Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIERRA LEONE NA GUINEA

1915-1947 Siku za Mapema (Sehemu ya 2)

1915-1947 Siku za Mapema (Sehemu ya 2)

Kukabiliana na “Wapiganaji”

Makasisi jijini Freetown walipoona kwamba waumini wao wanafurahia hotuba za Ndugu Brown, walijawa na wivu na chuki. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 1923, lilisema hivi: “Makasisi wameanza kuishambulia kweli kupitia vyombo vya habari. Ndugu Brown amekuwa akiwajibu tena na tena kupitia magazeti yanayochapisha hoja za pande zote mbili.” Hatimaye makasisi walinyamaza na hoja zao za uwongo zikafunuliwa. Kweli za Biblia zilikuwa zimetangazwa kwa mapana na marefu na kuwafanya wasomaji wa magazeti ya habari kuomba machapisho yanayotegemea Biblia. Makasisi walikuwa wamekusudia kuwanyamazisha watu wa Mungu, lakini Yehova ‘aliyageuza madhara yao yarudi juu yao.’Zab. 94:21-23.

Kikundi cha vijana wa kanisa walioitwa Wapiganaji, kikaibuka ili kuwatetea makasisi. Kikundi hicho kikapanga mikutano mbalimbali ya dini ili kuukomesha “Uruseli,” kama walivyokuwa wakiuita ujumbe wa Ufalme. Ndugu Brown aliwaalika kwenye mijadala kadhaa. Lakini Wapiganaji waliukataa mwaliko huo na kumkemea mhariri wa gazeti aliyechapisha mwaliko wa Ndugu Brown. Pia, walimkataza Ndugu Brown asihudhurie mikutano yao, hata hivyo, Alfred Joseph alihudhuria.

Mikutano hiyo ilifanywa kwenye kanisa la kifahari la Methodisti la Buxton Memorial Chapel, jijini Freetown. Alfred anakumbuka hivi: “Wakati wa kipindi cha maswali na majibu, nilihoji kuhusu mafundisho ya Anglikana kama vile Utatu, na mafundisho mengine yasiyo ya kimaandiko. Hatimaye, mwenyekiti alinizuia nisiulize maswali zaidi.”

Mmoja kati ya Wapiganaji waliokuwepo usiku ule alikuwa Melbourne Garber, ambaye mapema alikuwa amesikiliza hotuba za “Bible” Brown. Kwa kweli, yeye ndiye yule kasisi kijana aliyesema, “Bw. Brown anaijua Biblia yake!” Baada ya kuchanganua mambo aliyosikia, Garber alisadikishwa kwamba alikuwa ameipata kweli. Hivyo basi, akamwomba Ndugu Brown amfundishe Biblia. Ndugu Brown alimkaribisha Garber kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi lililokuwa likifanywa kila juma nyumbani kwake. Ingawa familia yake ilimkataa, Garber alifanya haraka maendeleo ya kiroho, na baada ya muda mfupi yeye na watu wengine kadhaa walibatizwa.

Jitihada za Shetani za kuzuia kazi ya kuhubiri ilipokuwa ikianza hazikufanikiwa. Kama vile meya wa jiji la Freetown alivyowaambia washiriki wa kikundi cha Wapiganaji: “Ikiwa hii ni kazi ya wanadamu, basi itakoma. Lakini ikiwa ni kazi ya Mungu, hamtaweza kuizuia.”Mdo. 5:38, 39.

Dini ya Akina Brown

Mapema mwezi wa Mei mwaka 1923, Ndugu Brown aliwasiliana na ofisi ya tawi ya London akiomba atumiwe machapisho mengi zaidi. Muda si muda vitabu 5,000 vikatumwa, na baadaye akatumiwa machapisho mengine zaidi. Pia, aliendelea kufanya mikutano ya dini hadharani ambayo iliwavutia maelfu ya watu.

Baadaye mwaka huo, gazeti la Mnara wa Mlinzi liliripoti hivi: “Kazi [nchini Sierra Leone] inasonga mbele kwa kasi hivi kwamba Ndugu Brown ameomba msaada; hivyo, Claude Brown, wa Winnipeg, ambaye zamani aliishi katika visiwa vya West Indies, sasa yuko njiani kwenda kujiunga naye.”

Claude Brown alikuwa na uzoefu na bidii katika kazi ya kuhubiri habari njema. Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, alivumilia mateso kwenye magereza ya Kanada na ya Uingereza kwa kuwa alikataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri yake ya Kikristo. Alitumikia nchini Sierra Leone kwa miaka minne, akiwaimarisha ndugu na dada wenyeji.

Pauline Cole alieleza hivi: “Kabla sijabatizwa mwaka 1925, Ndugu Claude aliniuliza maswali kwa makini. Aliniuliza hivi:

 “‘Dada Cole, je, umeelewa mambo ambayo umejifunza kwenye mabuku ya Studies in the Scriptures? Hatutaki uiache kweli kwa sababu hukuyaelewa mafundisho ya Biblia.’

Nikamjibu, “‘Ndugu Claude, nimeyasoma tena na tena mambo niliyojifunza. Huo ndio uamuzi wangu!’”

Pauline Cole

Pauline alimtumikia Yehova kwa zaidi ya miaka 60, mingi kati ya miaka hiyo akiwa painia wa pekee. Alifikia mwisho wa maisha yake duniani mwaka 1988.

Pia, William “Bible” Brown alikuwa macho kuwasaidia wengine wakuze sifa nzuri za kiroho. Alfred Joseph anaeleza hivi: “Nilipokutana na Ndugu Brown asubuhi, mazungumzo yetu yangekuwa hivi: ‘Habari za asubuhi Ndugu Joe. Andiko la siku ya leo linasemaje?’ Ikiwa nisingejibu, angenisisitizia umuhimu wa kujua andiko la kila siku kutoka kwenye kitabu Daily Manna. [Sasa kinaitwa Kuyachunguza Maandiko Kila Siku.] Asubuhi iliyofuata ningesoma andiko la siku mara moja ili tukikutana tena niwe tayari kumjibu. Mara ya kwanza, sikuthamini sana umuhimu wa mazoezi niliyopata, lakini baadaye nilianza kuyathamini.”

Mazoezi hayo yalikuwa na matokeo mazuri. Mwaka 1923, kutaniko lilianzishwa jijini Freetown na watu 14 walibatizwa. Mmoja wa ndugu hao wapya alikuwa George Brown, ambaye alifanya idadi ya familia zenye jina “Brown” kutanikoni kuwa tatu. Bidii ya familia hizo tatu iliwafanya wakazi wengi wa jiji la Freetown kuwaita wanafunzi hao wa Biblia, dini ya akina “Brown.”

Pauline Cole