Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MATUKIO MUHIMU YA MWAKA ULIOPITA

Habari Fupi Kutoka Sehemu Mbalimbali Ulimwenguni

Habari Fupi Kutoka Sehemu Mbalimbali Ulimwenguni

Polisi Walisaidia Kushusha Matofali

Kwa miaka 13 makusanyiko yalikuwa yakifanywa kwenye kiwanda kilichochakaa cha shampeni jijini Kutaisi, ambalo ndilo jiji la pili kwa ukubwa katika Jamhuri ya Georgia. Walitumia karatasi za plastiki ili kuzuia maji ya mvua yasiwamwagikie wasikilizaji. Sasa akina ndugu wana Jumba la Ufalme jipya na zuri ambalo linaweza kupanuliwa na kutumiwa kwa ajili ya makusanyiko. Wakati wa ujenzi, wajitoleaji 50 walipokuwa wakishusha matofali ya saruji kutoka kwenye lori, polisi walifika ili kuona ni nini kilichokuwa kikiendelea. Wakiwa wamevutiwa na shangwe na bidii ya wafanyakazi hao, polisi waliwapongeza na kisha wakawasaidia kushusha matofali hayo. Waliwaambia ndugu hao kwamba wasisite kuwaita ikiwa mtu yeyote atawasumbua. Polisi hao waliahidi kwamba watahudhuria kusanyiko la kwanza litakalofanywa kwenye Jumba hilo jipya la Kusanyiko.

Aliuza Baiskeli Yake

Malachi, mzee wa kutaniko nchini Burundi, alijipatia riziki kwa kulima na kusafirisha mizigo kwa baiskeli yake. Malachi aliamua kufika kila siku kwenye eneo la ujenzi ili kushiriki katika ujenzi wa Jumba lao la Ufalme. Ili afanye hivyo, alihitaji pesa kwa ajili ya mahitaji ya familia yake kwa muda wa miezi miwili ya ujenzi. Kwa hiyo, aliuza baiskeli yake na kumpa mke wake kiasi fulani cha pesa hizo kwa ajili ya matumizi ya familia, na aliweka kiasi kilichobaki kwenye sanduku la michango kwa ajili ya ujenzi. Matokeo ya jitihada zake ni kwamba alipata mazoezi mazuri kutoka kwa watumishi wa ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Baada ya Jumba la Ufalme kukamilika, Malachi alipata kazi za ujenzi kwa kuwa watu walimwona kuwa mjenzi stadi. Sasa Malachi amefanikiwa kununua baiskeli nyingine!

Walichochewa Kusaidia

Kujenga Majumba ya Ufalme katika maeneo ya mbali nchini Malawi hutokeza matatizo yasiyo ya kawaida. Katika mwaka wa utumishi uliopita, jumba moja lilijengwa katika eneo lenye barabara mbaya sana. Akina ndugu katika ofisi ya tawi walitumia magari yenye uwezo wa kupita kwenye barabara mbovu ili kufikisha vifaa vya ujenzi katika eneo hilo. Ndugu wenyeji walisema kwamba watu wa eneo hilo walivutiwa sana na mradi huo. Watu wengi ambao si Mashahidi katika eneo hilo walijitolea kufanya kazi hadi usiku wakishusha mchanga, mawe, mifuko ya saruji, na mabati. Kwa kweli, nyakati nyingine wale ambao hawakuwa Mashahidi walikuwa wengi kuliko Mashahidi! Jitihada za Mashahidi wa Yehova za kujenga mahali penye kuheshimika pa ibada katika eneo hilo la mbali ziliwavutia sana wakazi wa huko hivi kwamba walichochewa kusaidia.

Watoto Waliuza Peremende

Wenzi fulani wa ndoa ambao ni mapainia wa pekee nchini Côte d’Ivoire wanajifunza Biblia katika Kibete pamoja na wazazi wenye watoto kumi. Kusanyiko la kwanza katika Kibete lingefanywa katika mji wa Daloa mnamo Mei 2013, na kila mtu katika familia hiyo alitaka kuhudhuria. Hata hivyo, nauli ya kwenda na kurudi kwa mtu mmoja ilikuwa faranga 800 (dola 1.60 za Marekani) na baba huyo hangeweza kulipia nauli ya familia yote. Kwa kuwa waliazimia kuhudhuria, alitokeza wazo fulani. Alimpa binti yake mkubwa faranga 300 (dola 0.60 za Marekani) na kupendekeza kwamba aanze kuuza peremende, na binti huyo akafanya hivyo. Alipata faida ya kutosha kulipia nauli yake. Baba huyo aliwapa wale watoto wengine faranga 300 kila mmoja ili waanzishe biashara ya kuuza peremende hadi wote walipoweza kupata nauli kwa ajili ya safari. Hatimaye, walihudhuria kusanyiko hilo pamoja na watu wengine. Walifurahi sana kusikiliza programu hiyo katika lugha yao ya asili!