Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIERRA LEONE NA GUINEA

1915-1947 Siku za Mapema (Sehemu ya 3)

1915-1947 Siku za Mapema (Sehemu ya 3)

Kuhubiri Mikoani na Katika Maeneo ya Mbali Zaidi

Kutaniko la Freetown lilichochewa na kweli na hivyo likaanza “kushughulika sana na lile neno.” (Mdo. 18:5) Alfred Joseph anasimulia hivi: “Mara nyingi niliweka vitabu vinavyozungumzia Biblia ndani ya sanduku na kisha kuvibeba kwenye pikipiki yangu, halafu ningembeba Ndugu Thomas Grant au Sylvester Grant, na kuelekea vijijini, na katika miji midogo iliyo karibu na jiji la Freetown ili kuzungumza na watu.”

Kufikia mwaka 1927, wahubiri walikuwa wamehubiri kwa kiasi kikubwa ndani na kuzunguka Freetown katika eneo lililoitwa Colony. Hata hivyo, kuanzia mwaka 1928, kila mwaka kabla ya msimu wa mvua kuanza, kutaniko lilikodi basi na kusafiri hadi mikoani. Wale ambao hawangeweza kwenda walitoa michango ili kugharimia safari hizo. Melbourne Garber ndiye aliyeongoza safari hizo. Wahubiri hao walihubiri katika miji na vijiji vilivyo mashariki mwa Kailahun, na pia katika miji na vijiji vilivyo kusini hadi karibu na mpaka wa Sierra Leone na Liberia. Kila Jumapili ya kwanza ya mwezi, walirudi ili kuendeleza mazungumzo pamoja na watu waliopendezwa.

 Karibu na wakati huo, Ndugu Brown alitembelea West Indies na akarudi na gari ambalo lilikuwa miongoni mwa magari ya kwanza nchini Sierra Leone. Gari hilo lilikuwa na mfumo wa sauti wenye nguvu uliobuniwa kwa ajili ya mahubiri ya hadharani. Ndugu Brown angeegesha gari hilo mahali penye watu wengi na kufungulia muziki mzuri ili kuvutia umati. Kisha angetoa hotuba fupi au kucheza hotuba fulani iliyorekodiwa na kuwapa watu machapisho yanayozungumzia Biblia. Gari linalozungumza (kama lilivyojulikana wakati huo) liliwavutia watu wengi hivi kwamba walikusanyika ili kulisikiliza.

Wakitoa ushahidi kwa ujasiri

Kisha Ndugu Brown akaanza kuelekeza fikira zake katika maeneo ambayo hayakuwa yamehubiriwa, yaani, maeneo ya Afrika Magharibi yaliyotumia lugha ya Kiingereza. Mwishoni mwa miaka ya 1920, alianza kusafiri tena na tena nchini Gambia, Ghana, Liberia, na Nigeria ili kuhubiri. Ndugu Brown alipata watu waliopendezwa katika nchi hizo, hata hivyo, Nigeria ilionekana kuwa na watu wengi zaidi wanaopendezwa. Mwaka 1930, yeye na familia yake walihamia jijini Lagos. Akiwa jijini Lagos aliendelea kusimamia kazi ya Ufalme katika eneo la Afrika Magharibi.

Zaidi ya Mashahidi 500,000 sasa wanamtumikia Yehova katika nchi mbalimbali za Afrika Magharibi

Mnamo 1950, Ndugu Brown alilazimika kurudi nchini Jamaika kwa sababu ya matatizo ya afya, hata hivyo mambo aliyofanya bado yanakumbukwa. Kwa zaidi ya miaka 27, yeye na mke wake waliona idadi ya Mashahidi wa Yehova katika Afrika Magharibi ikiongezeka kutoka mashahidi wawili hadi zaidi ya 11,000. Walishuhudia kwa njia halisi utimizo wa unabii wa Isaya: “Mdogo atakuwa elfu na mnyonge atakuwa taifa lenye nguvu.” (Isa. 60:22) Leo, miaka 60 hivi baadaye, “taifa lenye nguvu” ambalo lina Mashahidi zaidi ya 500,000 wanamtumikia Yehova katika nchi mbalimbali za Afrika Magharibi.

Kusimama Imara Chini ya Marufuku

Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoanza kupiganwa barani Afrika, watu wa Yehova nchini Sierra Leone walishikilia msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote. (Mika 4:3; Yoh. 18:36) Serikali ya Uingereza iliwashutumu kwa madai ya kwamba ni wachochezi, hivyo ikaanza kufuatilia utendaji wao na kupiga marufuku machapisho yao. Pindi fulani maafisa wa forodha jijini Freetown walikamata machapisho yaliyokuwa yakiingizwa nchini na kuyachoma. Baadhi ya ndugu walikamatwa kwa sababu ya kuwa na machapisho yaliyopigwa marufuku, hata hivyo baada ya muda mfupi waliachiliwa huru. *

Licha ya marufuku, Mashahidi waliendelea kuhubiri. Pauline Cole alieleza hivi: “Ndugu fulani aliyekuwa mfanyakazi wa meli iliyofanya safari zake kwa ukawaida jijini Freetown aliendelea kutuletea magazeti ya Mnara wa Mlinzi. Tulitumia magazeti hayo kutoa chapa nyingine za ziada kwa ajili ya mikutano. Pia, tulichapisha vipeperushi vilivyozungumzia vichwa mbalimbali vya Biblia na kuvigawa kwa watu wote. Wakati uleule ndugu waliendelea kutoa hotuba za watu wote na kucheza hotuba zilizorekodiwa za Ndugu Rutherford, hasa katika vijiji vilivyo mbali na jiji la Freetown.”

Yehova alibariki sana jitihada hizo. James Jarrett, ambaye ametumikia kwa muda mrefu akiwa mzee na painia wa pekee, anakumbuka: “Vita vilipokuwa vikiendelea, nilikuwa nikifanya kazi ya kuchonga mawe dada fulani mzee aliponipa kijitabu Refugees (Wakimbizi). Kwa kuwa wakimbizi wengi walikuwa wakiingia jijini Freetown, kichwa cha kijitabu hicho kilinivutia sana. Nilisoma kijitabu hicho usiku huohuo na mara moja nikaitambua kweli. Asubuhi iliyofuata, nilimtafuta dada huyo na kumwomba nakala kadhaa kwa ajili ya ndugu zangu watatu. Sote wanne tuliikubali kweli.”

Vita vilipoisha mwaka 1945, Kutaniko la Freetown lilikuwa na wahubiri 32. Wahubiri hao walishikilia utimilifu wao na kubaki imara kiroho. Walikuwa na bidii na tayari kusonga mbele.

Kampeni ya Mkutano wa Watu Wote

Mnamo Agosti 29, 1945, katika Mkutano wa Utumishi wa kila wiki, Kutaniko la Freetown lilizungumzia kampeni iliyotangazwa kwenye Informant (sasa inaitwa Huduma Yetu ya Ufalme) toleo la Desemba 1944. Kila kutaniko lilipaswa kutangaza na kufanya mfululizo wa mikutano minne ya watu wote katika “kila jiji, mji, na kijiji” kwenye eneo lao. Kila mkutano ungekuwa na hotuba ya saa moja ambayo ingetolewa na ndugu (mwenye umri wa miaka 18 au zaidi) ambaye alikuwa amefanya vizuri katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Baada ya mikutano hiyo minne, ndugu wangepanga vikundi vya kujifunza Biblia ili kuwasaidia watu waliopendezwa katika maeneo yote hayo.

Wahubiri waliitikiaje mwongozo huo mpya? Rekodi za Mkutano wa Utumishi wa Kutaniko la Freetown zina maelezo yafuatayo:

Mwenyekiti: “Mnafikiri tunaweza kuifanya jinsi gani kampeni hii mpya?”

Ndugu wa Kwanza: “Tusitarajie kwamba tutakuwa na matokeo mazuri kama Marekani. Watu wa hapa ni tofauti.”

Ndugu wa Pili: “Nakubaliana nawe.”

Ndugu wa Tatu: “Ngoja tujaribu.”

Ndugu wa Nne: “Hata hivyo, haitakuwa rahisi.”

Ndugu wa Tano: “Lakini ni lazima tufuate mwongozo uliotolewa na tengenezo la Yehova.”

Ndugu wa Sita: “Sidhani kama kampeni hii inaweza kufanikiwa hapa kwetu.”

Dada wa Kwanza: “Licha ya hayo, mwongozo ulio kwenye Informant uko wazi. Acheni tujaribu!”

Basi wakafuata mwongozo huo. Hivyo, kuanzia pwani ya Freetown hadi katika jiji la Bo lililo kusini-mashariki, na pia kaskazini katika jiji la Kabala lililo katika nyanda za juu, akina ndugu walifanya mikutano kwenye madarasa, sokoni, na kwenye nyumba za watu binafsi. Utendaji huo ulichochea bidii ya kutaniko, na “neno la Yehova likaendelea kukua na kuenea.”Mdo. 12:24.

Hata hivyo, wahubiri walihitaji mazoezi ya kitheokrasi. Na Yehova akatimiza uhitaji huo.

^ fu. 11 Marufuku ilikoma mwaka 1948.