Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIERRA LEONE NA GUINEA

1945-1990 ‘Kuwaleta Wengi Kwenye Uadilifu’—Dan.12:3. (Sehemu ya 4)

1945-1990 ‘Kuwaleta Wengi Kwenye Uadilifu’—Dan.12:3. (Sehemu ya 4)

Kuwafundisha Watu Kusoma na Kuandika

Mapema mwaka 1963, wakati wa ziara yake ya pili nchini Sierra Leone, Milton Henschel alizungumzia jambo ambalo ofisi ya tawi ilikuwa imejitahidi kulitatua kwa muda mrefu. Aliwatia moyo ndugu waongeze jitihada zao za kuwafundisha watu kusoma na kuandika.

Baadhi ya makutaniko yalikuwa yakiendesha madarasa hayo kwa Kiingereza. Lakini baada ya ziara ya Ndugu Henschel, akina ndugu walianza kuwafundisha wanafunzi kusoma na kuandika kwa lugha zao za asili. Baadhi ya makutaniko yaliendesha madarasa hayo katika lugha mbili au tatu. Madarasa hayo yalijulikana sana hivi kwamba karibu asilimia 33 ya wahubiri wote nchini Sierra Leone walijiunga na madarasa hayo.

Mwaka 1966, akina ndugu nchini Liberia walitunga kijitabu cha kujifunzia kusoma na kuandika kwa ajili ya lugha ya Kikisi. Walipowaonyesha maofisa wa serikali ya Liberia kijitabu hicho, maofisa hao walivutiwa sana na kuamua kukichapisha na kukigawanya bila malipo. Kijitabu hicho kiligawanywa nchini Guinea, Liberia, na Sierra Leone, na kiliwasaidia mamia ya watu waliozungumza Kikisi kujifunza kusoma na kuandika. Hatimaye, vijitabu hivyo viliboreshwa na kuchapishwa katika lugha nyingine, hivyo kuwasaidia watu wengi zaidi kujua kusoma na kuandika.

Sia alirekodi utendaji wake wa kuhubiri kwa kutumia kamba nyeusi na nyekundu

Madarasa hayo hayakuwasaidia watu kujua kusoma na kuandika tu, bali pia yaliwasaidia kufanya maendeleo ya kiroho. Mfikirie Sia Ngallah, mhubiri mwenye umri wa miaka 50 ambaye hakujua kusoma wala kuandika, na wakati huo hakuwa amebatizwa. Dada Sia alirekodi utendaji wake wa kuhubiri kwa kutumia kamba nyeusi na nyekundu. Baada ya kuhubiri kwa saa moja, angefunga fundo moja kwenye kamba nyeusi. Baada ya kufanya ziara ya kurudia, angefunga fundo moja kwenye kamba nyekundu. Sia alijiunga na darasa la kujifunza kusoma na kuandika, ambalo lilimsaidia kutunza vizuri rekodi ya utendaji wake. Pia, alifanya maendeleo hadi kubatizwa na akaja kuwa mhubiri na mwalimu mzuri.

Leo, makutaniko mengi nchini Sierra Leone na Guinea bado yanafanya madarasa ya kujifunza kusoma na kuandika. Ofisa wa cheo cha juu katika serikali ya Sierra Leone aliwaambia hivi akina ndugu kwenye ofisi ya tawi: “Mbali na kazi yenu ya kuwafundisha watu Biblia, mnastahili pongezi kwa sababu ya kazi nzuri mnayofanya katika jamii ya kuwasaidia watu kujua kusoma na kuandika.”

“Mawe” Yapaaza Sauti

Kadiri watu wengi zaidi kutoka makabila mengine walivyozidi kujua kusoma na kuandika, ndivyo uhitaji wa kutafsiri ulivyoongezeka. Makabila mengi yalikuwa na vitabu vichache sana vya elimu katika lugha zao za asili. Wasomi nchini Sierra Leone walikuwa wanasoma Kiingereza na nchini Guinea walisoma Kifaransa. Ni nini ambacho kingefanywa ili waweze kusoma machapisho yanayotegemea Biblia katika lugha zao za asili?

Mwaka 1959, wahitimu wawili wa Gileadi walitafsiri trakti na kijitabu fulani katika lugha ya Kimende, lakini nakala chache tu ndizo zilizogawanywa. Miaka kumi baadaye, vijitabu “Habari Njema Hizi za Ufalme” na Kuishi Katika Tumaini la Taratibu Mpya Yenye Haki vilitafsiriwa katika lugha ya Kikisi. Vijitabu 30,000 hivi viligawanywa na vikatumiwa kuwafundishia watu Biblia.

Mnamo 1975, ofisi ya tawi ilianza kuchapisha makala za funzo la gazeti la Mnara wa Mlinzi katika lugha ya Kikisi. Wahubiri Wakisi walifurahi sana! Ndugu mmoja aliandika hivi: “Yehova ametufanyia jambo la ajabu sana. Hakuna yeyote kati yetu ambaye amepata nafasi ya kwenda shule. Ni kana kwamba tulikuwa kama mawe ambayo hayawezi kuzungumza. Lakini sasa kwa kuwa tuna gazeti la Mnara wa Mlinzi katika lugha ya Kikisi, tunaweza kuzungumza kuhusu matendo makuu ya Yehova.” (Luka 19:40) Machapisho mengine kadhaa yalitafsiriwa pia katika lugha ya Kikisi.

Leo, bado watu wengi nchini Sierra Leone na Guinea wanasoma machapisho yetu katika lugha ya Kiingereza au Kifaransa, lugha zinazotumiwa katika mikutano ya kutaniko. Hata hivyo, hivi karibuni idadi ya machapisho yanayotafsiriwa katika lugha za asili imeongezeka kwa kasi. Sasa machapisho yanayotegemea Biblia yanapatikana katika Kiguerze, Kikisi, Kikrio, Kimaninkakan, Kimende, Kipular, na Kisusu. Broshua Msikilize Mungu Uishi Milele na Msikilize Mungu zinapatikana katika lugha hizo zote. Machapisho hayo rahisi kufundishia yanawasaidia watu wengi ambao wana elimu kidogo waweze kuelewa na kuthamini ujumbe wa ajabu wa Biblia.

Kujenga Ofisi ya Tawi

Mwanzoni mwa miaka ya 1960, akina ndugu jijini Freetown walikuwa wakitafuta kiwanja ambacho ofisi mpya ya tawi ingejengwa. Hatimaye, mwaka 1965 walinunua kiwanja pembezoni mwa Barabara ya Wilkinson. Kiwanja hicho kilikuwa karibu na bahari katika mojawapo ya maeneo mazuri ya makazi jijini.

Ramani ya jengo la ofisi hiyo ilitia ndani Jumba la Ufalme, nyumba ya wamishonari, na ofisi. Mara nyingi ujenzi ulipokuwa ukiendelea, magari yaliendeshwa polepole sana hivi kwamba kulikuwa na foleni kubwa kwenye Barabara ya Wil­kinson, na hilo liliwawezesha madereva na abiria kuona vizuri ujenzi uliokuwa ukiendelea. Jengo hilo liliwekwa wakfu Agosti 19, 1967. Karibu watu 300 walihudhuria programu ya wakfu, walitia ndani watu maarufu nchini na Mashahidi kadhaa wa zamani waliobatizwa na “Bible” Brown mwaka 1923.

Ofisi ya tawi na nyumba ya wamishonari jijini Freetown (1965-1997)

Ofisi hiyo mpya ya tawi iliupandisha hadhi utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika akili za watu wengi. Pia, ilitoa jibu kwa baadhi ya wapinzani wa kidini ambao walisema kwamba Mashahidi wa Yehova hawangedumu nchini Sierra Leone. Jengo hilo jipya lilikuwa uthibitisho wa kwamba Mashahidi wa Yehova wangedumu nchini Sierra Leone.

Wamishonari Wenye Bidii Wachochea Ukuzi

Wahubiri wakipita katikati ya shamba la mpunga

Kuanzia katikati ya miaka ya 1970 na kuendelea, wamishonari waliozoezwa katika Shule ya Gileadi walichochea kazi nchini Sierra Leone na Guinea. Wengine walikuwa wametumikia katika nchi nyingine za Afrika na hivyo walizoea hali za nchi hizo haraka. Wengine ilikuwa mara yao ya kwanza kufika Afrika. Wangewezaje kukabiliana na “kaburi la wazungu”? Ona baadhi ya maelezo yao.

“Watu walikuwa wanyenyekevu na wenye njaa ya kiroho. Kuona jinsi ambavyo kweli iliboresha maisha yao kuliniridhisha sana.”Hannelore Altmeyer.

“Haikuwa rahisi kukabiliana na hali ya hewa ya joto na magonjwa. Lakini hayo hayakuwa kitu ukilinganisha na shangwe niliyopata ya kuwasaidia watu wamjue Yehova.”Cheryl Ferguson.

“Nilijifunza kusitawisha sifa ya subira. Nilipomuuliza dada fulani wageni wake wangekuja lini, alijibu: ‘Labda watakuja leo. Labda watakuja kesho. Au labda kesho kutwa.’ Ni lazima uso wangu ulionyesha kwamba nimepigwa na butwaa kwa sababu alinihakikishia hivi, ‘Lakini watakuja tu!’”Christine Jones.

“Wamishonari kumi na nne kutoka mataifa na tamaduni mbalimbali waliishi kwenye nyumba ya wamishonari jijini Freetown. Tulitumia vyoo viwili, bafu moja, mashine moja ya kufulia nguo, na chumba kimoja cha kupikia. Chakula hakikupatikana kwa urahisi na hakikuwa kizuri. Umeme ulikatika mara kwa mara—nyakati nyingine kwa siku kadhaa. Wengi wetu tuliugua malaria na magonjwa mengine ya kitropiki. Ingawa hayo yangetufanya tushindwe, tulijifunza jinsi ya kukaa pamoja, kusamehe, na hata kucheka kulipokuwa na hali ngumu. Kazi ya kuhubiri ilifurahisha sana, na wamishonari walikuwa na urafiki wa karibu.”Robert na Pauline Landis.

Pauline Landis akiongoza funzo la Biblia

 “Kipindi tulichokaa nchini Sierra Leone kilikuwa kati ya vipindi bora sana katika maisha yetu. Hatujuti wala kulalamika. Tunaikumbuka sana nchi hiyo.”Benjamin na Monica Martin.

“Siku moja tulilala kwa mwanamke fulani aliyekuwa amependezwa na habari njema. Alitupatia chakula fulani cha ajabu, kisha akasema: ‘Ni nyoka. Nimemng’oa meno yote. Je, mngependa kula kidogo?’ Tulijaribu kukataa kwa busara, lakini akaendelea kusisitiza tule. Licha ya kuwa tulijionea jambo kama hilo na mengine mengi yenye kutia hofu, kwa kweli tulithamini ukarimu wao na kuwapenda sana wenyeji wetu.”Frederick na Barbara Morrisey.

“Nimeishi na wamishonari zaidi ya 100 katika kipindi cha miaka 43 ya utumishi wangu wa umishonari. Limekuwa jambo lenye kugusa moyo sana kuwajua watu wengi kadiri hiyo, wote wakiwa na utu tofauti-tofauti lakini wakifanya kazi ili kutimiza lengo moja! Na ni furaha kubwa kuwa mfanyakazi mwenzi wa Mungu na kushiriki katika kazi ya kuwasaidia watu waijue kweli ya Biblia!”Lynette Peters.

“Ni furaha kubwa kuwa mfanyakazi mwenzi wa Mungu na kushiriki katika kazi ya kuwasaidia watu waijue kweli ya Biblia!”

Tangu mwaka 1947, wamishonari 154 wametumikia nchini Sierra Leone, na wengine 88 nchini Guinea. Mashahidi wengine wengi walikuja kusaidia kwenye maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Leo, kuna wamishonari 44 nchini Sierra Leone na wengine 31 nchini Guinea. Watu wengi wamesaidiwa kwa sababu ya jitihada na kujidhabihu kwao. Alfred Gunn, ambaye ni mshiriki wa muda mrefu wa Halmashauri ya Tawi, anasema hivi: “Tunawapenda na kuwakumbuka sana.”