Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIERRA LEONE NA GUINEA

Walimwita “Bible” Brown

William R. Brown

Walimwita “Bible” Brown
  • ALIZALIWA 1879

  • ALIBATIZWA 1908

  • MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Aliongoza kazi ya kuhubiri katika eneo la Afrika Magharibi.

MNAMO 1907, William alikuwa miongoni mwa wafanyakazi waliokuwa wakijenga Mfereji wa Panama. Siku moja alipokuwa akipita kwenye mtaa fulani, alisikia hotuba iliyokuwa ikitolewa na Isaiah Richards, Mwanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo. Mahubiri ya Richards yalitegemea “Chati ya Enzi,” mchoro uliotumiwa kufafanua makusudi ya Mungu. William alikubali kweli mara moja na kurudi nchini Jamaika ili akawaambie habari hizo mama na dada yake. Baada ya muda, wao pia wakawa Wanafunzi wa Biblia.

Ndugu Brown alitumikia kwa kipindi fulani katika jiji la Panama City, nchini Panama. Akiwa huko alikutana na Evan­der J. Coward, mwakilishi anayesafiri wa Wanafunzi wa Biblia ambaye alikuwa akitembelea nchini Panama na kutoa hotuba. Coward alikuwa msemaji mzuri, na watu walimiminika ili kumsikiliza. Ndugu Coward alipoona kwamba William alikuwa na bidii kwa ajili ya kweli, alimwalika aandamane naye kwenye ziara yake ya kuhubiri nchini Trinidad.

 Kwa kipindi cha miaka kumi au zaidi, William alitembelea maeneo mbalimbali katika visiwa vya West Indies, akipainia na kuviimarisha vikundi vidogo. Mnamo 1920, alimwoa Antonia, dada Mkristo mwaminifu. Siku mbili baada ya ndoa yao, William na Antonia walipanda meli hadi kwenye kisiwa kidogo cha Montserrat mojawapo ya Visiwa vya Pasifiki ya Kusini, wakiwa na sinema ya “Photo-Drama of Creation”—yenye sehemu nne na slaidi ya picha inayotegemea Biblia. Pia, walihubiri kwenye visiwa vya Barbados, Dominika, na Grenada. Walifurahia sana fungate lao kwa kushiriki katika utumishi wa Yehova.

Miaka miwili baadaye, William alimwandikia Joseph F. Rutherford, ambaye wakati huo alikuwa akisimamia kazi ya watu wa Yehova, akisema: “Kwa msaada wa Yehova nimetoa ushahidi katika visiwa vingi vya Karibea na kupata wanafunzi. Je, nirudi tena kwenye visiwa hivyo?” Siku kadhaa baadaye, Ndugu Rutherford alimjibu: “Nenda Sierra Leone, Afrika Magharibi, pamoja na mke na binti yako.”

Katika miaka 27 ambayo Ndugu Brown alitumikia Afrika Magharibi pamoja na familia yake, hakupenda kufanya kazi za ofisini. Alipenda sana kuhubiri. Kwa sababu alikazia sana umuhimu wa Biblia, watu walianza kumwita “Bible” Brown.

Mwaka 1950, akiwa na umri wa miaka 71, William Brown pamoja na mke wake walirudi nchini Jamaika kufanya upainia. William aliendelea kupainia hadi alipomaliza mwendo wake duniani mwaka 1967. Alipenda sana upainia! Alihisi kwamba ni moja kati ya mapendeleo makubwa sana ambayo mwanadamu anaweza kupewa.