Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIERRA LEONE NA GUINEA

2002-2013 Ongezeko la Karibuni (Sehemu ya 2)

2002-2013 Ongezeko la Karibuni (Sehemu ya 2)

Kuwasaidia Viziwi

Kulingana na kadirio fulani, karibu watu 3,000 hadi 5,000 nchini Sierra Leone na mamia ya watu nchini Guinea ni viziwi. Kwa kuwa ‘mapenzi ya Yehova ni kwamba watu wa namna zote waokolewe,’ basi viziwi wangejifunzaje habari njema?1 Tim. 2:4.

Michelle Washington, mmishonari aliyehitimu shule ya Gileadi na kuwasili nchini Sierra Leone mwaka 1998, anasimulia hivi: “Mimi na mume wangu, Kevin, tulipewa mgawo kwenye kutaniko ambalo viziwi wanne walikuwa wakihudhuria mikutano. Kwa kuwa ningeweza kuwasiliana nao kwa kutumia Lugha ya Ishara ya Marekani, nilitaka sana kuwasaidia. Ofisi ya tawi ilinipa mwaliko wa kukalimani mikutano na makusanyiko kwa ajili ya viziwi, na makutaniko yaliyo jirani yalijulishwa kuhusu mpango huo. Pia, ofisi ya tawi ilipanga kuwe na madarasa ya lugha ya ishara ili kuwafundisha wahubiri ambao wangependa kuwasaidia viziwi. Tulianza kuwatafuta viziwi na kisha kujifunza nao Biblia. Watu wengi walitupongeza kwa sababu ya bidii yetu ya kuwasaidia viziwi. Hata hivyo, si kila mtu alipendezwa na utendaji wetu. Kasisi fulani aliyekuwa mhudumu wa viziwi aliwaambia watu kwamba sisi ni ‘manabii wa uwongo.’ Hivyo akawaonya watu hao na familia zao watuepuke. Baadhi yao walionywa kwamba, ikiwa wangeshirikiana nasi basi msaada wao wa kifedha uliotolewa na kanisa ungesitishwa. Mara moja kukatokea makundi mawili ya viziwi: wale ambao hawajawahi kukutana nasi lakini walimuunga mkono kasisi huyo na wale ambao wamewahi kukutana nasi na hawamuungi mkono kasisi huyo. Baadhi ya viziwi katika kikundi hicho cha pili walikubali kweli na kisha wakafanya maendeleo na kubatizwa.”

Kwa mfano, Femi, alizaliwa kiziwi na angeweza kuwasiliana kwa kutumia ishara za msingi tu. Alimshuku kila mtu, hasa watu wenye uwezo wa kusikia, hakuwa na furaha na kuhisi hapendwi. Kisha akaanza kujifunza Biblia pamoja na ndugu walioshirikiana na kikundi cha lugha ya ishara. Baada ya muda mfupi alikuwa akihudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na alikuwa akijifunza lugha ya ishara. Femi alifanya maendeleo na kubatizwa, sasa anafurahia kuwafundisha kweli viziwi wengine.

Femi, (wa kwanza kulia)akiimba kwa lugha ya ishara wimbo wa ufalme

Mnamo Julai 2010, kikundi cha Lugha ya Ishara ya Marekani cha Freetown kikawa kutaniko. Pia, kuna vikundi vingine vya lugha ya ishara jijini Bo na Conakry.

Maskini Kimwili Lakini “Matajiri Katika Imani”

Biblia inafunua wazi kwamba Wakristo wengi wa karne ya kwanza walikuwa maskini kimwili. Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Mungu alichagua walio maskini kwa habari ya ulimwengu ili wawe matajiri katika imani.” (Yak. 2:5) Imani katika Yehova imewafariji na kuwapa tumaini wahubiri nchini Sierra Leone na Guinea.

Imani inazichochea familia nyingi maskini za Mashahidi wanaoishi vijijini wakusanye pesa kwa miezi kadhaa ili waweze kuhudhuria makusanyiko ya wilaya. Wengine wanapanda mazao ili waweza kupata pesa kwa ajili ya safari hizo. Vikundi vya wajumbe 20 hadi 30 wanajazana kwenye malori madogo yanayopita kwenye barabara mbaya, zenye vumbi na joto kali, na safari hizo zinaweza kuchukua hadi saa 20 au zaidi. Wajumbe wengine wanatembea umbali mrefu sana. Ndugu mmoja anasema: “Ili kufika kwenye kusanyiko, kwanza tulitembea umbali wa kilomita 80 tukiwa tumebeba mikungu ya ndizi. Tuliuza ndizi hizo njiani, na hivyo kupunguza mzigo tulio nao na kupata pesa zaidi za kutuwezesha kumalizia safari iliyobaki kwa kupanda lori.”

Kusafiri kwa lori ili kwenda kwenye kusanyiko la wilaya

Pia, imani imewachochea wahubiri wengi wapinge kishawishi cha kuhamia katika nchi zilizoendelea kiuchumi. “Tunaamini kwamba Yehova atatosheleza mahitaji yetu,” anasema Emmanuel Patton, mhitimu wa Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja. “Kwa kuwa tunaishi katika nchi yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme, tumetambua kwamba utumishi wetu ni kitu chenye thamani sana.” (Mt. 6:33) Sasa, Emman­uel anatumikia akiwa mzee wa kutaniko. Yeye na mke wake, Eunice, wanamtumikia Yehova kwa bidii. Wahubiri wengine ambao ni vichwa vya familia waliamua kutoenda ng’ambo ili walinde umoja na hali ya kiroho ya familia zao. “Nilikataa kazi ambayo ingenifanya niwe mbali na familia yangu kwa vipindi virefu vya wakati,” anasema Timothy Nyuma, ambaye alitumikia akiwa painia wa pekee na mwangalizi badala wa mzunguko. “Pia, mimi na mke wangu, Florence, tuliwasomesha watoto wetu katika shule zilizo karibu badala ya kuwapeleka mbali ili wakalelewe na watu wengine.”

Ndugu na dada wengine wanaonyesha imani kwa kutoacha utendaji wa Kikristo licha ya hali ngumu. Kevin Washington, aliyetajwa awali, anaeleza hivi: “Wahubiri wengi wanahubiri kwa ukawaida na kutimiza majukumu ya kutaniko licha ya kukabili matatizo ambayo huenda yangenifanya mimi na mke wangu tukae tu nyumbani au kuhama eneo hilo. Kwa mfano, baadhi yao wanaumwa magonjwa yanayosababisha maumivu makali sana na hawana namna ya kufika kwenye vituo vya afya na kupata dawa, mambo ambayo yanapatikana kwa urahisi mahali pengine. Wengine wanafanya jitihada kubwa ili wajifunze kusoma na kuandika. Nikianza kumkosoa sana ndugu kuhusiana na jinsi alivyoshughulikia mgawo fulani, huwa ninajiuliza hivi: ‘Ikiwa ningekuwa nafanya kazi kutwa nzima, ningekuwa na matatizo mengi ya afya, macho hayawezi kuona bila miwani, na maktaba yangu haingekuwa na machapisho ya kutosha na hakuna umeme, je, nisingeshughulikia mgawo huo kama ndugu huyo alivyoshughulikia?’”

Ndugu na dada nchini Sierra Leone na Guinea wamemtukuza Yehova katika njia hizo na nyingine nyingi sana. Kama vile Wakristo wenzao wa karne ya kwanza, wanajipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu “kwa kuvumilia mengi, kwa dhiki, kwa hali za uhitaji, . . . kama maskini lakini wenye kuwatajirisha wengi, kama wasio na kitu chochote na bado wenye kuwa na vitu vyote.”2 Kor. 6:4, 10.

Kuukabili Wakati Ujao kwa Ujasiri

Zaidi ya miaka 90 iliyopita, Alfred Joseph na Leonard Black­man waliripoti kwamba mashamba ya Sierra Leone yalikuwa “meupe kwa ajili ya kuvunwa.” (Yoh. 4:35) ­Karibu miaka 35 baadaye, Manuel Diogo kutoka nchi ya Guinea, aliandika hivi: “Kuna watu wengi sana wanaopendezwa hapa.” Leo, watumishi wa Yehova katika nchi zote mbili wanaamini kwamba bado kuna watu wengi zaidi ambao watakubali habari njema.

Mwaka 2012, watu 3,479 walihudhuria Ukumbusho nchini Guinea, idadi hiyo ni zaidi ya mara nne na nusu ya wahubiri wote nchini. Wahubiri 2,030 nchini Sierra Leone waliwakaribisha watu kwenye Ukumbusho na 7,854 wakahudhuria, idadi hiyo ni karibu mara nne ya wahubiri wote nchini. Winifred Remmie, painia wa pekee mwenye umri wa miaka 93, ambaye amemtumikia Yehova kwa miaka mingi, alihudhuria Ukumbusho siku hiyo. Yeye na mume wake, Lichfield, waliingia nchini Sierra Leone mwaka 1963. Baada ya kutumia miaka 60 katika utumishi wa wakati wote, bado alikuwa akitumikia akiwa painia wa pekee. Winifred alisema hivi: “Ni nani ambaye angewazia kwamba Sierra Leone ­ingekuja kuwa na ndugu na dada wengi na wenye nguvu kiroho. Ingawa nimezeeka, bado ninataka kushiriki shangwe ya ongezeko hili.” *

Mashahidi wa Yehova nchini Sierra Leone na Guinea wanahisi kama Winifred alivyohisi. Kama vile miti mizuri ambayo imemwagiliwa maji ya kutosha, wameazimia kuendelea kuzaa matunda ili kumsifu Yehova. (Zab. 1:3) Kwa msaada wa nguvu za Yehova wataendelea kutangaza tumaini halisi litakalowapa wanadamu uhuru wa kweli, yaani, “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”Rom. 8:21.

Halmashauri ya Tawi, kuanzia kushoto kwenda kulia: Collin Attick, Alfred Gunn, Tamba Josiah, na Delroy Williamson

Kusafiri kwa lori ili kwenda kwenye kusanyiko la wilaya

^ fu. 16 Winifred Remmie alikufa wakati simulizi hili likiandaliwa.