Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIERRA LEONE NA GUINEA

Mwaka 2002-2013 Ongezeko la Karibuni (Sehemu ya 1)

Mwaka 2002-2013 Ongezeko la Karibuni (Sehemu ya 1)

 “Asante Sana Yehova!”

Kadiri hali zilivyozidi kutulia, ndugu na dada walivirudia vitu vilivyosalia katika nyumba zao. Makutaniko yaliyosambaratika wakati wa vita yalianzishwa tena, hasa katika eneo la mashariki lililoathiriwa sana na vita vya Sierra Leone. Mapainia fulani wa pekee kutoka eneo moja waliripoti hivi: “Watu 16 walihudhuria mkutano wetu wa kwanza, 36 wakaja katika mkutano uliofuata, 56 wakahudhuria mkutano wa tatu, na kisha watu 77 walihudhuria Ukumbusho! Tulifurahi sana!” Makutaniko mapya 9 yalianzishwa, na kufanya jumla ya makutaniko yote kuwa 24. Wamishonari kumi kutoka Gileadi waliwasili, na hivyo kuongeza nguvu mpya katika kazi ya kuhubiri. Mwaka 2004, hudhurio la Ukumbusho lilikuwa 7,594, idadi hiyo ilikuwa mara tano zaidi ya wahubiri wote! Pia, nchini Guinea kulikuwa na ongezeko kama hilo.

Baraza Linaloongoza lilitoa bila kukawia pesa za dharura ili kuwasaidia wakimbizi waliokuwa wakirejea wajiimarishe. (Yak. 2:15, 16) Timu za wajitoleaji wa kutoa msaada zilijenga au kukarabati Majumba ya Ufalme 12 na kurekebisha Jumba la Makusanyiko katika mji wa Koindu. Pia, walijenga nyumba 42 za matofali kwa ajili ya familia ambazo nyumba zao zilikuwa zimeharibiwa. Akiwa amesimama kando ya nyumba yake mpya iliyoezekwa kwa mabati huku akitiririkwa na machozi, mjane mmoja mwenye umri wa zaidi ya miaka 70 alisema hivi kwa sauti kubwa: “Asante sana Yehova! Asante sana Yehova! Asanteni sana akina ndugu!”

Pia, ofisi ya tawi ilianza kujenga Majumba ya Ufalme kwa kutumia pesa kutoka katika programu ya kusaidia nchi zisizo na uwezo mkubwa wa kifedha. Saidu Juanah, mzee na painia katika Kutaniko la Bo Magharibi, anaeleza: “Dada mmoja aliniambia hivi: ‘Nikisikia kwamba tutajengewa Jumba la Ufalme, nitapiga makofi kwa mikono na miguu!’ Nilipotangaza kwamba tungejengewa jumba jipya, dada huyo aliruka huku akipiga makofi na kucheza, yaani, alikuwa ‘akipiga’ makofi kwa mikono na miguu yake!”

Mnamo 2010, Kutaniko la Waterloo liliweka wakfu Jumba la Ufalme linaloweza kupanuliwa na kuwa Jumba la Makusanyiko lenye uwezo wa kuchukua watu 800. Siku ambayo kutaniko lilinunua mahali hapo, mnunuzi mwingine alimwahidi mmiliki wa eneo hilo pesa nyingi zaidi ili amuuzie mahali hapo. Hata hivyo mmiliki huyo akamweleza hivi: “Afadhali kuwe na kituo cha mikutano ya kidini kwenye kiwanja changu badala ya kukiuza ili kitumike kwa makusudi ya kibiashara.”

Majumba ya Ufalme 17 nchini Sierra Leone, na 6 nchini Guinea yamejengwa chini ya mpango wa kusaidia nchi ambazo hazina uwezo mkubwa wa kifedha. Majumba hayo madogo na yenye kuheshimika ambayo hutumiwa kwa ajili ya ibada yamewachochea watu wengi wahudhurie mikutano.

Kuwatafuta Kondoo wa Yehova Waliopotea

Kadiri kazi ya kuhubiri ilivyozidi kupamba moto, ofisi ya tawi ilipanga kampeni ya miezi miwili ili kuhubiri katika maeneo ambayo hayakuwa yamehubiriwa kwa ukawaida. Wahubiri waliwaachia watu karibu vitabu 15,000 na walifurahia mambo mengi mazuri yaliyoonwa. Watu fulani waliwaomba Mashahidi wa Yehova waanzishe makutaniko katika mojawapo ya miji yao. Matokeo ni kwamba makutaniko mapya mawili yalianzishwa. Katika kijiji kimoja cha mbali, akina ndugu waliwapata dada wawili ambao hawakuwa na mawasiliano yoyote na tengenezo kwa sababu ya vita. Mara moja, akina ndugu wakapanga mikutano ifanywe kwa ukawaida na wakaanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia katika kijiji hicho.

Mnamo 2009, ofisi ya tawi ilipata habari kwamba kuna watu kwenye kijiji fulani kilicho ndani kabisa ya msitu nchini Guinea ambao walidai kuwa Mashahidi wa Yehova. Baada ya kuwatuma akina ndugu kuchunguza, ofisi ya tawi ilitambua kwamba ndugu fulani mzee alirudi kijijini alikozaliwa baada ya kustaafu. Alijifunza na wanaume kadhaa kabla ya kufa. Mmoja wa wanaume hao alimwamini Yehova na akaanza kuwaambia watu kuhusu mambo aliyojifunza katika Biblia. Pia, aliongoza mikutano kwa kutumia machapisho ya yule ndugu aliyekufa. Kikundi hicho kilikuwa kikimwabudu Yehova kwa miaka 20 hadi mhubiri fulani alipogundua kwamba kuna kikundi hicho. Mara moja, ofisi ya tawi ilituma akina ndugu ili wakisaidie kiroho kikundi hicho. Mwaka 2012, watu 172 katika kijiji hicho walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo.

Katika siku za karibuni, idadi kubwa ya ‘kondoo waliopotea’ imekuwa ikipatikana. Kondoo hao ni wale ambao waliliacha au waliondolewa kutanikoni. Kondoo wengi kama hao, wamebadili maisha yao na kuirudia njia ya kweli. Watu wa Yehova wamewakaribisha kondoo hao kwa moyo mkunjufu kabisa.Luka 15:11-24.

Waislamu Wanyofu Waikubali Kweli

Alipokuwa akiwajulisha watu habari njema, mtume Paulo alikuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote.” (1 Kor. 9:22, 23) Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova nchini Sierra Leone na Guinea wamebadili utangulizi wao ili uwafae watu mbalimbali. Kwa mfano, ona vile wahubiri wanavyojadiliana na Waislamu wasio na msimamo mkali. Uislamu ndiyo kikundi kikubwa zaidi cha dini katika nchi zote mbili.

Saidu Juanah, ambaye zamani alikuwa Mwislamu, anaeleza hivi: “Waislamu wanaamini kwamba Adamu aliumbwa kutoka mavumbini lakini kwanza aliishi kwenye paradiso ya mbinguni. Ili kuwasaidia wapate maana sahihi, nawauliza hivi, ‘Mavumbi yanatoka wapi?’

“‘Duniani,’ wanajibu.

“‘Kwa hiyo ni lazima Adamu aliumbwa wapi?’ Ninaendelea.

“‘Duniani,’ wanajibu.

“Ili niwasaidie waelewe wazo kuu, ninasoma Mwanzo 1:27, 28 na kisha nawauliza, ‘Je, viumbe wa mbinguni wana watoto?’

“‘Hapana. Malaika si wanaume wala wanawake,’ wanajibu.

“‘Mungu alipowaambia Adamu na Hawa wazae watoto, ni lazima wawe walikuwa wapi?’ Ninawauliza.

“‘Duniani,’ wanajibu.

“‘Kwa hiyo Mungu atakaporudisha Paradiso, lazima Paradiso hiyo itakuwa wapi?’ Nawauliza.

“‘Hapa duniani,’ wananijibu.”

Saidu anamalizia hivi: “Kujadiliana kwa njia hiyo na kutumia Maandiko ifaavyo kunawachochea Waislamu wanyofu waendelee kusikiliza na kukubali machapisho yanayozungumzia Biblia.”

Mfikirie Momoh, Mwislamu muuza duka ambaye ali­tumaini kwamba siku moja angekuwa Imamu. Wakati wamishonari Mashahidi walipojadiliana naye kwa kutumia Maandiko, Momoh akaanza kuwa na maswali mengi. Alihudhuria sehemu fulani ya kusanyiko la mzunguko na akapenda mambo aliyosikia. Siku nne baadaye, yeye na mke wake, Ramatu, na watoto wao watano walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Kisha, Momoh alianza kujifunza Biblia kwa bidii. Baada ya kujifunza mara kadhaa aliacha kuuza sigara. Aliwaambia wateja wake kuwa sigara zinawadhuru watu na kwamba Mungu hakubaliani na uvutaji wa sigara. Pia, alianza kujifunza na mke na watoto wake hapohapo ­dukani kwake. Wateja walipokuja wakati familia ikijifunza, aliwaomba waketi na kusubiri akiwaeleza kwamba funzo hilo lilikuwa muhimu sana kwa familia yake. Yeye na Ramatu walipohalalisha ndoa yao, familia zao zikaanza kuwapinga vikali sana. Bila hofu yoyote, Momoh na Ramatu waliwatolea ushahidi kwa ujasiri watu wao wa ukoo, ambao baadaye walianza kuheshimu mwenendo wao mzuri. Momoh alibatizwa mwaka 2008, na Ramatu mwaka 2011.

Kuheshimu Utakatifu wa Damu

Watu wa Yehova hawayumbiyumbi inapohusu kuunga mkono viwango vya Mungu vya maadili, kutia ndani maoni yake kuhusu damu. (Mdo. 15:29) Msimamo huo unaheshimiwa na wataalamu wengi wa tiba nchini Sierra Leone na Guinea.

Akina ndugu wakimfariji dada hospitalini

Mwaka 1978, akina ndugu waliwapatia madaktari, wauguzi, viongozi wa hospitali, wanasheria, na mahakimu kotekote nchini Sierra Leone kijitabu Mashahidi wa Yehova na Suala la Damu. Muda mfupi baadaye, dada fulani aliyekuwa amepatwa na uchungu wa kuzaa alikuwa akivuja damu kwa ndani, lakini madaktari walikataa kumtibu bila damu. Hata hivyo, daktari mmoja alikubali kumsaidia kwa sababu ya elimu na mambo aliyokuwa amesoma kwenye kijitabu Damu. Dada huyo alijifungua mvulana mwenye afya nzuri na akapona kabisa.

Karibu mwaka 1991, Dk. Bashiru Koroma, daktari mpasuaji wa Hospitali ya Kenema, alisoma broshua Damu Yaweza Kuokoaje Uhai Wako? Alivutiwa sana na mambo aliyosoma hivi kwamba akaanza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Shahidi fulani mvulana mwenye umri wa miaka tisa alipopata aksidenti na kupasuka bandama, madaktari wa mvulana huyo walikataa kumfanyia upasuaji bila kutumia damu. Wakawaambia hivi wazazi wake, “Mchukueni mtoto wenu akafie nyumbani! ” Wazazi hao walimpeleka mvulana wao kwa Dk. Koroma, ambaye alifanikiwa kumtibu mtoto huyo.

Baada ya muda mfupi, Dk. Koroma akawa Ndugu Koroma—mteteaji thabiti wa matibabu yasiyohusisha damu. Madaktari wengine walimtenga kwa sababu ya msimamo wake, hata hivyo, wakati wote wagonjwa wake walipona. Baadaye, baadhi ya wafanyakazi wenzake walianza kumwomba msaada wa kushughulikia hatua fulani za upasuaji mgumu.

Tangu 1994, Dawati la Habari za Hospitali katika ofisi ya tawi jijini Freetown, limekuwa likiunda Halmashauri za Uhusiano na Hospitali katika nchi ya Sierra Leone na Guinea. Kwa upendo, halmashauri hizo zimewasaidia Mashahidi wengi wagonjwa na kuwashawishi wataalamu wengi wa tiba ili wawatibu Mashahidi bila kutumia damu.