Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 KUHUBIRI NA KUFUNDISHA DUNIANI KOTE

Oceania

Oceania
  • IDADI YA NCHI 29

  • IDADI YA WATU 39,508,267

  • IDADI YA WAHUBIRI 96,088

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 63,333

“Sasa Ninaelewa”

Freda, ambaye ni kiziwi, alifurahi sana alipojua kwamba yeye na dada aliyekuwa akimfundisha Biblia wangejiunga na kutaniko la kwanza la lugha ya ishara nchini Papua New Guinea. Kutaniko hilo lilianzishwa Machi 1, 2013. Sasa Freda alielewa mikutano vizuri zaidi kwa kuwa alikazia fikira ishara zilizotolewa badala ya kusoma machapisho. Kwa kufanya hivyo, alishinda woga na kuanza kutoa  maelezo mara kadhaa kwenye mikutano. Mnamo Aprili 2013, alistahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa na anafanikiwa kuwachochea viziwi wengine kwenda naye kwenye mikutano. Alipoulizwa kwa nini mara nyingi hutokwa na machozi wakati wa mikutano, alijibu, “Kwa sababu sasa ninaelewa.”

Aliingia Kwenye Gari la Mtu Mwingine

Alipokuwa akienda kwenye kikundi cha utumishi wa shambani nchini Australia, Barbara aliegesha gari lake kando ya barabara ili kutafuta daftari lake la ziara za kurudia. Ghafla mwanamke fulani alifungua mlango wa gari na kuingia.

“Samahani,” akasema Barbara, “sidhani hili ni gari lako.”

“Pole,” mwanamke huyo akajibu. “Nilidhani wewe ndiye mwanamke aliyepaswa kuja kunichukua.” Alipoona magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, mwanamke huyo alisema, “zamani nilikuwa nikipata magazeti haya kutoka kwa wanawake wawili waliokuwa wakinifundisha Biblia.” Barbara alifurahi kumpa magazeti hayo na baadaye akaanza kujifunza naye Biblia.

“Barua Kutoka kwa Mungu”

New Zealand: Violet anawafundisha kweli watu wengi kupitia barua

Violet ni dada mgonjwa mwenye umri wa miaka 82 anayeishi jijini Christchurch, New Zealand. Yeye hutuma kwa ukawaida barua na machapisho kwenye makao ya kuwatunzia wazee na makao ya wagonjwa mahututi. Wauguzi wanaomtunza ambao hupeleka barua hizo wanasema kwamba wazee wanaoishi kwenye makao hayo husubiri kwa hamu barua kutoka kwa Mungu,  kama wanavyoziita. Baadhi yao husoma barua na machapisho hayo na kubadilishana na wengine au kuwasomea kwa sauti wasio na uwezo mzuri wa kuona. Pia, wauguzi hao wanasema kwamba wazee wanaosoma barua na machapisho hayo ni watulivu, wenye mtazamo unaofaa, na wenye amani zaidi kuliko wale wasiosoma. Violet anasema hivi kuhusu jitihada zake za kuhubiri: “Ninahisi kwamba bado Yehova ananitumia kuwasaidia wengine. Kuwaambia wengine kweli kwa njia hiyo hunitia moyo sana.”

 Alisoma Kuhusu Waridi

“Tayari nimelisoma.” Jibu hilo ambalo hakutazamia lilimshangaza Bernie Jumamosi moja asubuhi alipokuwa akiwapa watu magazeti ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi katika kisiwa cha Saipan. Alijiuliza, Bernadette, ambaye ni mwanafunzi wa chuo, anawezaje kuwa tayari amelisoma gazeti hili? Bernie alipomwonyesha gazeti lingine tofauti, Bernadette alimwambia, “Hata hilo nimelisoma.” Akiwa amepigwa na butwaa, Bernie alimwuliza: “Ulisoma wapi magazeti haya? Kwani wewe ni Shahidi wa Yehova na umekuja hapa kwa ajili ya likizo?” Bernadette alimweleza kwamba yeye si Shahidi, bali alikuwa amesoma magazeti hayo kwenye mtandao. Siku moja alipokuwa akifanya utafiti kwenye Intaneti kuhusu maua, Bernadette aliandika neno “waridi” na alishangaa kuona kichwa cha makala moja ya Amkeni!, “Waridi Maridadi Kutoka Afrika” kilichokuwa katika Tovuti ya Mashahidi wa Yehova. Bernadette alimwambia Bernie kwamba alifurahia sana makala hiyo, hivi kwamba aliamua kuchunguza Tovuti hiyo kwa undani. Kwanza alitafuta tu habari zilizohusu mimea na wanyama lakini punde si punde akagundua kwamba kulikuwa na habari zenye kupendeza kuhusu Biblia. Alipotambua kwamba Bernadette anapendezwa na habari za Biblia, Bernie alimwuliza ikiwa angependa kujifunza Biblia bila malipo, na baadaye akarudi na kumpa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Bernie alipomtembelea Bernadette mara ya tatu, walianza kujifunza sura ya kwanza ya kitabu hicho. Mwaka mmoja hivi baadaye, Novemba 2012, Bernadette alibatizwa. Bernadette alifanya maendeleo haraka sana hivi kwamba marafiki wake walisema kwamba alipata kweli “ghafla bila kutarajia.” Kwa kweli Tovuti yetu ilimpa mwanzo mzuri.