Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIERRA LEONE NA GUINEA

Aliyekuwa Mwanajeshi Mtoto Awa Painia wa Kawaida

Aliyekuwa Mwanajeshi Mtoto Awa Painia wa Kawaida

NILIKUWA na umri wa miaka 16 nilipolazimishwa na wanajeshi waasi nijiunge na jeshi lao. Walinipa dawa za kulevya na pombe, na mara kwa mara nilipigana kwa sababu ya kuleweshwa na dawa za kulevya. Nilipigana vita vingi na kutenda ukatili mbaya sana. Ninajuta sana kuhusiana na jambo hilo.

Siku moja, Shahidi fulani mwenye umri mkubwa alikuja kuhubiri katika kambi zetu. Watu wengi waliwaogopa na kuwadharau waasi, lakini shahidi huyo alitaka kutusaidia kiroho. Aliponikaribisha kwenye mkutano, nilikubali. Sikumbuki kilichosemwa katika mkutano ule, lakini nakumbuka vizuri sana jinsi nilivyokaribishwa kwa uchangamfu.

Vita vilipopamba moto, tulipotezana na Mashahidi. Halafu nilijeruhiwa vibaya na kupelekwa katika eneo lililodhibitiwa na waasi ili nipate nafuu. Kabla ya vita kuisha, nilifanikiwa kutoroka na kukimbilia katika eneo lililodhibitiwa na serikali na nikaingizwa kwenye mpango wa kuwapokonya waasi silaha, kutolewa jeshini, na kurejeshwa uraiani.

Nilihitaji sana msaada wa kiroho. Hivyo, nilihudhuria mikutano ya kanisa la Pentekoste, lakini waumini wa kanisa hilo waliniita Shetani aliye katikati yao. Kwa hiyo, nilianza kuwatafuta Mashahidi wa Yehova. Baada ya kuwapata, nilianza kujifunza na kuhudhuria mikutano. Nilipoungama matendo yangu maovu, akina ndugu walinisomea maneno ya Yesu yenye kufariji: “Watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua ndio wanaomhitaji. . . . Nilikuja kuwaita, si watu waadilifu, bali watenda-dhambi.”Mt. 9:12, 13.

Maneno hayo yalinigusa sana moyo! Nilimkabidhi sime yangu ndugu aliyekuwa akinifundisha Biblia, na kumwambia: “Niliibeba silaha hii ili kujilinda dhidi ya walipiza kisasi. Lakini sasa, kwa kuwa najua Yehova na Yesu wananipenda, siitaki tena.”

Akina ndugu walinifundisha kusoma na kuandika. Hatimaye, nilibatizwa na kuwa painia wa kawaida. Leo, ninapowahubiria wale waliokuwa waasi zamani, wao husema kwamba wananiheshimu kwa sababu nimebadili maisha yangu. Hata nilijifunza na aliyekuwa msaidizi wa kamanda wa kikosi chetu cha zamani.

Nilipokuwa mwanajeshi, nilipata wavulana watatu. Baada ya kujifunza kweli, nilitaka kuwasaidia kiroho. Nilifurahi sana wawili kati yao walipokubali! Mmoja ni mhubiri ambaye hajabatizwa, na mwanangu wa kwanza sasa ni painia msaidizi.