Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Miaka Mia Moja Iliyopita—1914

Miaka Mia Moja Iliyopita—1914

“TUNAAMINI kwamba Mwaka wa 1914 unatupatia nafasi nzuri ya kuhubiri Kweli kuliko miaka mingine iliyopita ya Mavuno,” likaeleza gazeti Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1914. Mwaka ambao Wanafunzi wa Biblia walikuwa wakiutarajia kwa miaka kadhaa hatimaye ulifika, nao walikuwa na bidii katika huduma. Kwa sababu ya bidii ya Wanafunzi wa Biblia mwaka huo, mamilioni ya watu walisikia kuhusu ahadi za Biblia. Hata hivyo, ulimwengu uliowazunguka ulielekeza jitihada zake katika jambo tofauti kabisa.

 Vurugu Zaongezeka Duniani

Mapema mwaka wa 1914, moja kati ya matukio ya kikatili zaidi katika historia ya migomo ya wafanyakazi lilitukia Marekani na kusababisha mauaji ya wanaume, wanawake, na watoto. Wachimba-migodi waliogoma pamoja na familia zao walifurushwa kutoka kwenye nyumba za kampuni, na wakalazimika kuishi kwenye mahema. Tarehe 20 Aprili, risasi zilifyatuliwa katika mahema yaliyokuwa karibu na mji wa Ludlow, Colorado, na mahema yote kambini yakateketezwa. Wachimba-migodi wenye hasira kali walilipiza kisasi kwa kuua walinzi wengi wa kampuni katika eneo hilo. Jeshi liliitwa ili kurejesha utulivu.

Mambo yalikuwa mabaya zaidi barani Ulaya. Mnamo Juni 28, Gavrilo Princip, Mserbia kutoka Bosnia mwenye umri wa miaka 19, alimpiga risasi na kumuua Francis Ferdinand, Mwana-mfalme wa Austria. Jambo hilo lilisababisha Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Mwishoni mwa mwaka huo, Vita vya Kwanza vya Ulimwengu (wakati huo vilijulikana kama Vita Vikuu) vilikuwa vimeenea barani Ulaya.

Makusanyiko Yakazia Umuhimu wa Kazi ya Kuhubiri

Ghasia hizo zilipokuwa zikiongezeka, Wanafunzi wa Biblia walitiana moyo ili wawe na bidii katika kazi ya kuhubiri. Kusanyiko la kwanza la watu wa Mungu kufanywa nchini Afrika Kusini lilianza Aprili 10. Lilihudhuriwa na kilele cha watu 34. William W. Johnston aliandika: “Tulikuwa ‘kundi dogo’ sana. Karibu nusu ya [waliohudhuria] Kusanyiko walibatizwa. Ndugu nane na dada nane walionyesha wakfu wao kama Bwana alivyoagiza.” Siku ya mwisho ya kusanyiko hilo, wahudhuriaji walizungumzia jinsi ya kupanua kazi ya kuhubiri nchini Afrika Kusini. Leo, zaidi ya wahubiri 90,000 wanashuhudia mafanikio ya lile ‘kundi dogo.’

Juni 28, 1914, siku ileile ambayo Mwana-mfalme Ferdinand alipigwa risasi, Wanafunzi wa Biblia walikusanyika katika mji wa Clinton, Iowa, Marekani. Tarehe 30 Juni, A. H. MacMillan alisema hivi katika kusanyiko hilo: “Ikiwa tunataka kupokea  thawabu yetu, tunahitaji kuendelea kufanya mapenzi ya Mungu kwa bidii, kwenda utumishi kadiri hali zetu zinavyoruhusu.”

Mamilioni ya Watu Wavutiwa na Sinema ya “Photo-Drama”

Januari 11, 1914, sinema ya “Photo-Drama of Creation” yenye hotuba zilizorekodiwa zinazotegemea Biblia, na muziki ambao uliambatanishwa na slaidi za rangi na picha mbalimbali, ilionyeshwa kwa mara ya kwanza katika jiji la New York City. Watu elfu tano walitazama onyesho hilo la kwanza, na wengine wengi hawakuruhusiwa kuingia kwa sababu hakukuwa na mahali pa kuketi.

Ilichukua miaka miwili kutayarisha sinema ya “Photo-Drama of Creation,” hata hivyo gazeti la Mnara wa Mlinzi liliripoti kwamba, “sinema hiyo haikuwa tayari kuonyeshwa mbele ya umati katika mwezi wa Januari.” Katika miezi sita ya kwanza ya mwaka 1914, akina ndugu waliifanyia marekebisho kadhaa sinema hiyo. Kwa mfano, waliongeza sehemu ya utangulizi yenye maelezo ya Ndugu Charles Taze Russell, ambayo yalitaja waziwazi watu walioitayarisha.

Kwenye kilele cha maonyesho yake, sinema ya “Photo-Drama” ilionyeshwa katika majiji 80 hivi kwa wakati mmoja. Kufikia Julai 1914, sinema hiyo ilikuwa imefika Uingereza, na kuonyeshwa katika nyumba zilizojaa watu katika miji ya Glasgow na London. Kufikia Septemba, ilifika Denmark, Finland, Ujerumani, Sweden na Uswisi, na mwezi Oktoba ilifika Australia na New Zealand. Kwa ujumla, zaidi ya watu milioni tisa walikuwa wameitazama sinema ya “Photo-Drama” katika mwaka wake wa kwanza.

Kila nakala ya “Photo-Drama” ilikuwa na mamia ya slaidi, sinema, na habari nyingi zilizorekodiwa. Kutayarisha nakala za “Photo-Drama” ilikuwa ghali sana, na kila onyesho lilihitaji ndugu na dada wenye uzoefu. Kwa hiyo, sinema nzima ya “Photo-Drama” ilionyeshwa katika majiji makubwa tu. Ili kuwafikia watu vijijini, Wanafunzi wa Biblia walitayarisha sinema tatu zilizofupishwa za “Photo-Drama.” Sinema moja iliyofupishwa  iliitwa “Eureka Drama Y,” ilikuwa na slaidi za rangi zilizoambatanishwa na hotuba zilizorekodiwa zinazotegemea Biblia, pamoja na muziki. Nyingine ziliitwa “Eureka Drama X” na “Eureka Family Drama” ambayo ilikuwa fupi zaidi ya zote. Zote mbili zilikuwa na sauti tu bila slaidi za rangi wala picha. Hadi kufikia mwishoni mwa 1914, zaidi ya watu 70,000 nchini Marekani walikuwa wametazama sinema ya “Eureka Drama,” miezi minne hivi baada ya sinema hiyo kutolewa.

Makolpota na Wajitoleaji Washiriki Katika Kazi ya Kuhubiri

Ingawa kuonyesha watu sinema ya “Photo-Drama” lilikuwa jambo jipya na la kufurahisha, Wanafunzi wa Biblia walitambua kwamba njia nyingine za kuhubiri ndizo zilizohitaji kupewa kipaumbele. Barua ambayo Charles Taze Russell aliwatumia makolpota (sasa wanaitwa mapainia) ilisema hivi: “Hakuna njia nyingine ya huduma yenye matokeo zaidi katika kipindi hiki cha Mavuno. Kwa sababu hiyo, tunawatia moyo Makolpota wasifanye kazi ya kuonyesha watu Photo-Drama . . .  Ndugu na dada wengine, ambao pia ni waaminifu kwa Bwana . . . wanaweza kufanya kazi hiyo.”

Mnamo Januari 1914, kulikuwa na makolpota 850. Katika mwaka huo, waeneza-injili hao wenye bidii waligawa zaidi ya nakala 700,000 za mabuku ya Studies in the Scriptures. Waandishi wa gazeti la Mnara wa Mlinzi walionyesha jinsi “wanavyopendezwa” na makolpota na kuwachochea wasomaji wake “wawatie moyo; kwa kuwa kufanya kazi hiyo si jambo rahisi.”

Wanafunzi wengine wa Biblia waligawa trakti nyingi katika lugha mbalimbali. Katika mwaka 1914, waligawa zaidi ya nakala milioni 47 za trakti The Bible Students Monthly pamoja na trakti nyingine.

Bila shaka watu waliitambua kazi ya Wanafunzi wa Biblia. Walihubiri hadharani, na hawakuwatoza watu pesa katika mikutano yao. Mhudumu mmoja wa dini alisema hivi kwa huzuni: “Hivi punde watu wataanza kufikiri kwamba ni kosa kutoa sadaka, nasi tutaishije? Pasta Russell ametuharibia jina kweli kweli.”

Mwisho wa Nyakati za Mataifa

Wanafunzi wa Biblia waliamini kuwa ‘nyakati za Mataifa,’ zinazozungumziwa katika Luka 21:24, zingefikia mwisho wake karibu Oktoba 1, 1914. Matarajio yao yalizidi kuwa makubwa kadiri Oktoba ilivyokaribia. Baadhi ya Wanafunzi wa Biblia walibeba kadi za kuhesabia ili kuhesabu siku zilizosalia. Wengi walihisi kwamba wengechukuliwa kwenda mbinguni, au wangeingia ndani ya pazia tarehe hiyo.

Asubuhi ya Oktoba 2, 1914, Ndugu Russel aliingia katika chumba cha kulia chakula cha Betheli na kuitangazia familia ya Betheli hivi: “Nyakati za Mataifa zimekwisha; siku za wafalme wao zimekwisha.” Baadhi ya wale waliokuwapo walitambua maneno hayo, yaliyokuwa katika wimbo namba 171 kwenye kitabu cha nyimbo kilichoitwa Hymns of the Millennial Dawn. Tangu mwaka 1879, Wanafunzi wa Biblia walikuwa wakiimba “Nyakati za Mataifa zinakaribia kwisha,” lakini maneno hayo hayakuwa sahihi tena, kwa kuwa Nyakati za Mataifa, au  “nyakati zilizowekwa za mataifa” zilikuwa zimekwisha. (Luka 21:24)Kadiri wakati ulivyopita, mabadiliko hayo yameonekana wazi katika vitabu vyetu vya nyimbo.

Kadi ya kuhesabia iliyoitwa “Uwe Mwaminifu Mpaka Kifo” ilitumiwa na baadhi ya Wanafunzi wa Biblia walioazimia kubaki waaminifu hadi mwisho

Mwishoni mwa mwaka huo, Ufalme wa Kimasihi ulikuwa umesimamishwa mbinguni, na Wanafunzi fulani wa Biblia walifikiri kwamba kazi yao ilikuwa imekwisha. Hata hivyo, hawakujua kwamba walikuwa karibu kuingia kwenye kipindi cha kujaribiwa na kupepetwa. Andiko la mwaka 1915 lilikuwa “Munaweza kunywa kikombe nitakachokunywa?” lililotegemea Mathayo 20:22 katika tafsiri ya Zaire Swahili Bible. “Kikombe” ambacho Yesu alikuwa akizungumzia, kilitia ndani majaribu ambayo angekabili kabla ya kufa. Wanafunzi wa Biblia wangekabili majaribu kutoka kwa washiriki wenzao na nje ya kutaniko. Kuvumilia majaribu hayo kungethibitisha ushikamanifu wao kwa Yehova.