Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIERRA LEONE NA GUINEA

1945-1990 ‘Kuwaleta Wengi Kwenye Uadilifu’—Dan.12:3. (Sehemu ya 2)

1945-1990 ‘Kuwaleta Wengi Kwenye Uadilifu’—Dan.12:3. (Sehemu ya 2)

Kuheshimu Zawadi ya Ndoa

William Nushy alipokuwa akiendelea na mgawo wake, alitambua kwamba baadhi ya wahubiri hawafuati kanuni za Yehova zinazohusu ndoa. Watu fulani waliishi pamoja bila kuandikisha kisheria ndoa zao. Wengine walifuata desturi za kutofunga ndoa hadi mwanamke apate mimba, hivyo kuhakikisha kwamba watapata watoto katika ndoa yao.

Hivyo basi, Mei 1953, ofisi ya tawi iliyaandikia makutaniko yote barua iliyofafanua wazi viwango vya Biblia kuhusu ndoa. (Mwa. 2:24; Rom. 13:1; Ebr. 13:4) Watu hao walipewa muda ili waandikishe ndoa zao, ikiwa hawangefanya hivyo wangeondolewa kutanikoni.1 Kor. 5:11, 13.

Wahubiri wengi walifurahia rekebisho hilo. Hata hivyo, baadhi ya wahubiri waliona kwamba hakukuwa na haja ya kuwa na vikwazo hivyo. Zaidi ya nusu ya wahubiri katika makutaniko mawili waliacha kushirikiana na tengenezo la Yehova. Hata hivyo, wale ambao walibaki waaminifu waliongeza bidii, jambo lililothibitisha kwamba Yehova alikuwa akiwabariki.

 Baada ya jitihadi nyingi sana za akina ndugu, Jumba la Ufalme la Freetown lilitambuliwa rasmi kuwa mahali pa kuandikishia ndoa. Septemba 3, 1954, ndugu wakafanya kwa mara ya kwanza sherehe ya ndoa. Baadaye, serikali iliwapa akina ndugu wanaostahili mamlaka ya kusajili ndoa katika wilaya saba nchini Sierra Leone. Hilo liliwawezesha watu wanaopendezwa waandikishe ndoa zao na kustahili kuwa wahubiri wa habari njema.

Ndoa yafungwa kwenye Jumba la Ufalme

Watu wengi waliopendezwa ambao walikuwa na wake wengi walichukua hatua ya kuishi kulingana na kanuni za Mungu. Samuel Cooper, ambaye anaishi mjini Bonthe, anasimulia hivi: “Nilianza kuhudhuria mikutano mwaka 1957 nikiwa na wake zangu wawili, na baada ya muda mfupi nilijiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Siku moja, nilipewa mgawo wa hotuba iliyohusu ndoa ya Kikristo. Nilipokuwa nikifanya utafiti wa hotuba hiyo, nilitambua kwamba nilipaswa kumwacha mke wangu mdogo. Nilipowaambia ndugu zangu wa ukoo kuhusu jambo hilo, wote walinipinga. Mke wangu mdogo alikuwa amenizalia mtoto ilhali mke mkubwa alikuwa tasa. Hata hivyo, nilikuwa nimeazimia kufuata kanuni za Maandiko. Nilishangaa sana, kwani mke wangu mdogo aliporudi kwao, mke wangu mkubwa alianza kupata watoto. Sasa mimi na mke wangu aliyekuwa tasa tumepata watoto ­watano.”

Honoré Kamano, mwanaume mwingine aliyependezwa ambaye aliishi nchini Guinea, alipowaacha wake zake wawili kati ya watatu aliokuwa nao, mke wake wa kwanza alithamini msimamo wake na akaanza kuiheshimu sana kweli. Mmoja kati ya wake walioachwa na Kamano alipendezwa sana na msimamo wa mume wake wa kutii kanuni za Biblia licha ya kwamba alikuwa amevunjika moyo kwa sababu ya kuachwa. Aliomba afundishwe Biblia na baadaye aliweka maisha yake wakfu kwa Yehova.

Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana kuwa watu wanaoheshimu ndoa

Leo, Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana nchini Sierra Leone na Guinea kuwa watu wanaoheshimu ndoa. Uaminifu wao katika ndoa unayaletea sifa njema mafundisho ya Mungu na kumtukuza Mwanzilishi wa mpango wa ndoa.Mt. 19:4-6; Tito 2:10.

Mgawanyiko Jijini Freetown

Mnamo 1956, wahitimu wengine wawili wa Gileadi, Charles na Reva Chappell, waliwasili jijini Freetown. Wakiwa njiani kuelekea katika nyumba ya wamishonari walishtushwa na bango kubwa lililokuwa likitangaza hotuba ya Biblia ambayo ingetolewa kwenye ukumbi wa Wilberforce Memorial Hall. Charles anasema “mtoaji wa hotuba hiyo alikuwa C.N.D. Jones, mwakilishi wa ‘Kikundi cha Mashahidi wa Yehova.’”

Jones, ambaye alidai kuwa mtiwa-mafuta, alikuwa kiongozi wa kikundi kilichojitenga na kutaniko la Freetown miaka kadhaa mapema. Washiriki wa kikundi hicho walidai kuwa wao ndio mashahidi wa “kweli” wa Yehova na wakawaita wamishonari na wale waliobaki washikamanifu kwa wawakilishi wa tengenezo kuwa “walaghai” na “wahuni kutoka Gileadi.”

Mambo yaliharibika zaidi wakati Jones na baadhi ya wafuasi wake walipotengwa na ushirika. Ndugu Chappell anasema hivi: “Tangazo hilo liliwashtua baadhi ya ndugu ambao waliwavumilia wapinzani hao, na wachache kati yao walionyesha hadharani kutofurahishwa na hatua hiyo. Ndugu hao na wengine waliendelea kushirikiana na waasi hao na walijaribu kuvuruga mikutano na mipango ya utumishi wa shambani. Kwa hiyo, waliketi pamoja kwenye mikutano katika eneo lililopewa jina mgawanyiko. Hatimaye wengi wao waliiacha kweli. Hata hivyo, wengine walipata tena nguvu za kiroho na wakawa wahubiri wenye bidii.”

Ushikamanifu ulioonyeshwa na wengi ulisababisha roho takatifu ya Mungu itiririke kwa uhuru. Mwaka uliofuata mwangalizi wa eneo la dunia Harry Arnott alilitembelea jiji la Freetown, na kuripoti hivi: “Kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka kadhaa hatujawahi kuwa na ongezeko kubwa kadiri hii nchini Sierra Leone. Hilo linafanya kuwe na matumaini kwamba kutakuwa na ongezeko kubwa wakati ujao.”

Kuwafundisha Wakisi

Muda mfupi baada ya ziara ya Ndugu Arnott, Charles Chappell alipokea barua kutoka kwa ndugu aliyekuwa katika nchi ya Liberia. Ndugu huyo alitaka kuanza kuwahubiria ndugu zake wa ukoo nchini Sierra Leone. Ndugu huyo alikuwa Mkisi, watu wa kabila hilo huishi katika eneo la milima lenye misitu na mabonde yanayounganisha nchi za Sierra Leone, Liberia, na Guinea. Ilionekana kwamba watu waliokuwa wakizungumza Kikisi walitaka kujua Biblia.

Kwa kuwa Wakisi wengi hawakujua kusoma wala kuandika, madarasa ya kujifunza kusoma na kuandika yaliandaliwa mjini Koindu ili kuwafundisha kweli za msingi za Biblia. Madarasa hayo yaliwavutia mamia ya wanafunzi. Charles anakumbuka hivi: “Punde si punde kikundi hicho kikawa na wahubiri wapya watano, kisha 10, 15, halafu 20. Watu waliingia kwenye kweli kwa haraka sana hivi kwamba nilianza kutilia shaka ikiwa walikuwa wahubiri wa kweli. Lakini nilikuwa nimekosea. Wengi wao hawakuwa waaminifu tu, bali pia wahubiri wenye bidii!”

Baada ya muda mfupi wahubiri hao wapya wenye bidii walieneza habari njema hadi nje ya mji wa Koindu na hatimaye katika nchi ya Guinea. Walihubiri kwenye mashamba na vijiji walipokuwa wakitembea kwa saa nyingi kwenye milima na mabonde. Eleazar Onwudiwe, aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko wakati huo, anasema, “hatukusikia sauti ya gari kwa majuma, nyakati nyingine hata kwa miezi kadhaa.”

Kadiri ndugu na dada Wakisi walivyopanda na kumwagilia mbegu za Ufalme, ndivyo Mungu alivyozikuza. (1 Kor. 3:7) Kijana mmoja kipofu alipoisikia kweli, alikariri kijitabu “Habari Njema Hizi za Ufalme,” chenye kurasa 32. Baadaye, aliweza kukumbuka fungu lolote alipokuwa akihubiri na kuongoza mafunzo yake ya Biblia. Jambo hilo liliwashangaza sana watazamaji. Mwanamke mmoja kiziwi ambaye aliikubali kweli, alifanya mabadiliko makubwa hivi kwamba wifi yake akaanza kuhudhuria mikutano, akitembea zaidi ya kilometa kumi ili kufika kwenye mikutano hiyo.

Kazi katika eneo la Wakisi ilisonga mbele kwa kasi. Makutaniko mawili yakaanzishwa. Karibu wahubiri 30 walianza kazi ya utumishi wa upainia. Chifu wa mji wa Koindu alipendezwa na kweli na hivyo, akatoa kiwanja ili Jumba la Ufalme lijengwe. Zaidi ya watu 500 walipohudhuria kusanyiko la mzunguko mjini Kailahun, kutaniko lilianzishwa katika mji huo pia. Muda si muda, nusu ya wahubiri wote nchini Sierra Leone walikuwa Wakisi, hata ingawa idadi ya watu wa kabila hilo ilikuwa chini ya asilimia mbili ya idadi ya watu wote nchini humo.

Si watu wote waliofurahia maendeleo hayo, hasa viongozi wa kidini wa Wakisi. Wakiwa wamejawa na wivu, waliazimia kukomesha “tishio” hilo lililohatarisha mamlaka yao. Hata hivyo, akina ndugu hawakujua wakati na jinsi ambavyo wangeshambuliwa.