MAKALA YA 24

WIMBO 24 Njooni Kwenye Mlima wa Yehova

Endelea Kuwa Mgeni wa Yehova Milele!

Endelea Kuwa Mgeni wa Yehova Milele!

“Ee Yehova, ni nani anayeweza kuwa mgeni katika hema lako?”ZAB. 15:1.

JAMBO KUU

Kuchunguza matakwa tunayopaswa kutimiza ili kuendelea kufurahia urafiki pamoja na Yehova na kujikumbusha jinsi ambavyo Yehova anataka tuwatendee rafiki zake.

1. Tunaweza kunufaikaje kwa kuchunguza Zaburi 15:​1-5?

 KATIKA makala iliyotangulia, tulijifunza kwamba watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu wanaweza kuwa wageni katika hema lake la mfano kwa kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja naye. Lakini tunahitaji kufanya nini ili tustahili kuwa na uhusiano huo pamoja na Yehova? Zaburi ya 15 inaeleza mengi kuhusu jambo hilo. (Soma Zaburi 15:​1-5.) Zaburi hiyo inatueleza mambo hususa ambayo yanaweza kutusaidia kumkaribia Mungu zaidi.

2. Ni jambo gani ambalo huenda lilimchochea mtunga zaburi Daudi kutaja hema la Yehova?

2 Zaburi ya 15 inaanza kwa maswali haya: “Ee Yehova, ni nani anayeweza kuwa mgeni katika hema lako? Ni nani anayeweza kukaa katika mlima wako mtakatifu?” (Zab. 15:1) Alipotaja “hema” la Yehova, huenda mtunga zaburi Daudi alikuwa akifikiria hema la ibada, ambalo kwa muda fulani lilikuwa Gibeoni. Pia, Daudi anataja kuhusu ‘mlima mtakatifu’ wa Mungu, na huenda anarejelea Mlima Sayuni uliopo Yerusalemu. Akiwa huko, kilomita kadhaa kusini mwa Gibeoni, Daudi alitengeneza hema ambalo lingehifadhi sanduku la agano hadi wakati ambapo mahali pengine pa kudumu pangejengwa kwa ajili ya sanduku hilo.—2 Sam. 6:17.

3. Kwa nini tunapaswa kupendezwa na Zaburi ya 15? (Tazama pia picha.)

3 Bila shaka, Waisraeli wengi hawakuruhusiwa kutumikia kwenye hema la ibada, sembuse kuingia ndani ya hema ambapo sanduku la agano liliwekwa. Lakini watumishi wote waaminifu wa Yehova wangeweza kuwa wageni katika hema lake la mfano kwa kuwa rafiki zake na kudumisha urafiki huo. Hilo ni jambo ambalo sisi sote tunatamani. Zaburi ya 15 inataja baadhi ya sifa ambazo tunahitaji kusitawisha na kuonyesha ili tuendelee kuwa rafiki za Yehova.

Waisraeli katika siku za Daudi wangeweza kuwazia wakiwa wageni katika hema la Yehova (Tazama fungu la 3)


TEMBEA BILA KOSA NA UTENDE YALIYO SAWA

4. Tunajuaje kwamba Yehova anatarajia tufanye mengi zaidi ya kubatizwa? (Isaya 48:1)

4 Kwenye Zaburi 15:​2, rafiki ya Mungu anafafanuliwa kuwa mtu “anayetembea bila kosa, anayezoea kutenda yaliyo sawa.” Maneno “anayetembea” na “anayezoea kutenda” yanaonyesha kwamba tendo fulani linahitajika ambalo linafanywa kwa ukawaida na kwa kuendelea. Lakini je, kweli tunaweza ‘kutembea bila kosa’? Ndiyo. Ingawa hakuna mwanadamu aliye mkamilifu, Yehova atatuona kuwa watu ‘wanaotembea bila kosa’ ikiwa tutafanya yote tunayoweza ili kumtii yeye. Tunapojiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa, ndipo tunapoanza safari yetu pamoja na Mungu. Kwa mfano, katika nyakati za Biblia, kuwa tu katika taifa la Israeli hakukumaanisha moja kwa moja kwamba mtu angestahili kuwa mgeni wa Yehova. Baadhi ya watu walimwitia Mungu lakini si “katika kweli na uadilifu.” (Soma Isaya 48:1.) Waisraeli wanyoofu walihitaji kujifunza kuhusu matakwa ya Yehova na kuyafuata. Vivyo hivyo, ili tufurahie kibali cha Mungu leo, tunahitaji kufanya mengi zaidi ya kubatizwa na kushirikiana na kutaniko la Kikristo. Ni lazima tuendelee ‘kuzoea kutenda yaliyo sawa.’ Hilo linahusisha nini?

5. Kumtii Yehova katika mambo yote kunahusisha nini?

5 Machoni pa Yehova, ‘kutembea bila kosa’ na ‘kuzoea kutenda yaliyo sawa’ kunamaanisha mengi zaidi ya kushiriki kwa ukawaida katika baadhi ya mambo yanayofanywa kwenye sehemu za ibada. (1 Sam. 15:22) Ni lazima tujitahidi kumtii Mungu katika kila sehemu ya maisha yetu, hata tunapokuwa peke yetu. (Met. 3:6; Mhu. 12:​13, 14) Ni muhimu tujitahidi kumtii Yehova hata katika mambo yanayoonekana kuwa madogo. Tunapofanya hivyo tunaonyesha kwamba tunampenda kikweli, na hilo linamfanya atupende hata zaidi.—Yoh. 14:23; 1 Yoh. 5:3.

6. Kulingana na Waebrania 6:​10-12, ni jambo gani lililo muhimu zaidi kuliko matendo yoyote ya uaminifu tuliyofanya wakati uliopita?

6 Yehova anathamini sana mambo tuliyomfanyia wakati uliopita. Hata hivyo, matendo yetu ya uaminifu ya wakati uliopita hayatoshi kufanya tustahili kuendelea kuwa wageni katika hema la Yehova. Hilo linaonyeshwa wazi kwenye Waebrania 6:​10-12. (Soma.) Yehova hasahau matendo yetu mazuri ya wakati uliopita. Lakini anataka tuendelee kumwabudu kwa nafsi yote “mpaka mwisho.” Atatuthawabisha kwa kuwa rafiki yetu milele “ikiwa hatutachoka kabisa.”—Gal. 6:9.

SEMA UKWELI MOYONI MWAKO

7. Kusema ukweli moyoni mwetu kunahusisha nini?

7 Mtu anayetaka kuwa mgeni anayekubalika katika hema la Yehova ni lazima ‘aseme ukweli moyoni mwake.’ (Zab. 15:2) Hilo linahusisha mengi zaidi ya kuepuka kudanganya. Yehova anataka tuwe wanyoofu katika kila jambo tunalofanya na kusema. (Ebr. 13:18) Jambo hilo ni muhimu, “kwa maana Yehova humchukia mtu mwenye hila, lakini ana urafiki wa karibu na watu wanyoofu.”—Met. 3:32.

8. Tunapaswa kuepuka mwenendo gani?

8 Wale ‘wanaosema ukweli moyoni mwao’ hawajifanyi kuwa watiifu wakiwa hadharani huku wakivunja sheria za Mungu sirini. (Isa. 29:13) Wanaepuka kutenda kwa hila. Mtu mwenye hila huenda akaanza kutilia shaka hekima iliyo katika baadhi ya sheria za Yehova. (Yak. 1:​5-8) Huenda akakosa kumtii Yehova inapohusu mambo ambayo yanaonekana kwake kuwa si muhimu sana. Kisha ikiwa inaonekana hakuna jambo lolote baya linalotokea anapokosa kutii, huenda akapata ujasiri wa kuvunja sheria nyingine za Mungu, na ibada yake itakuwa ya kinafiki. (Mhu. 8:11) Lakini sisi tungependa kuwa wanyoofu katika mambo yote.

9. Tunaweza kujifunza nini kwa kuchunguza pindi Yesu na Nathanaeli walipokutana kwa mara ya kwanza? (Tazama pia picha.)

9 Tunaweza kujifunza kuhusu umuhimu wa kuwa na moyo mnyoofu kwa kuchunguza pindi Yesu na Nathanaeli walipokutana kwa mara ya kwanza. Filipo alipomleta Nathanaeli, rafiki yake, akutane na Yesu, jambo la pekee lilitukia. Ingawa Yesu hakuwa amewahi kukutana na Nathanaeli, alisema hivi: “Ona, Mwisraeli kwa hakika ambaye hamna udanganyifu ndani yake.” (Yoh. 1:47) Bila shaka, Yesu aliwaona mitume wake wengine kuwa wanyoofu, lakini kwa Nathanaeli aliona unyoofu wa pekee. Kama tu sisi, Nathanaeli alikuwa mtu ambaye si mkamilifu. Lakini hakuwa na unafiki wowote, badala yake alikuwa mnyoofu katika mambo yote. Yesu alivutiwa na jambo hilo na akampongeza Nathanaeli. Kwa kweli, litakuwa pendeleo kubwa ikiwa Yesu atasema hivyo pia kutuhusu!

Filipo alimpeleka Nathanaeli, rafiki yake, kwa Yesu. Nathanaeli alikuwa mwanamume ambaye hakuwa na udanganyifu ndani yake. Je, hilo linaweza kusemwa pia kutuhusu sisi? (Tazama fungu la 9)


10. Kwa nini tunapaswa kuepuka kutumia vibaya zawadi ya usemi? (Yakobo 1:26)

10 Matakwa mengi yaliyoorodheshwa kwenye Zaburi ya 15 yanahusu jinsi tunavyowatendea wengine. Zaburi 15:3 inasema kwamba mgeni katika hema la Yehova “hachongei kwa ulimi wake, hamtendei jirani yake jambo lolote ovu, naye hawaharibii sifa rafiki zake.” Kutumia usemi wetu vibaya katika njia hizo kunaweza kuwadhuru sana wengine na kufanya tusistahili kuwa wageni katika hema la Yehova.—Soma Yakobo 1:26.

11. Uchongezi ni nini, na wachongezi wasiotubu wanafanywa nini?

11 Mtunga zaburi anataja kihususa kuhusu uchongezi. Uchongezi ni nini? Kwa ujumla, ni habari za uwongo zinazoweza kuharibu sifa ya mtu. Wachongezi wasiotubu wanaondolewa katika kutaniko la Kikristo.—Yer. 17:10.

12-13. Ni katika hali zipi tunaweza bila kukusudia, kuwa na hatia ya kuwaharibia sifa rafiki zetu? (Tazama pia picha.)

12 Pia, Zaburi 15:3 inatukumbusha kwamba wageni wa Yehova hawawatendei jambo lolote ovu jirani zao na hawawaharibii sifa rafiki zao. Huenda tukawaharibiaje sifa rafiki zetu?

13 Tunaweza kumharibia mtu sifa bila kukusudia kwa kueneza habari mbaya kumhusu. Fikiria kuhusu hali zifuatazo: (1) dada anaacha kutumikia akiwa painia, (2) wenzi wa ndoa hawatumikii tena Betheli, au (3) ndugu hatumikii tena akiwa mzee au mtumishi wa huduma. Je, inafaa kukisia-kisia sababu za mabadiliko hayo na kuwaeleza wengine maoni yako? Huenda kuna sababu za mabadiliko hayo ambazo sisi hatujui. Zaidi ya hilo, mgeni kwenye hema la Yehova “hamtendei jirani yake jambo lolote ovu, naye hawaharibii sifa rafiki zake.”

Ni rahisi kueneza habari mbaya kuhusu watu wengine, na habari hizo huenda zikafikia hatua ya kuwa uchongezi (Tazama fungu la 12-13)


WAHESHIMU WALE WANAOMWOGOPA YEHOVA

14. Fafanua jinsi wageni wa Yehova wanavyomkataa “mtu yeyote anayedharauliwa.”

14 Zaburi 15:4 inasema kwamba rafiki wa Yehova “humkataa mtu yeyote anayedharauliwa.” Tunawezaje kufanya hivyo? Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, hatustahili kuamua ikiwa mtu fulani ni mwenye kudharauliwa. Kwa nini? Kwa sababu kiasili huenda tukapendezwa na mtu fulani kwa msingi wa sifa zake na sifa za wengine zikatuudhi. Hivyo, tunapaswa kuwakataa wale tu ambao Yehova anawaona kuwa wenye ‘kudharauliwa.’ (1 Kor. 5:11) Watu hao wanatia ndani wale ambao wana mazoea ya kufanya mambo mabaya bila kutubu, hawaheshimu mambo tunayoamini, au wanajaribu kudhoofisha hali yetu ya kiroho.—Met. 13:20.

15. Taja njia moja ya kuwaonyesha heshima “wale wanaomwogopa Yehova.”

15 Kwa upande mwingine, Zaburi 15:4 inasema tuwaheshimu “wale wanaomwogopa Yehova.” Hivyo, tunatafuta njia za kuwaonyesha fadhili na heshima rafiki za Yehova. (Rom. 12:10) Jinsi gani? Zaburi 15:4 inaonyesha kwamba mgeni katika hema la Yehova “havunji ahadi yake, hata ikimletea hasara.” Bila shaka kuvunja ahadi zetu kunaweza kuwaumiza wengine. (Mt. 5:37) Kwa mfano, Yehova anatarajia wageni wake waishi kulingana na nadhiri yao ya ndoa. Pia, anafurahi wazazi wanapojitahidi kutimiza ahadi walizotoa kwa watoto wao. Upendo wetu kwa Mungu na jirani utatuchochea kufanya yote tunayoweza ili kutimiza ahadi zetu.

16. Ni kwa njia gani nyingine tunaweza kuwaheshimu rafiki za Yehova?

16 Njia nyingine ya kuwaheshimu rafiki za Mungu ni kwa kuwa mkaribishaji wageni na kuwa mkarimu. (Rom. 12:13) Pindi za tafrija pamoja na ndugu na dada zetu zinatusaidia kuimarisha urafiki wetu pamoja nao na pamoja na Yehova. Isitoshe, tunapokuwa wakaribishaji wageni, tunamwiga Yehova.

NJIA YAKO YA MAISHA IWE BILA UPENDO WA PESA

17. Kwa nini suala la pesa linatajwa kwenye Zaburi ya 15?

17 Biblia inasema kwamba mgeni wa Yehova “hakopeshi pesa zake kwa faida, naye hakubali rushwa ili kumkandamiza asiye na hatia.” (Zab. 15:5) Kwa nini masuala ya pesa yanatajwa kwenye zaburi hii fupi? Kwa sababu kutokuwa na usawaziko inapohusu masuala ya pesa kunaweza kuwaumiza wengine na kuharibu urafiki wetu pamoja na Mungu. (1 Tim. 6:10) Katika nyakati za Biblia, baadhi ya watu waliwatumia vibaya ndugu zao waliokuwa maskini kwa kuwatoza riba walipokopa pesa. Pia, baadhi ya waamuzi walipokea rushwa, kisha waliwahukumu isivyo haki wale wasio na hatia. Mazoea kama hayo yanamchukiza Yehova.—Eze. 22:12.

18. Ni maswali gani yanayoweza kutusaidia kuchunguza mtazamo wetu kuelekea pesa? (Waebrania 13:5)

18 Ni vema tuchunguze mtazamo wetu kuelekea pesa. Jiulize hivi: ‘Je, mara kwa mara ninafikiria kuhusu pesa na vitu ninavyoweza kununua? Ninapokopa pesa, je, ninachukua muda mrefu kuzirudisha, nikijiambia kwamba aliyenikopesha hazihitaji? Je, kuwa na pesa kunanifanya nijione kuwa mtu muhimu, lakini ni vigumu kwangu kuwa mkarimu? Je, ninawahukumu ndugu na dada wenye pesa kuwa watu wanaopenda mali? Je, ninasitawisha urafiki pamoja na matajiri, lakini ninawapuuza walio maskini?’ Tumepata pendeleo kubwa kuwa wageni wa Yehova. Tunaweza kulinda pendeleo hilo ikiwa tutahakikisha kwamba njia yetu ya maisha itakuwa bila upendo wa pesa. Tukifanya hivyo, Yehova hatatuacha kamwe!—Soma Waebrania 13:5.

YEHOVA ANAWAPENDA RAFIKI ZAKE

19. Kwa nini Yehova anataka tutii matakwa yaliyo kwenye Zaburi ya 15?

19 Zaburi ya 15 inamalizia kwa ahadi hii: “Yeyote anayefanya mambo hayo hatatikiswa kamwe.” (Zab. 15:5) Katika mstari huo, mtunga zaburi anafunua kwamba Yehova anataka tutii mambo yote yanayotajwa kwenye zaburi hiyo. Yehova anataka tuwe na furaha. Hivyo, anatupatia mwongozo utakaotuletea baraka na ulinzi wake.—Isa. 48:17.

20. Wageni wa Yehova wanaweza kutazamia nini kwa hamu?

20 Wageni wa Yehova waliokubaliwa naye wanaweza kutazamia wakati ujao mzuri. Watiwa-mafuta waaminifu watakaribishwa kwenye “makao mengi” ambayo Yesu amewatayarishia huko mbinguni. (Yoh. 14:2) Wale walio na tumaini la kuishi duniani wanatazamia kwa hamu kuona utimizo wa ahadi iliyo katika Ufunuo 21:3. Bila shaka, sisi sote tunahisi ni pendeleo kubwa sana kupata mwaliko wa kuwa rafiki za Yehova, na kuwa wageni katika hema lake milele!

WIMBO 39 Jifanyie Jina Zuri Mbele za Mungu