Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mapilgrimu wenye bidii walikuwa miongoni mwa washiriki wa Ndugu Russel

Miaka Mia Moja Iliyopita—1916

Miaka Mia Moja Iliyopita—1916

MWANZONI mwa mwaka wa 1916, Vita Kuu, inayojulikana kuwa Vita vya Kwanza vya Dunia ilikuwa imedumu kwa zaidi ya mwaka. Watu wengi walikufa.

Gazeti The Watch Tower la Januari 1, 1916, liliripoti hivi: “Vita hiyo iliwachochea watu wengi kuwa wanadini kwa kuwa walihofia wakati wao ujao.” Makala hiyo iliongeza hivi: “Acheni tuthamini pendeleo na fursa tunazopata, kwa kuendelea kuwa jasiri na wenye bidii kwa ajili ya Mungu na Ujumbe Wake.”

Andiko la mwaka wa 1916 liliwahimiza akina ndugu kuendelea kuwa na ‘nguvu katika imani,’ kulingana na Waroma 4:20 King James Version. Wanafunzi wengi wa Biblia (Mashahidi wa Yehova) walifanya hivyo, nao walibarikiwa sana na Yehova.

Mapilgrimu Waliandaa Kitiamoyo

Wawakilishi wa Watch Tower Society walioitwa mapilgrimu walisafiri kutoka mji mmoja hadi mwingine ili kuwapa maagizo na kuwatia moyo Wanafunzi wa Biblia. Mwaka wa 1916, mapilgrimu karibu 69 hivi walisafiri kilometa 800,000 ili kufanya kazi yao.

Pilgrimu aitwaye Walter Thorn akiwa kusanyikoni huko Norfolk, Virginia, aliilinganisha vita ya Kikristo na Vita Kuu: “Inakadiriwa kwamba kuna wanaume milioni 20 hadi 30 hivi ambao wako vitani. . . . Kuna askari wengine ambao ulimwengu hauwajui. Ni askari wa Bwana, na kama askari wa Gideoni wanapigana vita, lakini bila silaha halisi. Wanapigania kweli na uadilifu, na vita yao ni vita nzuri ya imani.”

Kutumikia Licha ya Hali Ngumu za Vita

Nchini Ufaransa, watu zaidi ya milioni moja walijeruhiwa au kuuawa katika lile Pigano la Kwanza la Somme, mwishoni mwa mwaka wa 1916. Katika maeneo mengine nchini Ufaransa ndugu walishirikiana na madarasa au makutaniko licha ya hali ngumu sana za vita. Gazeti The Watch Tower la Januari 15, 1916, lilichapisha barua ya Joseph Lefèvre, Mwanafunzi wa Biblia aliyelazimika kuhama mji wa Denain, Ufaransa, ulipovamiwa na majeshi ya Ujerumani mwaka wa 1914. Alihamia Paris na akaanza kushirikiana na darasa la Wanafunzi wa Biblia katika jiji hilo. Licha ya hali mbaya ya afya, alianza kuongoza mikutano yote.

Baadaye, Théophile Lequime ambaye pia alihama kutoka Denain, aliungana na Joseph. Mwanzoni Ndugu Lequime alipohama Denain alienda Auchel, Ufaransa, ambako alianza kutafsiri makala za gazeti The Watch Tower na kuzituma kwa ndugu waliokuwa katika maeneo mengine ya Ufaransa yaliyokuwa salama. Mamlaka ya kijeshi ilimlazimisha Ndugu Lequime aondoke Auchel kwa sababu ya kutilia shaka kazi yake. Ndugu Lequime alipowasili jijini Paris, Ndugu Lefèvre alihisi kwamba sala yake imejibiwa.

Kazi yao ilibarikiwa sana jijini Paris. Ndugu Lefèvre aliripoti hivi: “Sasa tuna darasa lenye watu 45 hivi . . . Wengi wamejua uzuri na umuhimu wa kujidhabihu, na wanafanya maendeleo makubwa ya kiroho. Karibu washiriki wote wanahudhuria mikutano ya ushuhuda ya kila juma.”

Hawakuunga Mkono Upande Wowote

Vita ilipokuwa ikiendelea, ndugu wengi walikabili suala la kutounga mkono upande wowote. Nchini Uingereza, Sheria ya Utumishi wa Jeshi ilipitishwa kwamba wanaume wote wenye umri wa miaka 18 hadi 40 waende jeshini. Hata hivyo, Wanafunzi wengi wa Biblia walidumisha msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote.

Kwa mfano, gazeti The Watch Tower la Aprili 15, 1916, lilichapisha barua ya W. O. Warden kutoka Scotland. Alieleza hivi: “Mtoto wangu mmoja amefikisha miaka 19. Kufikia sasa ametoa ushahidi mzuri kwa ajili ya Bwana kwa kukataa kujiandikisha jeshini, na hata ikimaanisha kifo bado atakataa. Ninatumaini kwamba Yehova atamsaidia ili aendelee kusimama imara kwa ajili ya kweli na uadilifu.”

James Frederick Scott, kolpota kijana kutoka Edinburgh, Scotland, alishtakiwa kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi. Baada ya kusikiliza ushahidi, mahakama iliamua kwamba Ndugu Scott hakuwa na hatia kwa “mujibu wa sheria.”

Hata hivyo, ndugu wengine wengi hawakuachiliwa. Kufikia Septemba, kati ya ndugu 264 ambao waliomba kuachiliwa, 23 walipangiwa kazi zisizohusisha vita. Baadhi ya waliobaki “waliteswa kwa njia mbalimbali,” na walipelekwa kufanya “kazi za Ujenzi wa Taifa kama vile kujenga barabara, uchimbaji wa madini na kazi nyinginezo,” liliripoti gazeti Watch Tower la Oktoba 15, 1916. Ni ndugu watano tu waliosamehewa kujiunga na jeshi.

Kifo cha Charles Taze Russell

Oktoba 16, 1916, Charles Taze Russell, aliyekuwa akiongoza kazi ya Wanafunzi wa Biblia wakati huo, alianza ziara ya kutoa hotuba magharibi mwa Marekani. Hata hivyo, hakurudi kutoka safari yake. Alasiri ya Jumanne, Oktoba 31, Ndugu Russell mwenye umri wa miaka 64 alikufa akiwa ndani ya garimoshi katika Pampa, Texas.

Ndugu wengi walianza kujiuliza yule ambaye angechukua mahali pa Ndugu Russell. Wasia wake ulioandikwa katika gazeti The Watch Tower la Desemba 1, 1916, ulieleza nia yake kuhusu kazi aliyokuwa anaiongoza kwa muda mrefu. Hata hivyo, swali lilikuwa: Ni nani atakayekuwa mrithi wake?

Swali hilo lingejibiwa katika mkutano wa mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, ambao ungefanywa mapema mwaka wa 1917. Wote waliohudhuria walipiga kura na kukubaliana. Hata hivyo, miezi iliyofuata ilionyesha wazi kwamba umoja huo ulikuwa wa muda mfupi, na ndugu wangekabili majaribu makali.