Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 23

WIMBO 28 Kuwa Rafiki ya Yehova

Mwaliko wa Pekee wa Yehova wa Kuwa Wageni Wake

Mwaliko wa Pekee wa Yehova wa Kuwa Wageni Wake

“Hema langu litakuwa pamoja nao, nami nitakuwa Mungu wao.”EZE. 37:27.

JAMBO KUU

Kuongeza uthamini wetu kwa mwaliko wa Yehova wa kuwa wageni kwenye hema lake la mfano na kwa jinsi anavyotutunza akiwa Mwenyeji wetu.

1-2. Yehova anawapatia waabudu wake washikamanifu mwaliko gani?

 YEHOVA ana sehemu gani maishani mwako? Huenda ukasema hivi: ‘Yehova ni Baba yangu, Mungu wangu, na Rafiki yangu.’ Pia, kuna majina mengine ya cheo ambayo unaweza kutumia inapomhusu Yehova. Hata hivyo, je, unamwona pia akiwa Mwenyeji wako?

2 Mfalme Daudi alilinganisha urafiki uliopo kati ya Yehova na waabudu wake washikamanifu na uhusiano kati ya mwenyeji na wageni wake. Daudi aliuliza hivi: “Ee Yehova, ni nani anayeweza kuwa mgeni katika hema lako? Ni nani anayeweza kukaa katika mlima wako mtakatifu?” (Zab. 15:1) Kutokana na maneno hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu, tunajifunza kwamba tunaweza kuwa wageni wa Yehova, yaani, rafiki zake. Je, huo si mwaliko wa pekee kutoka kwa Yehova?

YEHOVA ANATAKA TUWE WAGENI WAKE

3. Mgeni wa kwanza wa Yehova alikuwa nani, na Yehova alihisije kuhusu mgeni wake, na mgeni huyo alihisije kumhusu Yehova?

3 Kabla ya uumbaji, Yehova alikuwa peke yake. Lakini baada ya muda fulani, alimwalika Mwana wake mzaliwa wa kwanza kwenye hema lake la mfano. Yehova alifurahia sana jukumu lake jipya akiwa Mwenyeji wake. Biblia inafunua kwamba Yehova ‘alimpenda sana’ Mwana wake. Naye, akiwa mgeni wake wa kwanza, ‘alishangilia mbele za Yehova wakati wote.’—Met. 8:30.

4. Yehova alipanuaje mipaka ya hema lake hatua kwa hatua?

4 Kisha, Yehova aliwaumba viumbe wengine wa roho, na kuwaalika wawe wageni wake pia. Malaika wake wanaitwa ‘wana wa Mungu,’ nao wanafafanuliwa kuwa wenye furaha wakiwa mbele za Yehova. (Ayu. 38:7; Dan. 7:10) Kwa kipindi fulani, viumbe waliokuwa na urafiki pamoja na Mungu ni wale tu waliokuwa mbinguni, mahali anapoishi. Baadaye, alipanua mipaka ya hema lake ili kuwaalika pia wanadamu duniani. Baada ya muda, Enoko, Noa, Abrahamu, na Ayubu walikuwa miongoni mwa watu waliopata kibali chake. Waabudu hao wa kweli walifafanuliwa kuwa rafiki za Mungu, au wale waliotembea pamoja “na Mungu wa kweli.”—Mwa. 5:24; 6:9; Ayu. 29:4; Isa. 41:8.

5. Tunajifunza nini kutokana na unabii unaopatikana kwenye Ezekieli 37:26, 27?

5 Katika karne zilizofuata, Yehova aliendelea kuwaalika rafiki zake ili wawe wageni wake. (Soma Ezekieli 37:26, 27.) Kwa mfano, katika unabii wa Ezekieli tunajifunza kwamba Mungu anatamani sana waabudu wake washikamanifu wawe na uhusiano wa karibu pamoja naye. Anaahidi kufanya “agano la amani pamoja nao.” Unabii huo unarejelea wakati ambao wale walio na tumaini la kwenda mbinguni na wale walio na tumaini la kuishi duniani wataunganishwa pamoja chini ya hema lake la mfano wakiwa “kundi moja.” (Yoh. 10:16) Wakati huo ni sasa!

MUNGU ANATUJALI MAHALI POPOTE TULIPO

6. Mtu anawezaje kuwa mgeni katika hema la Yehova, na hema Lake linapatikana wapi?

6 Katika nyakati za Biblia, hema la mtu lilikuwa mahali alipopumzika na kulindwa kutokana na hali mbaya ya hewa. Mgeni katika hema hilo angeweza kutarajia kutunzwa vizuri. Tunapojiweka wakfu kwa Yehova, tunakuwa wageni katika hema lake la mfano. (Zab. 61:4) Tunafurahia chakula kingi cha kiroho na urafiki pamoja na wengine ambao pia ni wageni wa Yehova. Hema la mfano la Yehova haliko mahali fulani hususa. Huenda umetembelea nchi ya kigeni, labda ili kuhudhuria kusanyiko la pekee, na ukakutana na wengine ambao wamepata baraka ya kuwa katika hema la Mungu. Hema hilo linapatikana mahali popote ambapo waabudu wake watiifu wanapatikana.—Ufu. 21:3.

7. Kwa nini tunaweza kusema kwamba waabudu waaminifu ambao wamekufa bado ni wageni katika hema la Yehova? (Tazama pia picha.)

7 Namna gani kuhusu waabudu waaminifu ambao wamekufa? Je, tunaweza kufikia mkataa kwamba bado wao ni wageni katika hema la Yehova? Ndiyo! Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Kwa sababu bado wako hai katika kumbukumbu ya Yehova. Yesu alisema hivi: “Hata Musa alifunua kwamba wafu watafufuliwa, katika masimulizi kuhusu kichaka cha miiba, anapomwita Yehova ‘Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.’ Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai, kwa maana kwake, wote wako hai.”—Luka 20:37, 38.

Hata waabudu waaminifu ambao wamekufa wanaweza kuonwa kuwa wageni katika hema la Mungu (Tazama fungu la 7)


MAJUKUMU NA MANUFAA YA KUWA WAGENI WA YEHOVA

8. Tunanufaikaje tunapokuwa wageni katika hema la Yehova?

8 Kama tu ambavyo hema halisi linaweza kuwa mahali pa kupumzika na kujilinda kutokana na hali mbaya ya hewa, hema la Yehova linawapa wageni wake ulinzi kutokana na madhara ya kiroho na tumaini halisi la wakati ujao. Tunapoendelea kuwa karibu na Yehova, Shetani hawezi kutusababishia madhara yoyote ya kudumu. (Zab. 31:23; 1 Yoh. 3:8) Katika ulimwengu mpya, Yehova ataendelea kuwalinda rafiki zake waaminifu kutokana na madhara ya kiroho, na pia kutokana na kifo.—Ufu. 21:4.

9. Yehova anatarajia wageni wake wajiendeshe kwa njia gani?

9 Kwa kweli, ni pendeleo kubwa sana kuwa mgeni katika hema la Yehova, yaani, kufurahia uhusiano wa kibinafsi pamoja naye ambao unaweza kudumu milele. Tunapaswa kujiendeshaje ikiwa tungependa kuendelea kuwa wageni wake? Ikiwa mtu angekualika nyumbani kwake, ungependa kufanya mambo ambayo yangemfurahisha. Kwa mfano, huenda akatarajia uvue viatu kabla ya kuingia ndani, nawe kwa hiari ungekuwa tayari kufanya hivyo. Bila shaka, sisi pia tungependa kujua matakwa ya Yehova kwa wale wanaotaka kuendelea kuwa wageni katika hema lake. Upendo wetu kwa Yehova unatuchochea kufanya yote tunayoweza “ili kumpendeza kikamili.” (Kol. 1:10) Na ingawa tunamwona Yehova kuwa Rafiki yetu, tunatambua kwamba yeye pia ni Mungu wetu na Baba yetu, na anastahili heshima kutoka kwetu. (Zab. 25:14) Tukiwa na hilo akilini, sikuzote tunapaswa kumwonyesha heshima kubwa, na kamwe tusisahau yeye ni nani. Staha ya aina hiyo itatusaidia kuepuka mwenendo ambao utamkasirisha. Bila shaka, tunatamani ‘kutembea kwa kiasi’ pamoja na Mungu wetu.—Mik. 6:8.

YEHOVA HAKUWAONYESHA UBAGUZI WALIPOKUWA NYIKANI

10-11. Njia ambayo Yehova alitumia kushughulika na Waisraeli walipokuwa kwenye nyika ya Sinai inaonyeshaje kwamba hana ubaguzi?

10 Yehova haonyeshi ubaguzi anaposhughulika na wageni wake. (Rom. 2:11) Tunaweza kujifunza zaidi kuhusu jinsi ambavyo Yehova haonyeshi ubaguzi kupitia njia aliyotumia kushughulika na Waisraeli walipokuwa kwenye nyika ya Sinai.

11 Baada ya kuwakomboa watu wake kutoka kwenye utumwa nchini Misri, Yehova aliwaweka rasmi makuhani ili watumikie kwenye hema la ibada. Walawi walipewa mgawo wa kushughulikia kazi nyingine zilizohusiana na hema la ibada. Je, wale waliotumikia kwenye hema la ibada au wale waliopiga kambi karibu nalo walitunzwa vizuri zaidi na Yehova kuliko wengine? Hapana! Yehova hana ubaguzi.

12. Njia ambayo Yehova alitumia kushughulika na taifa lake jipya ilionyeshaje kwamba hana ubaguzi? (Kutoka 40:38) (Tazama pia picha.)

12 Watu wote waliopiga kambi walikuwa na fursa ileile ya kufurahia urafiki pamoja na Yehova, haidhuru walikuwa na mgawo gani wa pekee au waliishi umbali gani kutoka kwenye hema la ibada. Kwa mfano, Yehova alihakikisha kwamba taifa lote lingeweza kuona nguzo ya kimuujiza ya wingu na nguzo ya moto zilizoonekana juu ya hema la ibada. (Soma Kutoka 40:38.) Wingu hilo lilipoanza kuelekea sehemu mpya, hata wale waliopiga kambi mbali zaidi na hema la ibada waliweza kuliona wingu hilo, kukusanya mali zao, kubomoa mahema ya familia yao, na kwenda sambamba na taifa lote. (Hes. 9:15-23) Wote wangeweza kusikia sauti kubwa ya tarumbeta mbili za fedha zikimjulisha kila mtu aanze kuhama. (Hes. 10:2) Ni wazi kwamba kuishi karibu sana na hema la ibada hakukuthibitisha kwamba mtu alikuwa na urafiki wa karibu zaidi na Yehova. Badala yake, kila mtu katika taifa hilo jipya la Yehova angeweza kuwa mgeni Wake na kuwa na uhakika kwamba angepata mwongozo na ulinzi Wake. Vivyo hivyo leo, haidhuru mahali tunapoishi duniani, tunaweza kunufaika kutokana na upendo, utunzaji, na ulinzi wa Yehova.

Mpango wa Mungu wa hema la ibada ulionyesha hana ubaguzi (Tazama fungu la 12)


MIFANO YA SIKU ZETU INAYOONYESHA KWAMBA YEHOVA HANA UBAGUZI

13. Leo, Yehova anaonyeshaje kwamba hana ubaguzi?

13 Leo, baadhi ya watu wa Mungu wanaishi karibu na makao makuu ya ulimwenguni pote au ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Na wengine hata wanatumikia katika sehemu hizo. Hivyo, wanaweza kushiriki katika utendaji unaofanywa katika sehemu hizo na kushirikiana moja kwa moja na wale wanaoongoza. Wengine wanatumikia wakiwa waangalizi wanaosafiri au katika aina nyingine ya utumishi wa pekee wa wakati wote. Hata ikiwa wewe si miongoni mwa ndugu na dada ambao kwa sasa wanatumikia katika aina hizo za utumishi, uwe na uhakika kwamba Yehova, Mwenyeji wetu, anawapenda wageni wake wote wenye kibali chake. Na anawajali wote kibinafsi. (1 Pet. 5:7) Watu wote wa Mungu wanapata chakula cha kiroho, mwongozo, na ulinzi wanaohitaji.

14. Toa mfano mwingine unaoonyesha kwamba Yehova hana ubaguzi akiwa Mwenyeji wetu.

14 Mfano mwingine unaoonyesha kwamba Yehova akiwa Mwenyeji wetu hana ubaguzi ni kwamba amefanya Biblia ipatikane kwa watu ulimwenguni pote. Awali, Maandiko Matakatifu yaliandikwa katika lugha tatu: Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki. Je, wale wanaoweza kusoma Biblia katika lugha hizo za awali wana uhusiano wa karibu zaidi na Yehova kuliko wale ambao hawawezi? Hapana.—Mt. 11:25.

15. Ni jambo gani linalothibitisha kwamba Yehova hana ubaguzi? (Tazama pia picha.)

15 Kupata kibali cha Yehova hakutegemei elimu yetu au uwezo wetu wa kuzungumza lugha mbalimbali. Yehova anafanya hekima yake ipatikane kwa watu wote duniani, iwe wana elimu ya juu sana au la. Biblia, Neno lake lililoongozwa na roho, limetafsiriwa katika maelfu ya lugha; hivyo, watu ulimwenguni pote wanaweza kunufaika kutokana na mafundisho yake na kujifunza jinsi wanavyoweza kuwa rafiki zake.—2 Tim. 3:16, 17.

Upatikanaji wa Biblia leo unathibitishaje kwamba Mungu hana ubaguzi? (Tazama fungu la 15)


ENDELEA ‘KUKUBALIWA’ NA YEHOVA

16. Kulingana na Matendo 10:34, 35, tunawezaje kuendelea kukubaliwa na Yehova?

16 Ni pendeleo kubwa kualikwa na Yehova kuwa wageni katika hema lake la mfano. Yeye ni Mwenyeji wetu mwenye fadhili zaidi, mwenye upendo zaidi, na mkaribishaji wageni bora zaidi. Zaidi ya hayo, Yehova hana ubaguzi, anatukaribisha sisi sote haidhuru mahali tunapoishi, malezi yetu, elimu, jamii, kabila, umri, au jinsia yetu. Hata hivyo, wale tu wanaotimiza viwango vyake wanakubaliwa kuwa wageni wake.—Soma Matendo 10:34, 35.

17. Tunaweza kupata wapi habari zaidi kuhusu kuwa wageni katika hema la Yehova?

17 Kama ilivyoandikwa kwenye Zaburi 15:1, Daudi aliuliza maswali haya: “Ee Yehova, ni nani anayeweza kuwa mgeni katika hema lako? Ni nani anayeweza kukaa katika mlima wako mtakatifu?” Mtunga zaburi huyo aliongozwa na roho ya Mungu kujibu maswali hayo. Katika makala inayofuata tutazungumzia habari zaidi kuhusu baadhi ya matakwa hususa ambayo lazima tutimize ili tuendelee kukubaliwa na Yehova.

WIMBO 32 Simama Upande wa Yehova!