Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MATUKIO MUHIMU YA MWAKA ULIOPITA

JW.ORG—“Ushahidi kwa Mataifa Yote”

JW.ORG—“Ushahidi kwa Mataifa Yote”

Yesu alisema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14) Kwa kweli, Tovuti ya jw.org imefanikiwa sana kuyafikia “mataifa yote” katika muda mfupi ambao umebaki kabla ya mwisho kuja.

Walipokuwa wakihubiri katika kijiji kimoja cha wavuvi katika Visiwa vya Solomon, wenzi wa ndoa ambao ni wamishonari walikutana na wanaume wanne wazee. Walipoona kwamba wanaume hao walikuwa na simu za mkononi, wamishonari hao waliwauliza ikiwa walijua jinsi ya kutumia Intaneti. Walijua. Wenzi hao waliwaonyesha jinsi ya kufungua Tovuti ya jw.org, jinsi ya kupata lugha yao, jinsi ya kupakua magazeti na Biblia, na jinsi wanavyoweza kutumia ile sehemu ya familia na watoto. Wanapokuwa shambani, wamishonari hao hufurahia kuwaonyesha watoto ile video kuhusu sala, Pray Anytime. Baada ya kikundi kimoja cha watoto kuona video hiyo, walikimbilia kichakani huku wakiimba kwa furaha wimbo ulio kwenye video hiyo.

Ulaanbaatar, Mongolia

Zifuatazo ni baadhi ya barua nyingi za shukrani ambazo zimetumwa kwenye makao yetu makuu jijini New York:

“Mimi na mume wangu tulihamia Mexico, na tunajifunza Kihispania ili tuweze kumhubiria kila mtu tunayekutana naye. Kila mara ninapofungua tovuti ya jw.org, ninamshukuru Yehova kwa sababu imenisaidia kusikiliza na kujifunza. Ina vitu vingi sana—magazeti, vitabu, muziki, na drama—katika lugha nyingi sana. Ninawapenda na asanteni sana kwa kazi yenu.”—D.H., Mexico.

“Ninakaribia kuwa kipofu, na ninapenda sana Tovuti yenu kwa sababu ina machapisho mengi yaliyorekodiwa ambayo ninaweza kusikiliza. Ninawaandikia kuwatia moyo mwendelee kuweka vitabu, broshua, na machapisho mengine kwenye faili za kielektroniki, yaani, MP3 ili niweze kuzisikiliza siku nzima.”—K.G., Marekani.

“Ninaipenda Tovuti ya jw.org! Ni rahisi kutumia na imenichochea niwe na bidii ya kujifunza kibinafsi na kuhubiri. Nina umri wa miaka 72, nimebatizwa kwa miaka 47, nimekuwa painia kwa miaka zaidi ya 30. Nina watoto 9 waliobatizwa, wajukuu 16, na vitukuu 3. Sasa tuna mapainia wa kawaida wa vizazi vinne katika familia yetu. Ninamshukuru Yehova kwa chakula hiki cha kiroho kinachotolewa kwa wakati unaofaa.”—M.T., Marekani.

“Ninaandika barua hii saa 10:00 alfajiri. Mara nyingi sipati usingizi usiku kwa sababu ya ugonjwa wa neva na magonjwa mengine ambayo pia yanawapata ndugu na dada zetu wa kiroho ulimwenguni pote. Yehova anaendelea kututunza kiroho, na ningependa kuwashukuru kwa sababu ya jambo hilo. Mimi hujifunza kupitia picha, na kwa hiyo muundo wa Tovuti yetu hunisaidia sana. Ninashukuru sana kwa chati, video fupi, picha, na maelezo yake yaliyo wazi.”—B.B., New Zealand.

“Hii ni barua ya kuwashukuru. Mimi ni daktari katika eneo la mbali nchini Sri Lanka, ambako ni vigumu kupata magazeti katika lugha yangu. Lakini kupitia Tovuti yenu, ninaweza kupakua na kuyasoma. Tovuti yenu ni mojawapo ya zawadi bora ambazo Yehova amewapa watu kama mimi.”—N.F., Sri Lanka.

“Ninawaandikia ili kuwashukuru kwa kazi mnayofanya ya kuwasaidia watu wajifunze kumhusu Yehova. Tafadhali endeleeni kuweka video kwenye jw.org. Video hizo zimenisaidia mimi na familia yetu kutatua matatizo. Video iliyonisaidia sana ni Mshinde Mnyanyasaji Bila Kutumia Ngumi. Asanteni sana kwa kazi yenu.”—Y.S., mwenye umri wa miaka 9, Marekani.

“Ningependa kuwashukuru ninyi na Yehova kwa chakula cha kiroho tunachopata. Tovuti ya jw.org imenisaidia sana, hasa ile sehemu ya ‘Matineja.’ Pia asanteni kwa ule mfululizo wenye kichwa Uwe Rafiki ya Yehova. Nina dada wadogo watatu, na ninaona matokeo mazuri ya habari hiyo. Ingawa tuko mbali sana nanyi, tunafurahia undugu wenye umoja kwa sababu sote tunampenda Yehova. Asanteni sana.”—A.B., Peru.