Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MATUKIO MUHIMU YA MWAKA ULIOPITA

Kuwekwa Wakfu kwa Ofisi za Tawi

Kuwekwa Wakfu kwa Ofisi za Tawi

Oktoba 20, 2012, Mashahidi wa Yehova nchini Korea walifurahi sana majengo yao ya ofisi ya tawi yaliyokarabatiwa na yale mapya yalipowekwa wakfu kwa Yehova. Tukio hilo lilikuwa muhimu sana kwa kuwa akina ndugu walikumbuka miaka 100 ya utumishi mwaminifu. Isitoshe, katika mwaka wa 2012, idadi ya wahubiri ilipita 100,000. Wajitoleaji wenyeji 1,200 hivi na watumishi na wajitoleaji wa kimataifa 239 kutoka nchi tisa walijenga jengo jipya la makao, kiwanda cha kuchapisha, studio, na gereji. Zaidi ya hilo, majengo mengi ya zamani yalikarabatiwa kabisa.

Anthony Morris, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya wakfu iliyowatia moyo ndugu na dada 3,037 waliohudhuria. Siku iliyofuata, mkutano maalumu ulifanywa kwenye ukumbi mkubwa wa maonyesho, na zaidi ya makutaniko 1,300 nchini Korea yaliunganishwa kupitia Intaneti. Jumla ya Mashahidi wa Yehova na watu wanaopendezwa 115,782 walifurahia sana programu hiyo nzuri ya kiroho.

Machi 9, 2013, itakumbukwa kwa muda mrefu kuwa tarehe muhimu katika historia ya waabudu wa Yehova nchini Liberia. Wageni kutoka nchi 11 walikusanyika kwa ajili ya kuwekwa wakfu kwa ofisi ya tawi iliyokarabatiwa na kupanuliwa. Wahudhuriaji wote walifurahia sana kusikiliza hotuba ya wakfu iliyotolewa na Guy Pierce, mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Baada ya mipango ya ujenzi kuchelewesha kwa sababu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyodumu kwa zaidi ya miaka kumi, ofisi ya tawi ilipanuliwa na kuunganishwa na uwanja uliopakana nayo ambao awali ulitumiwa kama maficho ya waasi na kambi ya wakimbizi. Washiriki 51 wa familia ya Betheli wanafurahia kuishi kwenye jengo lenye vyumba 35, ofisi zilizokarabatiwa, bohari jipya la machapisho, jengo jipya la idara ya udumishaji, na jengo jipya lenye chumba cha kulia chakula na jiko.

Jamhuri ya Georgia ni nchi yenye watu wachangamfu wanaopenda mambo ya kiroho. Baada ya Muungano wa Sovieti kuvunjika, kulikuwa na kipindi cha ukuzi mkubwa wa kitheokrasi kilichofuatiwa na kipindi cha mateso makali. Upinzani umepungua kwa kiasi kikubwa, na tukio muhimu katika historia ya Mashahidi wa Yehova nchini Georgia lilitukia Jumamosi, Aprili 6, 2013, David Splane wa Baraza Linaloongoza alipotoa hotuba ya kuweka wakfu ofisi ya tawi iliyokarabatiwa na kupanuliwa, Jumba la Kusanyiko, na jengo jipya kwa ajili ya Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme, na pia Shule ya Waangalizi Wanaosafiri na Wake Zao. Wageni 338 kutoka nchi 24 walijiunga na Mashahidi wenyeji zaidi ya 800 kwa ajili ya programu ya wakfu.

Georgia

Siku iliyofuata, watu 15,200 walisikiliza hotuba ya pekee ya Ndugu Splane walipounganishwa kwa simu au video katika mahali pa ibada kotekote nchini Georgia. Tukio hilo la kimataifa liliwagusa sana watu wengi. Ndugu mmoja kijana alisema, “Sasa ninajua jinsi ulimwengu mpya utakavyokuwa.”

Juni 29, 2013, jengo jipya la ofisi lenye ghorofa tatu katika Betheli iliyo jijini Yangon, Myanmar, liliwekwa wakfu. Guy Pierce wa Baraza Linaloongoza aliwatolea hotuba ya wakfu wasikilizaji 1,013 ambao walitia ndani wageni kutoka nchi 11. Mwanaume fulani anayeishi katika nchi ambayo kazi ya Mashahidi wa Yehova imepigwa marufuku, aliwakaribia ndugu na dada waliokuwa wakiwakaribisha wageni hao kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Yangon. Akinyooshea kidole mabango yenye maandishi “Karibuni Mashahidi wa Yehova” waliyokuwa wameshika aliwauliza, “Je, mnawakaribisha mashahidi kwa ajili ya kesi fulani mahakamani?” Mashahidi wakamjibu, “Hapana, tunawakaribisha rafiki zetu.” “Na huyu Yehova ni nani?” mwanaume huyo akauliza. Pasipo shaka, ndugu na dada zetu walimtolea ushahidi mzuri. Siku iliyofuata programu ya wakfu, mkutano maalumu ulifanywa kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Myanmar, ambako Ndugu Pierce alizungumzia hotuba yenye kichwa, “Mtumikie Yehova kwa Moyo Wenye Uelewaji.” Maeneo sita nchini humo yaliunganishwa kwa simu, hivyo watu 2,963 walisikiliza habari hiyo iliyotolewa kwa wakati unaofaa. Dereva mmoja wa basi ambaye alisafirisha kikundi cha ndugu na dada wenyeji kwenye programu hiyo maalumu jijini Yangon alisema hivi: “Nimeona kwamba ninyi mko tofauti kabisa na dini nyingine. Mna tabia nzuri, mnavaa vizuri, na wenye fadhili sana. Nimebeba vikundi vya watu mbalimbali kwa miaka mingi, lakini sijawahi kamwe kuona watu wastaarabu kama ninyi!”

Myanmar: Wahubiri wenyeji wakiwakaribisha wageni kwa ajili ya programu ya kuwekwa wakfu kwa ofisi ya tawi

Watumishi washikamanifu wa Yehova nchini Moldova walikuwa na sababu nzuri ya kushangilia siku ya Jumatano, Julai 3, 2013, Stephen Lett wa Baraza Linaloongoza alipotoa hotuba ya wakfu wa majengo ya ofisi ya tawi yaliyopanuliwa hivi karibuni. Majengo hayo yanatia ndani jengo lenye ghorofa tatu lililo na bohari la machapisho na vyumba kumi vya makao, na pia Jumba la Ufalme lenye ghorofa mbili ambalo linatumiwa na makutaniko saba. Washiriki 33 wa familia ya Betheli nchini Moldova walifurahi kuwakaribisha wageni kutoka Ireland, Marekani, Rumania, Uholanzi, Ujerumani, Ukrainia, na Urusi. Pia, kati ya wale waliohudhuria kulikuwa na ndugu na dada ambao walimtumikia Yehova kwa uaminifu chini ya marufuku, hata baadhi yao walisaidia kunakili machapisho na kuyagawanya wakati huo. Pia miongoni mwa wahudhuriaji kulikuwa na ndugu na dada wengi ambao walisafirishwa pamoja na wazazi wao hadi Siberia wakati wa kampeni mbalimbali dhidi ya Mashahidi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti. Jumapili, Ndugu Lett alitoa hotuba yenye kuchochea iliyotafsiriwa katika Kirumania na Kirusi kwa ajili ya wahudhuriaji 14,705. Huo ulikuwa mkusanyiko mkubwa zaidi wa Mashahidi wa Yehova kuwahi kufanywa nchini Moldova.

Endeleeni Kusali Bila Kukata Tamaa

Yesu alikazia kwamba tunapaswa ‘kusali bila kukata tamaa.’ (Luka 18:1) Mnaposali, tumaini lenu linaimarishwa. Hivyo, “salini bila kuacha,” naam, “dumuni katika sala.” (1 The. 5:17; Rom. 12:12) Mnapoendelea kufanya hivyo, “Mungu wa amani . . . na awape ninyi vifaa vyema vya kila namna ili kufanya mapenzi yake, akifanya katika [ninyi] kupitia Yesu Kristo lile ambalo linapendeza vema machoni pake.”Ebr. 13:20, 21.