Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIERRA LEONE NA GUINEA

Yehova Amenisaidia

Jay Campbell

Yehova Amenisaidia
  • ALIZALIWA 1966

  • ALIBATIZWA 1986

  • MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Mgonjwa wa polio ambaye alikuja kuwa painia wa kawaida.

TANGU utotoni nimekuwa kiwete kuanzia kiunoni kushuka chini, niliishi pamoja na mama yangu na baadhi ya familia nyingine maskini jijini Freetown kwenye nyumba kadhaa zilizokuwa ndani ya ua. Kwa kuwa nilikuwa na aibu na niliogopa vile ambavyo wageni wangeniona, nilitoka nje ya ua huo mara moja tu katika kipindi chote cha miaka 18.

Nilipokuwa na miaka 18, Pauline Landis, mmishonari ambaye ni Shahidi wa Yehova, alitutembelea nyumbani kwetu na kuniomba anifundishe Biblia. Nilipomwambia kwamba sijui kusoma wala kuandika, Pauline akaniambia kwamba angenifundisha pia kusoma na kuandika. Kwa hiyo nikakubali.

Mambo niliyojifunza kutoka kwenye Biblia yalinifanya niwe na shangwe sana. Siku moja, nilimuuliza Pauline ikiwa ningeweza kuhudhuria mkutano wa kutaniko uliofanywa kwenye nyumba ambayo haikuwa mbali na mahali nilipoishi. “Nitatembea hadi kwenye nyumba hiyo kwa kutumia vibao vyangu,” nikamwambia.

Pauline alipokuja kunichukua, mama na jirani zangu waliniangalia kwa wasiwasi. Kwa kuwa miguu yangu ilikuwa imepooza, nilitumia vipande viwili vya mbao ili kujikokota. Nilipokuwa nikikaribia kutoka nje kabisa ya ua, majirani wakaanza kumpigia kelele Pauline: “Wewe unamlazimisha tu huyu binti atembee. Aliwahi kujaribu kutembea wakati uliopita lakini alishindwa.”

“Jay, ungependa kwenda?” Pauline akaniuliza kwa upole.

“Ndiyo!” Nikamjibu. “Huo ndio uamuzi wangu.”

Majirani waliendelea kuniangalia huku wakiwa kimya kadiri nilivyozidi kulikaribia lango. Nilipotoka nje kabisa ya ua, wakalipuka kwa furaha.

Nilifurahia sana mkutano huo! Baadaye, niliazimia kufika kwenye Jumba la Ufalme. Ili kufika huko nilihitaji kujikokota hadi mwisho wa mtaa wetu, kisha nikodi teksi, na hatimaye nipate ndugu wa kunibeba kwenye kilima chenye mwinuko mkali. Mara nyingi nilifika nikiwa nimelowa na kuchafuka kwa matope, kwa hiyo ningehitaji kubadili nguo zangu baada ya kufika Jumba la Ufalme. Baadaye, dada fulani nchini Switzerland alinitumia kiti cha magurudumu, ambacho kilinisaidia nisafiri bila kuchafuka.

Kusoma masimulizi ya Mashahidi wengine walemavu kulinichochea nimtumikie Yehova kwa ukamili hata zaidi. Mwaka 1988, nikaanza upainia wa kawaida. Nilimwomba Yehova anisaidie nifikie lengo langu, yaani, kumsaidia mtu fulani katika familia yangu na katika eneo letu awe mtumishi wa Yehova. Sala zangu zilijibiwa nilipowasaidia wana wawili wa dada yangu na mwanamke mmoja ambaye nilikutana naye katika mahubiri ya barabarani wajifunze kweli.

Sasa mikono yangu haina nguvu tena, kwa hiyo ninategemea watu wengine wanisukume katika kiti changu. Pia, ninasumbuliwa na maumivu yasiyokoma. Hata hivyo, niligundua kwamba dawa moja ya maumivu hayo ni kuwafundisha watu kuhusu Yehova. Shangwe ninayopata kwa sababu ya kuwafundisha watu hutuliza maumivu yangu na kunifariji kwa kuwa Yehova amenisaidia, na sasa maisha yangu yana kusudi.