Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza

Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza

Watumishi Wenzetu Wapendwa:

Tunafurahi sana kuwaandikia barua hii mwanzoni mwa mwaka huu wa kihistoria! Kufikia mwishoni mwa 2014, karne moja itakuwa imepita tangu Mfalme wetu Yesu Kristo alipoanza kutawala katikati ya adui zake.Zab. 110:1, 2.

Mwanzoni mwa mwaka huu wa utumishi, katika mkutano wa mwaka wa shirika la Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, Halmashauri ya Kutafsiri Biblia ya Ulimwengu Mpya ilitangaza toleo la Kiingereza lililorekebishwa la tafsiri bora zaidi ya Biblia kuwahi kutafsiriwa. Yehova aliwatumia wana wake waliozaliwa kwa roho ili kutoa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya awali kabisa. (Rom. 8:15, 16) Bila shaka, jambo hilo linafanya tafsiri hii iwe ya pekee, sivyo?

Kwa miaka mingi, Halmashauri ya Uandikaji ya Baraza Linaloongoza imeipa kipaumbele kazi ya kutafsiri  Biblia. Leo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inapatikana katika lugha 121 ikiwa nzima au sehemu. Tunawatia moyo mwithamini sana Biblia hiyo ili Yehova aone jambo hilo waziwazi. Isomeni na kutafakari kila siku, kwa kufanya hivyo mtamkaribia zaidi Mtungaji wake, Yehova Mungu.Yak. 4:8.

Tunatiwa moyo sana tunaposikia ndugu na dada zetu wapendwa wanaendelea kuvumilia majaribu. Inaeleweka kwamba nyakati fulani huenda ikawa vigumu kwao kushangilia pamoja na ndugu zao. Kwa mfano, hivi karibuni barani Asia, maisha ya familia moja yamebadilika kabisa mama yao alipopooza ghafla. Wataalamu wa tiba walishindwa kabisa kutibu tatizo hilo. Inasikitisha sana! Sasa mume anamhudumia mke wake kwa saa 24. Mwana wao na binti zao wawili wanaweka mfano mzuri wakiwa Wakristo kwa kuwasaidia wazazi wao. Familia hiyo nzuri pamoja na ninyi nyote ambao mmefanikiwa kukabiliana na hali ngumu mnaweza kuhisi shangwe inayotokana na kuvumilia majaribu ya imani yenu. (Yak. 1:2-4) Yehova anawahakikishia watiwa-mafuta na kondoo wengine kwamba tutakuwa na furaha kwa sababu tuliendelea kuvumilia majaribu. Hatimaye, tutabarikiwa kwa kupewa zawadi ya uzima wa milele!Yak. 1:12.

Mwaka jana, hudhurio la Ukumbusho lilikuwa 19,241,252. Inatia moyo sana kuona watu wengi wakimheshimu Yehova na Yesu Kristo kwa kuhudhuria mkutano huo muhimu zaidi kwa watu wa Mungu unaofanywa kila mwaka! Wakati wa majira ya Ukumbusho, sauti kubwa za sifa zilipaa mbinguni watu zaidi ya milioni mbili walipotumikia wakiwa mapainia wasaidizi mwezi wa Machi na Aprili. Hilo linatia moyo sana! Bila shaka, mlifurahi kujua  kwamba wale wanaofanya upainia msaidizi wakati wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko wanaweza kuhudhuria mkutano mzima unaoongozwa na mwangalizi, hata ikiwa ziara yake haitafanywa mwezi wa Machi au Aprili! Wale wenye hekima kiroho wanaelewa umuhimu wa kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri na utendaji wa kutaniko. Kuwa na mengi ya kufanya kunatusaidia tubaki imara na thabiti, kupinga jitihada za Ibilisi za kuidhoofisha imani yetu na kutukengeusha.1 Kor. 15:58.

Ni jambo linaloimarisha kwelikweli kujua kwamba mwaka wa utumishi uliopita, watu 277,344 walionyesha wakfu wao kwa kubatizwa katika maji na sasa wako katika barabara inayoongoza kwenye uzima pamoja na ndugu zao ulimwenguni pote! (Mt. 7:13, 14) Wapya hao wanahitaji msaada wetu ili ‘waimarishwe katika imani.’ (Kol. 2:7) Endeleeni kutiana moyo ili mvumilie hadi mwisho. (Mt. 24:13) “Semeni kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika, tegemezeni walio dhaifu, iweni wenye ustahimilivu kuelekea wote.” (1 The. 5:14) Hivyo basi, sisi sote na ‘tusali bila kuacha,’ kwamba: “Ufalme wako na uje.”1 The. 5:17; Mt. 6:10.

Tafadhali, furahieni kusoma kitabu hiki, na jueni kwamba tunawapenda sana ninyi nyote mnaompenda Yehova!

Ndugu zenu,

Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova