidi wa Yehova walisema kwamba jambo hilo lingetukia. Je, baadhi ya watu watakaoona matukio hayo watabadili njia zao na kujiunga na watu wa Yehova?—Ufu. 17:5; Eze. 33:33.

13 Jambo hilo likitukia, itakuwa sawa na jambo lililotukia Misri katika siku za Musa. Kumbuka kwamba “kundi kubwa lenye mchanganyiko wa watu” lilijiunga na Waisraeli walipoondoka Misri. Huenda baadhi ya watu hao walianza kusitawisha imani walipoona mambo ambayo Musa alionya kuhusu yale Mapigo Kumi yakitimia. (Kut. 12:38) Ikiwa hali itakuwa hivyo baada ya kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa, je, tutaona kuwa si jambo la haki kwamba watu waliweza kujiunga nasi muda mfupi kabla ya mwisho kufika? Bila shaka, la! Tunataka kumwiga Baba yetu wa mbinguni ambaye ni “Mungu mwenye rehema na huruma, si mwepesi wa hasira, [na ana] upendo mwingi mshikamanifu na kweli.” bKut. 34:6.

Baadhi ya watu watakaoona “Babiloni Mkubwa” akiharibiwa watakumbuka kuwa Mashahidi wa Yehova walisema kwamba jambo hilo lingetukia (Tazama fungu la 12-13) d


14-15. Je, wakati ujao wa milele wa mtu unategemea atakufa wakati gani au mahali anapoishi? Eleza. (Zaburi 33:​4, 5)

14 Nyakati fulani, ndugu au dada yetu huenda akasema hivi kuhusu mtu wa ukoo ambaye hamtumikii Yehova: “Ingekuwa bora zaidi ikiwa mtu wangu wa ukoo angekufa kabla ya dhiki kuu kuanza ili awe na tumaini la kufufuliwa.” Bila shaka maneno hayo yanasemwa kwa nia nzuri. Lakini wakati ujao wa milele wa mtu hautegemei anakufa wakati gani. Yehova ni Mwamuzi mkamilifu—anafanya maamuzi kwa uadilifu na haki. (Soma Zaburi 33:​4, 5.) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba “Mwamuzi wa dunia yote” atatenda jambo la haki.—Mwa. 18:25.

15 Pia, inafaa kufikia mkataa kwamba wakati ujao wa milele wa mtu hautegemei mahali anapoishi. Yehova hawezi kamwe kuwahukumu mamilioni ya watu kuwa “mbuzi” kwa sababu tu wanaishi katika nchi ambazo hawakuwa na fursa ya kusikia ujumbe wa Ufalme. (Mt. 25:46) Mwamuzi wa dunia yote ambaye ni mwadilifu anawajali watu hao kuliko hata sisi tunavyowajali. Hatujui jinsi Yehova atakavyoongoza mambo wakati wa dhiki kuu. Huenda baadhi ya watu hao watapata nafasi ya kujifunza kumhusu Yehova, kuonyesha imani kwake, na kuchukua msimamo upande wa Yehova atakapojitakasa mwenyewe mbele ya mataifa yote.—Eze. 38:16.

Baada ya dhiki kuu kuanza, . . . je, baadhi ya watu watakaoona matukio hayo watabadili njia zao na kujiunga na watu wa Yehova?

16. Tumejifunza nini kumhusu Yehova? (Tazama pia picha.)

16 Kupitia funzo letu la Biblia, tumejua jinsi Yehova anavyothamini uhai wa mwanadamu. Alimtoa Mwana wake kuwa dhabihu ili sisi sote tuweze kuwa na tumaini la kuishi milele. (Yoh. 3:16) Sote tumehisi upendo mwororo wa Yehova. (Isa. 49:15) Anamjua kila mmoja wetu kwa jina. Kwa kweli, anamjua vizuri sana kila mmoja wetu hivi kwamba ikiwa tutakufa anaweza kutufufua kwa sababu anakumbuka kila kitu kutuhusu na kumbukumbu zetu zote tulizokuwa nazo! (Mt. 10:​29-31) Bila shaka, tuna kila sababu ya kuwa na uhakika kwamba Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo atamhukumu kila mtu kwa ukamilifu kwa sababu yeye ni mwenye usawaziko, mwadilifu, na mwenye rehema.—Yak. 2:13.

Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atamhukumu kila mtu kwa ukamilifu kwa sababu yeye ni mwenye usawaziko, mwadilifu, na mwenye rehema (Tazama fungu la 16)


17. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

17 Marekebisho hayo katika uelewaji wetu yanafanya kazi yetu ya kuhubiri iwe yenye uharaka zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Na ni nini kinachotuchochea kuendelea kuhubiri kwa bidii habari njema bila kuacha? Tutazungumzia majibu ya maswali hayo kwa kina katika makala inayofuata.

WIMBO 76 Unahisije?

a Kwa maelezo zaidi kuhusu kwa nini mabadiliko haya yamefanywa, tazama makala yenye kichwa ‘Hii Ndiyo Njia Unayoikubali’ katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 2015, uku. 7-11.

b Baada ya kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa, kila mtumishi wa Yehova atajaribiwa wakati wa shambulio la Gogu wa Magogu. Mtu yeyote atakayejiunga na watu wa Mungu baada ya Babiloni Mkubwa kuharibiwa, naye pia atajaribiwa.

c MAELEZO YA PICHA: Picha tatu zinazoonyesha kwa nini huenda baadhi ya watu hawafikiwi na kazi yetu ya kuhubiri ya ulimwenguni pote: (1) Mwanamke anayeishi katika nchi ambayo dini kuu inafanya isiwe salama kuhubiri, (2) wenzi wa ndoa wanaoishi katika nchi ambayo mfumo wao wa kisiasa unafanya kazi yetu ya kuhubiri isiwe halali kisheria na iwe hatari kuhubiri, na (3) mwanamume anayeishi katika eneo la mbali sana ambalo si rahisi kufika.

d MAELEZO YA PICHA: Mwanamke kijana ambaye aliacha kweli anakumbuka mambo aliyojifunza kuhusu kuharibiwa kwa “Babiloni Mkubwa.” Anabadili njia zake na kurudi kwa wazazi wake Wakristo. Ikiwa hali hiyo itatukia, tungependa kumwiga Baba yetu wa mbinguni mwenye rehema na huruma na kushangilia kwamba mtenda dhambi amerudi.