Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

KUHUBIRI NA KUFUNDISHA DUNIANI KOTE

Oceania

Oceania
  • IDADI YA NCHI 29

  • IDADI YA WATU 40,208,390

  • IDADI YA WAHUBIRI 97,583

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 64,675

Waliacha Vifurushi vya Machapisho

Visiwa vingi vya Micronesia havijahubiriwa kwa ukawaida, hivyo kikundi cha wahubiri kutoka Visiwa vya Marshall kilipanga safari ya majuma mawili kwa mashua. Walianza safari katika kisiwa cha Majuro kwenda visiwa vya Wotje na Ormed, vilivyoko Wotje Atoll.

Ili kuwatolea ushahidi watu wengi iwezekanavyo, kikundi hicho kiliandaa vifurushi vya machapisho kabla ya kuanza safari. Kila kifurushi kilikuwa na magazeti manne na broshua mbili. Kwa kuwa wahubiri hao hawakujua siku ambayo wangerudi kwenye kisiwa hicho, waliwaachia waliopendezwa vifurushi hivyo na kuwatia moyo wajifunze na familia na marafiki. Katika safari hiyo ya majuma mawili, wahubiri hao waliwaachia watu broshua 531, magazeti 756, na vitabu 7.

“Asante kwa Kutukumbuka”

Mnamo Februari 2014, Mashahidi sita kutoka Papua New Guinea walianza ziara ya siku kumi ya kuhubiri kwenye vijiji vya eneo la kisiwa cha volkano cha Karkar. Watu wengi waliitikia vizuri na wakawaachia machapisho 1,064. Dada anayeitwa Relvie anasema hivi: “Siku ya kwanza tulihubiri mpaka saa 9:00 alasiri. Tuliishiwa na maji ya kunywa, na kwa sababu ya kuongea bila kupumzika, taya zetu zilichoka na midomo yetu ilikauka. Nilikuwa nikizungumza na msichana mdogo. Nilitaka kumsomea andiko, lakini nilishindwa kwa sababu nilihisi kiu sana. Mara moja akanipa maji ya kunywa.”

Jioni moja kabla hatujaondoka katika kijiji kimoja, kulikuwa na mkutano mkubwa katika kijiji hicho, na viongozi wa kidini walikuwepo. Relvie anasema, “Nilihisi kama Stefano mbele ya Sanhedrini wakati alipohitaji kuitetea kweli, tofauti ni kwamba wasikilizaji wetu walikuwa wenye urafiki.” Baada ya wahubiri sita kumaliza kuzungumza, kiongozi wa shule ya Jumapili ya Kanisa la Kilutheri alisimama na kumshukuru mama yake mkubwa, ambaye alikuwa miongoni mwa wahubiri hao, kwa kuwaletea watu wake habari njema. Kiongozi huyo alimwambia hivi: “Mfano wako mzuri ni kama wa yule mwanamke Msamaria aliyeenda kuiambia familia yake kuhusu mambo mazuri aliyosikia kutoka kwa Yesu. Asante kwa kutukumbuka.”

Si Wachanga Mno Kuhubiri

Kiribati: Teariki na Tueti

Asubuhi moja, Teariki, mvulana wa miaka saba katika kisiwa cha Tarawa, ambacho ni sehemu ya Kiribati, alikuwa akihubiri pamoja na baba yake aitwaye Tueti. Walipoingia kwenye nyumba moja, walikutana na kikundi cha wanaume na wanawake kumi hivi wenye umri wa miaka 20 hivi. Baada ya baba ya Teariki kuzungumza na kikundi hicho kuhusu ujumbe wa Ufalme, mmoja wao alimwambia Tueti hivi: “Tumegundua kwamba nyote huambatana na watoto wenu mnapoenda kuhubiri. Kwa nini mnawalazimisha? Ni wachanga mno kuhubiri kuhusu Mungu.”

Tueti alijibu hivi: “Je, mngependa kujua ikiwa kijana wangu anaweza kuhubiri? Labda nitoke nje, ili mmsikilize.” Wote wakasema, “Ndiyo, tungependa kumsikia.”

Tueti alipotoka nje, Teariki aliwauliza hivi: “Je, mnajua jina la Mungu?”

Mmoja wao akajibu, “Ndiyo. Ni Yesu!” Mwingine akasema hivi: “Ni Mungu.” Na mwingine akasema, “Bwana.”

Teariki akawaambia: “Acheni tuone Biblia inasema nini. Tunaweza kufungua andiko la Isaya 42:5, na kulisoma pamoja.” Baada ya kusoma andiko hilo, akawauliza hivi: “Andiko hili linazungumza kuhusu nani?”

Mmoja wao akajibu hivi: “Mungu.” Kisha Teariki akasema: “Ndiyo, Mungu wa kweli. Tukisoma mstari wa nane, Mungu wa kweli anatuambia nini? ‘Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu, nami sitampa mwingine yeyote utukufu wangu mwenyewe.’ Je, mmeona jina la Mungu?”

Wakajibu, “Yehova.”

Kwa kuwa wote walisikiliza kwa makini, Teariki aliwauliza hivi: “Je, kuna manufaa yoyote ya kutumia jina la Mungu, Yehova? Natusome andiko la Matendo 2:21 ili tupate jibu. Linasema: ‘Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.’ Kuna manufaa gani ya kutumia jina la Mungu?”

Mmoja wao akajibu, “Tutaokolewa”

Ndipo baba ya Teariki alipoingia tena chumbani. Kisha akawauliza hivi: “Sasa mnaonaje? Je, vijana wetu wanaweza kuhubiri? Je, ni sawa tuambatane nao?” Wote walikubali kwamba watoto hao walijua kuhubiri na walistahili kushiriki katika kazi hiyo. Kisha Tueti akasema, “Nyinyi pia mnaweza kuwahubiria wengine kama Teariki alivyofanya, kama mngekuwa mmejifunza Biblia.”

Habari Njema Zafika Kwenye Kijiji cha Mlimani

Katika mwezi wa Novemba 2013, Jean-Pierre anayetumikia katika ofisi ya utafsiri iliyoko mji wa Port-Vila, Vanuatu, alisafiri kwenda kisiwa cha kwao ili kuhudhuria kusanyiko la mzunguko. Jean-Pierre alipowasili, kikundi cha watu wanaopendezwa wanaoishi kusini mwa kisiwa hicho walimfikia na kuomba machapisho ya Biblia. Aliwaachia karibu magazeti yote aliyokuwa amebeba. Pia, kiongozi wa kidini alimwomba machapisho. Kiongozi huyo wa kidini alimwomba aende kijijini kwao, akisema: “Tuna njaa ya kiroho. Unapaswa kuja kijijini kwetu ili ujibu maswali yetu yote.” Siku moja baada ya kusanyiko, asubuhi na mapema, Jean-Pierre alianza safari ndefu ya kupanda mlima mkali. Mwishowe alifika kijiji cha mbali sana kilichokuwa juu mlimani. Baada ya kukaribishwa vizuri na wenyeji wa kijiji hicho, Jean-Pierre alizungumzia Trakti Habari za Ufalme Na. 38 yenye kichwa “Je, Kweli Wafu Wataishi Tena?” Aliwatia moyo wasikilizaji wote, watu 30 hivi, kufungua Biblia zao anaposoma maandiko. Mazungumzo hayo yaliendelea kwa saa saba hivi. Wanakijiji hao walikuwa na njaa ya kiroho kwelikweli! Mwanaume mmoja mwenye miaka 70 alisema hivi: “Katika maisha yangu yote, sijawahi kamwe kusikia maelezo kama hayo yaliyo wazi kuhusu wafu!”

Jean-Pierre alilala kwenye kijiji hicho. Alilala kwa mchungaji. Alipoamka asubuhi, mchungaji huyo alikuwa anasoma mojawapo ya magazeti yetu. Jean-Pierre alimuuliza alichokuwa akisoma, na mchungaji huyo akasema kwa furaha kwamba anasoma kuhusu Ufalme wa Mungu. Alikubali kwamba Ufalme wa Mungu haukuwa ndani ya mioyo ya Mafarisayo, ambao Yesu aliwashutumu katika andiko la Luka 17:21. Akafikia mkataa kwamba Ufalme wa Mungu hauwezi kuwa ndani ya moyo wa mtu, kama kanisa lake linavyofundisha. Hata baada ya kurudi Port-Vila, Jean-Pierre anaendelea kuwasiliana kwa simu na watu wanaopendezwa katika kijiji hicho. Ndugu watatu kutoka kutaniko jirani walijitolea kufanya mipango ya Ukumbusho katika kijiji hicho, na watu 109 walihudhuria!

Vanuatu