Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MATUKIO MUHIMU YA MWAKA ULIOPITA

Kutembelea Maonyesho ya Historia ya Mashahidi wa Yehova

Kutembelea Maonyesho ya Historia ya Mashahidi wa Yehova

 

Mnamo Oktoba 2012, maonyesho ya historia ya Mashahidi wa Yehova yalifunguliwa kwa mara ya kwanza huko Brooklyn, New York. Wale wanaotembelea maonyesho hayo hawahitaji mtu wa kuwaongoza. Maonyesho hayo yanakazia jitihada za wale waliofuata Ukristo aliofundisha Yesu na hatari walizokabili.

Katika juma la kwanza, zaidi ya watu 4,200 waliotia ndani wageni na washiriki wa familia ya Betheli walitembelea maonyesho hayo. Naomi, Shahidi anayeishi karibu na mahali hapo, alitembelea maonyesho hayo mara tu yalipofunguliwa. Alisema hivi: “Mfuatano wa matukio ulinisaidia kujua wakati na sababu zilizofanya mambo yatendeke kwa njia fulani. Nilijifunza mambo mengi kuhusu tengenezo letu na historia yake ya sasa.”

 Maonyesho yanaanza na historia ya Ukristo tangu mwaka wa 33 W.K. hadi leo. Maonyesho hayo yamepangwa katika sehemu nne. Kila sehemu ina kichwa kinachotegemea Andiko na inaanza kwa video fupi inayochezwa katika Kiingereza, na maelezo mafupi katika lugha saba.

Sehemu ya kwanza ina kichwa, “Watu Wamelipenda Giza,” kinachotegemea maneno ya Yesu kwenye Yohana 3:19. Biblia ilitabiri kwamba baada ya mitume kufa, watu waovu ‘wangesimama na kusema mambo yaliyopotoka.’ (Matendo 20:30) Wale ambao walijaribu kupinga mafundisho hayo waliadhibiwa vikali.

Kinyume na hilo, sehemu inayofuata yenye kichwa, “Nuru na Iangaze,” kinachotegemea andiko la 2 Wakorintho 4:6, inaelezea mfuatano wa matukio kuanzia mwishoni mwa miaka ya 1800 wakati wanafunzi wanyofu wa Biblia walipoanza kujifunza Maandiko. Waliacha mafundisho waliyoamini kwa muda mrefu ambayo hayapatikani katika Biblia na wakahubiri kwa ujasiri nuru ya kweli. Sehemu hii inazungumzia jinsi ujuzi na idadi yao ilivyoongezeka kabla ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu.

Kisha, chumba kinachofuata kinakazia jambo linalowashangaza Mashahidi wa Yehova hadi leo. Mwaka wa 1914 Wanafunzi wa Biblia (kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo) walianza kuonyesha sinema ya “Photo-Drama of Creation.” Mamilioni waliona sinema hiyo iliyokuwa na picha na sauti. Vitu vilivyowekwa katika chumba hicho vinatia ndani picha za awali, sauti zilizorekodiwa za utangulizi wa sinema hiyo, na slaidi zaidi ya 500 zenye rangi.

 Mateso ambayo Shetani anawaletea wafuasi wa Kristo yanayotajwa kwenye Ufunuo 12:17, ndicho kichwa cha sehemu ya tatu “Yule Joka Mkubwa Akawa na Ghadhabu.” Inakazia msimamo wa Wakristo wa kutounga mkono upande wowote wakati wa vita. Video fupi zinafafanua zaidi picha na vitu vya kale vinavyoonyesha jitihada zilizofanywa ili kuwalazimisha ndugu waliokataa kwenda vitani kwa sababu ya dhamiri wavunje msimamo wao. Mfano mmoja ni Remigio Cuminetti kutoka Italia, aliyekataa kuvaa sare za jeshi au kupigana katika Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Video nyingine inaonyesha Alois Moser kutoka Austria. Alikataa kusema “Heil Hitler” na hivyo alipoteza kazi yake na mwishowe akapelekwa kwenye kambi ya mateso ya Dachau. Gereza lenye mwangaza hafifu linamsaidia mtu kuelewa vizuri picha zinazoonyesha hali ambazo Mashahidi wa Yehova walikabili walipokuwa wamefungwa kwa sababu ya imani yao nchini Japani, Poland, Ugiriki, Yugoslavia ya zamani, na nchi nyingine.

Sehemu ya mwisho yenye kichwa, “Habari Njema kwa Mataifa Yote,” kinachotegemea Ufunuo 14:6, inakazia utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika miaka ya karibuni. Ukuzi wao wa haraka, bidii yao ya kuhubiri, na upendo wao wa kindugu unaonyeshwa katika picha zilizobandikwa ukutani. Pia, kuna vibanda kadhaa vyenye kompyuta ambazo mtu anaweza kufungua na kutembelea majengo yaliyoitwa Bible House na Brooklyn Tabernacle ambayo yalitumiwa na Mashahidi wa Yehova zaidi ya miaka 100 iliyopita.

Maonyesho hayo yako kwenye jengo lililo katika barabara ya 25 Columbia Heights huko Brooklyn, New York. Yanafunguliwa Jumatatu hadi Ijumaa, kuanzia saa 2:00 asubuhi hadi saa 11:00 jioni, na hakuna kiingilio. Ikiwa uko jijini New York City, unaalikwa kutembelea maonyesho hayo ya historia ya Mashahidi wa Yehova.