SIERRA LEONE NA GUINEA
Ninaipenda Sana Nchi ya Sierra Leone
Cindy McIntire
ALIZALIWA 1960
ALIBATIZWA 1974
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Mmishonari tangu 1992. Alitumikia nchini Guinea na Senegal, na sasa anatumikia Sierra Leone.
NILIPOFIKA kwa mara ya kwanza katika nchi ya Sierra Leone, ilinichukua wiki mbili tu kuipenda. Nilishangazwa na jinsi watu walivyobeba mizigo mizito kichwani kwa njia rahisi sana. Majirani walikuwa na shughuli nyingi. Katika mitaa, watoto walifurahia michezo mbalimbali. Nilizungukwa na watu wachangamfu, waliopenda muziki, na mavazi yenye rangi mbalimbali.
Jambo linalonifurahisha zaidi ni kuhubiri. Wasierra Leone ni watu wakarimu kwelikweli. Wanaiheshimu Biblia na kusikiliza ujumbe wake. Mara nyingi, wao hunikaribisha katika nyumba zao. Ninapoondoka, wengine hunisindikiza hadi barabarani. Sifa hizo nzuri zinanisaidia kukabiliana na mambo mengine madogo-madogo, kama vile uhaba wa maji na kukatika-katika kwa umeme.
Kwa kuwa ningali mseja, wakati mwingine watu huniuliza ikiwa mimi huhisi upweke. Kwa kweli, nina mambo mengi ya kufanya hivi kwamba sihisi nikiwa mpweke. Maisha yangu yana kusudi.