Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIERRA LEONE NA GUINEA

Tuliwakimbia Wanajeshi Waasi

Andrew Baun

Tuliwakimbia Wanajeshi Waasi
  • ALIZALIWA 1961

  • ALIBATIZWA 1988

  • MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa painia wa kawaida mjini Pendembu, Mkoa wa Mashariki, nchini Sierra Leone, vita vilipozuka mwaka 1991.

ALASIRI moja waasi waliingia katika mji wetu, na kupiga risasi zao hewani kwa muda wa karibu saa mbili. Baadhi yao walikuwa vijana wadogo ambao walihangaishwa na uzito wa silaha zao. Walikuwa wachafu sana, nywele zao zilikuwa zimetimka, na walionekana kuwa wametumia dawa za kulevya.

Siku iliyofuata mauaji yalianza. Watu walilemazwa vibaya au kuuawa kikatili. Wanawake walibakwa. Kulikuwa na vurugu kubwa. Ndugu Amara Babawo na familia yake na watu wengine wanne waliokuwa wanapendezwa walikimbilia kwenye nyumba yangu. Tuliogopa sana.

Muda mfupi baadaye, kamanda wa waasi akatokea na kutuamuru turipoti kwa ajili ya mazoezi ya kijeshi asubuhi ya siku iliyofuata. Tuliazimia kutounga mkono upande wowote, ingawa kufanya hivyo kulimaanisha kifo. Tulisali sana usiku huo. Tuliamka mapema, na kusoma andiko la siku huku tukiwasubiri wanajeshi waasi waje. Hawakurudi.

“Mnasoma andiko la siku. Ni lazima iwe ninyi ni Mashahidi wa Yehova”

Baadaye ofisa wa waasi na wanaume wengine wanne waliiteka nyumba yangu kwa ajili ya shughuli za kijeshi. Walituambia tuendelee kukaa, hivyo tuliendelea kufanya mikutano na kuzungumzia andiko la siku hapo nyumbani. Baadhi ya wanajeshi hao walisema: “Mnasoma andiko la siku. Ni lazima iwe ninyi ni Mashahidi wa Yehova.” Hawakupendezwa na mambo ya Biblia, lakini walituheshimu.

Siku moja kamanda wa cheo cha juu alikuja ili kukagua vikosi vilivyokuwa vimepiga kambi kwenye nyumba yangu. Alimpigia saluti Ndugu Babawo na kumsalimia kwa mkono. Akiwahutubia wanajeshi, kamanda huyo alisema hivi kwa kufoka: “Mtu huyu ni mkubwa wangu na wenu pia. Ikiwa atapatwa na jambo lolote baya au watu walio pamoja naye, mtakiona cha mtema kuni. Tumeelewana?” Wakajibu “Ndiyo bwana mkubwa!” Kisha, kamanda huyo akatupatia barua ambayo iliwaagiza wanajeshi wa Revolutionary United Front wasitudhuru kwa sababu sisi ni raia wenye amani.

Miezi kadhaa baadaye, vikundi vya waasi vilianza kupigana vyenyewe kwa vyenyewe, hivyo tukakimbilia nchini Liberia. Tukiwa huko tulitishwa na kikundi kingine cha waasi. Tuliwaambia kwamba “sisi ni Mashahidi wa Yehova.” Kisha askari mmoja akatuuliza, “kwa hiyo, andiko la Yohana 3:16 linasemaje?” Tulipomweleza maneno ya andiko hilo, akaturuhusu tuondoke.

Baadaye, tulikutana na kamanda wa kikundi kingine cha waasi ambaye aliniamuru mimi na Ndugu Babawo tuandamane naye. Tuliogopa sana. Kisha mwanajeshi huyo akatuambia kwamba alikuwa amejifunza Biblia na Mashahidi kabla ya vita. Alitupatia fedha na kisha tukampa barua yetu ili aipeleke kwa akina ndugu katika kutaniko lililokuwa jirani. Muda mfupi baada ya jambo hilo, akina ndugu wawili walifika wakiwa na misaada na kutupeleka kwenye eneo lililokuwa salama.