Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 26

WIMBO 8 Yehova Ni Kimbilio Letu

Mfanye Yehova Kuwa Mwamba Wako

Mfanye Yehova Kuwa Mwamba Wako

“Hakuna mwamba kama Mungu wetu.”1 SAM. 2:2.

JAMBO KUU

Jifunze sifa zinazofanya Yehova awe kama mwamba kwetu na jinsi tunavyoweza kuiga sifa hizo.

1. Kama ilivyorekodiwa katika Zaburi 18:​46, Daudi anamlinganisha Yehova na nini?

 TUNAISHI katika ulimwengu ambao tunakabili changamoto zisizotarajiwa zinazoweza kuvuruga—au hata kubadili kabisa—maisha yetu. Tunashukuru sana kwamba tunaweza kumtegemea Yehova Mungu atusaidie! Katika makala iliyotangulia, tulikumbushwa kwamba Yehova ni Mungu aliye hai na sikuzote yuko tayari kutusaidia. Tunapopata msaada wake, hilo linatuhakikishia kwamba “Yehova yuko hai!” (Soma Zaburi 18:46.) Hata hivyo, baada tu ya kusema maneno hayo, Daudi alimwita Mungu “Mwamba wangu.” Kwa nini alimlinganisha Yehova, Mungu aliye hai, na kitu kisicho hai, yaani, mwamba?

2. Kwa nini tunapaswa kupendezwa na wazo la kwamba Daudi alimwita Yehova “Mwamba wangu”?

2 Katika makala hii, tutachunguza kwa nini Yehova anarejelewa kuwa kama mwamba na kile ambacho ufafanuzi huo unatufundisha kumhusu. Pia, tutajifunza jinsi tutakavyoweza kumtegemea akiwa Mwamba wetu. Mwishowe, tutazungumzia njia tunazoweza kuiga sifa za Yehova zilizo kama mwamba.

KWA NINI YEHOVA ANAITWA MWAMBA?

3. Mara nyingi Biblia inatumiaje neno “mwamba”? (Tazama picha.)

3 Biblia inatumia neno “mwamba” kama lugha ya picha inayotusaidia kuelewa baadhi ya sifa za Yehova. Mara nyingi, watumishi wa Yehova wanaotajwa katika Biblia wanapomsifu Mungu kwa sababu ya sifa zake nzuri, wanamrejelea kuwa kama mwamba. Katika Biblia, sehemu ya kwanza inayomrejelea Yehova kuwa “Mwamba” inapatikana kwenye Kumbukumbu la Torati 32:4. Hana alisema hivi katika sala yake: “Hakuna mwamba kama Mungu wetu.” (1 Sam. 2:2) Habakuki alimwita Yehova “Mwamba wangu.” (Hab. 1:12) Mwandishi wa Zaburi ya 73 alimwita Mungu, “mwamba wa moyo wangu.” (Zab. 73:26) Na hata Yehova mwenyewe alijiita Mwamba. (Isa. 44:8) Acheni tuzungumzie sifa tatu zinazofanya Yehova awe kama mwamba na tujifunze jinsi tunavyoweza kumfanya kuwa “Mwamba wetu.”Kum. 32:31.

Watu wa Mungu humwona Yehova kuwa Mwamba salama (Tazama fungu la 3)


4. Yehova ni kimbilio letu jinsi gani? (Zaburi 94:22)

4 Yehova ni kimbilio. Kama vile tu mwamba mkubwa unavyoweza kuwa mahali pa kujificha kutokana na dhoruba kubwa, ndivyo Yehova anavyoweza kutulinda kutokana na hali zenye kutisha maishani mwetu. (Soma Zaburi 94:22.) Anatulinda na kutuepusha na madhara ya kudumu. Na anaahidi kufanya mambo mengi hata zaidi. Hatimaye, ataondoa jambo lolote linalotishia amani na usalama wetu.—Eze. 34:​25, 26.

5. Yehova anawezaje kuwa kimbilio letu, kama Mwamba?

5 Njia moja ambayo tunaweza kumfanya Yehova kuwa Kimbilio letu, kama mwamba, ni kwa kusali kwake. Tunaposali, Yehova anatupatia “amani ya Mungu” ambayo inalinda moyo wetu na akili zetu. (Flp. 4:​6, 7) Fikiria mfano wa Artem, ndugu aliyefungwa kwa sababu ya imani yake. Alihojiwa mara kwa mara na mpelelezi mkali ambaye alimshinikiza na kumdhalilisha. Artem anasema hivi: “Nilikuwa na wasiwasi kila mara mpelelezi huyo aliponiita. . . . Sikuzote nilisali kwa Yehova. Nilimwomba anisaidie niwe mtulivu na mwenye hekima. Mbinu za mpelelezi huyo hazikufanikiwa. . . . Kwa msaada wa Yehova, ni kana kwamba nilikuwa nimesimama nyuma ya ukuta wa mawe.”

6. Kwa nini tunaweza kumtegemea Yehova sikuzote? (Isaya 26:​3, 4)

6 Yehova anategemeka. Kama mwamba ambao ni imara na hauwezi kuhama, sikuzote Yehova anapatikana na yuko tayari kutusaidia. Tunaweza kumtumaini kwa sababu yeye ni “Mwamba wa milele.” (Soma Isaya 26:​3, 4.) Sikuzote yuko hai ili kutimiza ahadi zake, kusikiliza sala zetu, na kutupatia msaada tunaohitaji. Pia, tunaweza kumtegemea Yehova kwa sababu yeye ni mshikamanifu kwa wale wanaomtumikia. (2 Sam. 22:26) Hatasahau kamwe mambo tunayofanya, na sikuzote atatuthawabisha.—Ebr. 6:10; 11:6.

7. Tunanufaikaje tunapomtegemea Yehova? (Tazama pia picha.)

7 Tunamfanya Yehova kuwa Mwamba wetu tunapomtegemea kikamili. Tunaamini kwamba tutanufaika kwa kumtii yeye, hata hali zinapokuwa ngumu. (Isa. 48:​17, 18) Tunapojionea utegemezo wake, uhakika wetu kwake utaimarika. Kisha, tutakuwa tumejitayarisha vizuri ili kukabiliana na majaribu ambayo ni Yehova tu anayeweza kutusaidia kuyashinda. Mara nyingi tunapokabili hali ambayo hakuna anayeweza kutusaidia, hapo ndipo tunapotambua jinsi Yehova anavyotegemeka. Vladimir anasema hivi: “Muda niliokuwa gerezani ulikuwa kipindi bora zaidi kilichoimarisha uhusiano wangu na Mungu. Nilijifunza kumtumaini Yehova kikamili zaidi kwa sababu nilikuwa peke yangu na sikuwa na uwezo wa kubadili hali hiyo.”

Tunamfanya Yehova kuwa Mwamba wetu tunapomtegemea kikamili (Tazama fungu la 7)


8. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova habadiliki? (b) Tunanufaikaje kwa kumfanya Mungu awe Mwamba wetu? (Zaburi 62:​6, 7)

8 Yehova ni imara na habadiliki. Kama mwamba mkubwa, Yehova ni imara na habadiliki. Utu wake na kusudi lake haliwezi kamwe kubadilika. (Mal. 3:6) Adamu na Hawa walipomwasi, Yehova hakubadili kusudi lake kwa wanadamu. Kama mtume Paulo alivyoandika, Yehova “hawezi kujikana mwenyewe.” (2 Tim. 2:13) Hilo linamaanisha kwamba hata nini kitokee au wengine wafanye nini, Yehova hawezi kamwe kubadili sifa zake, kusudi lake, au viwango vyake. Tukiwa na uhakika katika Mungu wetu ambaye ni imara na habadiliki, tunaweza kumtegemea atuokoe na kutusaidia tunapokabili hali ngumu.—Soma Zaburi 62:​6, 7.

9. Tunajifunza nini kutokana na kisa cha Tatyana?

9 Tunamfanya Yehova kuwa Mwamba wetu kwa kukazia akilini na kutafakari utu wake na kusudi lake. Kufanya hivyo kutatusaidia kuendelea kuwa watulivu na washikamanifu kwake wakati wa majaribu. (Zab. 16:8) Ilikuwa hivyo kwa dada anayeitwa Tatyana, ambaye alihukumiwa kifungo cha nyumbani kwa sababu ya imani yake. Anasema hivi: “Nilijipata peke yangu. Mwanzoni, hali hiyo ilikuwa ngumu sana. Nilivunjika moyo mara nyingi.” Hata hivyo, alipotambua jinsi jaribu lake lilivyohusiana na Yehova na kusudi lake, aliweza kukabiliana nalo na alipata utulivu na nguvu za kuendelea kuwa mwaminifu. Anasema hivi: “Kutafakari kwa nini hali hiyo ilikuwa ikitokea, kulinisaidia kukumbuka kwamba nilikuwa nikipitia hali hiyo kwa sababu ninampenda Yehova na ninataka kumpendeza. Hilo lilinisaidia kuacha kujihurumia sana.”

10. Tunawezaje kumfanya Yehova awe Mwamba wetu leo?

10 Hivi karibuni, tutakabili majaribu ambayo yatahitaji tumtegemee Yehova zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Sasa ni wakati wa kuendelea kuimarisha uhakika wetu kwamba Yehova ataendelea kutupatia chochote tunachohitaji ili tuvumilie kwa uaminifu. Unawezaje kufanya hivyo? Soma masimulizi ya Biblia na masimulizi ya watumishi wa Yehova leo. Tambua jinsi ambavyo Mungu ameonyesha sifa zilizo kama mwamba ili kuwategemeza watumishi wake. Tafakari kwa kina kuhusu masimulizi hayo. Kufanya hivyo, kutakusaidia kumfanya Yehova awe Mwamba wako.

IGA SIFA ZA YEHOVA ZILIZO KAMA MWAMBA

11. Kwa nini tungependa kuiga sifa za Yehova zilizo kama mwamba? (Tazama pia sanduku “ Lengo kwa Ajili ya Ndugu Vijana.”)

11 Tumetambua jinsi ambavyo Yehova amethibitika kuwa kama mwamba. Sasa tuchunguze jinsi tunavyoweza kuiga sifa zake zilizo kama mwamba. Tunapojitahidi kufanya hivyo, ndivyo tutakavyofanikiwa zaidi kulijenga kutaniko. Kwa mfano, Yesu alimpa Simoni jina Kefa (linalotafsiriwa kuwa “Petro”), linalomaanisha “Kipande cha Mwamba.” (Yoh. 1:42) Jina hilo lilionyesha kwamba angekuwa chanzo cha faraja na angeliimarisha kutaniko. Wazee wa kutaniko wanafafanuliwa kuwa “kivuli cha jabali kubwa.” Hilo linaonyesha jinsi wanavyowalinda wale walio katika kutaniko. (Isa. 32:2) Bila shaka, kutaniko linanufaika—ndugu na dada wote—wanapoiga sifa za Yehova zilizo kama mwamba.—Efe. 5:1.

12. Eleza njia ambazo tunaweza kuwa kimbilio kwa wengine.

12 Uwe kimbilio. Nyakati fulani, huenda tukawa kimbilio halisi kwa ndugu zetu waliokumbwa na majanga ya asili, misukosuko ya kijamii, au vita. Kadiri hali katika “siku za mwisho” zinavyozidi kuwa mbaya, bila shaka tutakuwa na fursa nyingi za kusaidiana. (2 Tim. 3:1) Pia, tunaweza kuwasaidia ndugu zetu kihisia na kiroho. Njia moja tunayoweza kufanya hivyo ni kwa kuwafanya wahisi wamekaribishwa wanapofika kwenye Jumba la Ufalme, na hilo litachangia mazingira yenye urafiki kutanikoni. Tunaishi katika ulimwengu uliojaa watu wakali, wenye ubaridi, na wanaotusababishia mkazo. Hivyo, ndugu na dada wanapohudhuria mikutano, tungependa kufanya yote tuwezayo kuwafanya wahisi wanapendwa, wanaburudishwa, na wako salama.

13. Wazee wanawezaje kuwa kimbilio kwa ndugu na dada wanaokabili hali ngumu? (Tazama pia picha.)

13 Wazee wanaweza kuwa kimbilio kutanikoni kwa wale wanaokabili dhoruba halisi au za mfano. Kunapokuwa na majanga ya asili au dharura za kitiba, wazee wanachukua hatua ya kwanza kupanga na kutoa msaada hususa. Pia, wanatoa msaada wa kiroho. Ndugu na dada watakuwa tayari kumfikia mzee ikiwa anajulikana kuwa mpole, mwenye huruma, na yuko tayari kusikiliza. Sifa kama hizo zitawasaidia kuhisi kwamba wanapendwa; hivyo, itakuwa rahisi zaidi kwao kutumia mwongozo unaotegemea Biblia ambao huenda mzee akatoa.—1 The. 2:​7, 8, 11.

Dhoruba halisi na za mfano zinapowaathiri wale walio katika kutaniko, wazee wanakuwa kimbilio kwao (Tazama fungu la 13) a


14. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunategemeka?

14 Uwe mwenye kutegemeka. Tungependa wengine waweze kututegemea, hasa wanapokabili hali ngumu. (Met. 17:17) Tunawezaje kusitawisha sifa ya kuwa wenye kutegemeka? Tunaweza kujitahidi kuonyesha sifa za Yehova kila siku, kama vile kutimiza ahadi tunazotoa na kujitahidi kufanya mambo kwa wakati. (Mt. 5:37) Tunaweza pia kutoa msaada hususa unapohitajika. Zaidi ya hayo, tunahakikisha tunatimiza migawo yetu kulingana na maagizo tunayopokea.

15. Kutaniko linanufaikaje wazee wanapokuwa wenye kutegemeka?

15 Wazee wanaotegemeka wanalinufaisha kutaniko. Jinsi gani? Wahubiri wanahisi wanategemezwa wanapojua kwamba wanapohitaji msaada wanaweza kuwasiliana kwa urahisi na wazee, kama vile mwangalizi wao wa kikundi cha utumishi. Pia, wahubiri wanahisi wanapendwa wanapojua kwamba wazee wako tayari kuwasaidia. Na wazee wanapotoa ushauri unaotegemea Neno la Mungu na machapisho ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, na si maoni yao, waabudu wenzao watawatumaini. Pia, ndugu na dada wanawatumaini wazee wanaotunza siri kuhusu mambo ya kibinafsi na kutimiza mambo waliyoahidi kufanya.

16. Tunapokuwa imara tunanufaikaje na tunawanufaishaje wengine?

16 Uwe imara. Tunaweza kuwa mfano mzuri kwa wengine ikiwa tutashikamana na mambo yaliyo sawa na ikiwa tutafanya maamuzi yanayotegemea kabisa kanuni za Biblia. Tunavyozidi kukua katika imani na ujuzi sahihi, tunakuwa imara zaidi katika kweli. Hatutakuwa wenye kusitasita, tusio imara, au kupotoshwa kwa urahisi na mafundisho ya uwongo na njia ya kufikiri ya ulimwengu huu. (Efe. 4:14; Yak. 1:​6-8) Imani yetu katika Yehova na ahadi zake itatusaidia kuendelea kuwa na usawaziko tunapopokea habari mbaya. (Zab. 112:​7, 8) Pia, tutaweza kuwasaidia wale ambao wanakabili majaribu.—1 The. 3:​2, 3.

17. Ni mambo gani yatakayowasaidia wazee wawaimarishe wengine?

17 Wazee wanapaswa kuwa wenye kiasi katika mazoea, wenye utimamu wa akili, utaratibu, na usawaziko. Wanaume hao wanawaimarisha wengine na kulitia nguvu kutaniko kwa ‘kufuata kikamili neno la uaminifu.’ (Tito 1:9; 1 Tim. 3:​1-3) Kupitia mfano wao na ziara za uchungaji, wazee huwasaidia wahubiri wahudhurie mikutano, wahubiri, na wawe na funzo la kibinafsi kwa ukawaida. Ndugu na dada wanapopata matatizo yanayowahangaisha, wazee wanaweza kutimiza mengi kwa kuwatia moyo waendelee kumkazia fikira Yehova na ahadi zake.

18. Kwa nini tunataka kumsifu Yehova na kumkaribia zaidi na zaidi? (Tazama pia sanduku “ Njia ya Kumkaribia Zaidi Yehova.”)

18 Baada ya kuchunguza sifa nzuri sana za Yehova, tunaweza kusema kama Mfalme Daudi aliyesema hivi: “Yehova, Mwamba wangu, na asifiwe.” (Zab. 144:1) Sikuzote tunaweza kumtegemea Yehova. Katika maisha yetu yote, hata tunapozeeka, tunaweza kuwa na sababu ya kutangaza hivi: “Yeye ni Mwamba wangu,” tukiwa na uhakika kwamba sikuzote atatusaidia kunawiri kiroho.—Zab. 92:​14, 15.

WIMBO 150 Mtafute Mungu Upate Ukombozi

a MAELEZO YA PICHA: Akiwa kwenye Jumba la Ufalme, dada anawafikia wazee wawili kwa uhuru.