Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kufanya Kazi Pamoja na Mungu—Kunaleta Furaha

Kufanya Kazi Pamoja na Mungu—Kunaleta Furaha

‘Huku tukifanya kazi pamoja naye, tunawasihi [tunawaomba] ninyi pia musipokee fazili zisizostahiliwa za Mungu kisha mukose kusudi lake.’2 WAKORINTHO 6:1.

NYIMBO: 75, 74

1. Yehova ni Mukubwa Zaidi, lakini amewaomba wengine wafanye nini?

YEHOVA ni Mukubwa Zaidi. Aliumba vitu vyote, iko na hekima nyingi sana na nguvu zake hazina mwisho. Kisha kumusaidia Ayubu aelewe jambo hilo, Ayubu alimuambia Yehova hivi: ‘[Sasa ninajua] kwamba unaweza kufanya mambo yote wala hakuna wazo lolote ambalo hauwezi kulifikia.’ (Ayubu 42:2) Yehova hana lazima ya musaada wa mutu fulani ili afanye mambo yote yenye amepanga kufanya. Lakini anaonyesha upendo kwa kuomba wengine wafanye kazi pamoja naye ili kutimiza mapenzi yake.

2. Yehova alimuomba Yesu afanye kazi gani ya maana?

2 Mungu alimuumba Yesu, Mwana wake, mbele ya kuumba viumbe vingine vyote. Kisha, Yehova alimuomba Mwana wake amusaidie kuumba vitu vingine vyote. (Yohana 1:1-3, 18) Mutume Paulo aliandika hivi juu ya Yesu: ‘Kwa njia yake vitu vingine vyote viliumbwa mbinguni na duniani, vitu vinavyoonekana na vitu visivyoonekana, hata vikuwe ni viti vya ufalme ao utawala ao serikali ao mamlaka. Vitu vingine vyote vimeumbwa kupitia yeye na kwa ajili yake.’ (Wakolosai 1:15-17) Yehova alimupatia Mwana wake kazi ya maana, na alijulisha pia wengine juu ya kazi hiyo. Hilo ni pendeleo kubwa!

3. Yehova alimuomba Adamu afanye nini, na sababu gani?

3 Yehova aliomba pia wanadamu wafanye kazi pamoja naye. Kwa mufano, alimupatia Adamu kazi ya kupatia wanyama majina. (Mwanzo 2:19, 20) Fikiria furaha yenye Adamu alikuwa nayo wakati alikuwa anafanya kazi hiyo! Alijifunza kwa uangalifu tabia na namna kila munyama aliumbwa, na kisha alipatia kila munyama jina lenye kufaa. Yehova alikuwa ameumba wanyama wote, kwa hiyo, yeye mwenyewe angewapatia majina. Lakini, alionyesha kwamba anamupenda sana Adamu kwa kumupatia kazi hiyo. Mungu alimupatia pia Adamu kazi ya kufanya dunia yote ikuwe paradiso. (Mwanzo 1:27, 28) Lakini, mwishowe Adamu aliamua kuacha kufanya kazi pamoja na Mungu; hilo lilimuletea yeye na wazao wake wote mateso.—Mwanzo 3:17-19, 23.

4. Namna gani watu fulani walifanya kazi pamoja na Mungu ili kutimiza mapenzi yake?

4 Kisha, Mungu aliomba watu wengine wafanye kazi pamoja naye. Noa alijenga safina yenye ilimusaidia yeye na familia yake waokoke Garika. Musa alikomboa taifa la Israeli kutoka Misri. Yoshua aliingiza Waisraeli katika Inchi ya Ahadi. Sulemani alijenga hekalu huko Yerusalemu. Maria alimuzaa Yesu. Watu hao wote waaminifu na wengine wengi walifanya kazi pamoja na Yehova ili kutimiza mapenzi yake.

5. Ni kazi gani yenye tunaweza kufanya, na Yehova alikuwa na lazima ya musaada wetu ili kufanya kazi hiyo? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

5 Leo, Yehova anatuomba tufanye yetu yote ili kutegemeza Ufalme wake. Kuko njia mbalimbali za kumutumikia Mungu. Sisi wote hatuwezi kumutumikia Yehova kwa njia moja; lakini sisi wote tunaweza kuhubiri habari njema ya Ufalme. Yehova angefanya kazi hiyo yeye mwenyewe. Angezungumuza na watu wenye kuwa duniani moja kwa moja kutoka mbinguni. Yesu alisema kwamba Yehova angeweza hata kufanya majiwe iseme na watu juu ya Mufalme wa Ufalme Wake. (Luka 19:37-40) Lakini Yehova anatuomba tukuwe “wafanyakazi wenzi” wake. (1 Wakorintho 3:9) Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Tukifanya kazi pamoja naye, tunawasihi ninyi pia musipokee fazili zisizostahiliwa za Mungu kisha mukose kusudi lake.’ (2 Wakorintho 6:1) Ni pendeleo kubwa kufanya kazi pamoja na Mungu. Tuzungumuzie basi sababu gani kufanya kazi pamoja na Mungu kunatuletea furaha kubwa.

KUFANYA KAZI PAMOJA NA MUNGU KUNATULETEA FURAHA

6. Mwana-muzaliwa wa kwanza wa Mungu anasema nini juu ya namna alijisikia wakati alikuwa anafanya kazi pamoja na Baba yake?

6 Kufanya kazi pamoja na Mungu kumeletea watumishi wake furaha sikuzote. Mbele ya kuja katika dunia, Mwana-muzaliwa wa kwanza wa Mungu alisema hivi: ‘Yehova alinitokeza nikiwa mwanzo wa njia yake . . . Nilikuwa kando yake nikiwa stadi [fundi] wa kazi. Na mimi nilikuwa yule ambaye yeye alimupenda sana kwa njia ya pekee siku baada ya siku; na mimi nilikuwa nikifurahi mbele zake wakati wote.’ (Methali 8:22, 30) Wakati Yesu alifanya kazi pamoja na Baba yake, alikuwa na furaha kwa sababu alitimiza mambo mengi na alijua kwamba Yehova alimupenda. Tunajisikia hivyo pia?

Hakuna jambo lenye linaweza kutuletea furaha zaidi kuliko kufundisha mutu kweli! (Picha hii inapatana na fungu la 7)

7. Sababu gani kazi ya kuhubiri inatuletea furaha?

7 Yesu alisema kwamba tunakuwa na furaha wakati tunatoa na wakati tunapokea. (Matendo 20:35) Tulifurahi wakati tulipata kweli, lakini, sababu gani kuhubiria watu kweli hiyo kunatuletea pia furaha? Kwa sababu tunawaona wanafurahi sana wakati wanaelewa mafundisho ya Biblia, na wanaanza kuwa na urafiki pamoja na Mungu. Tunafurahi kuona namna wanabadilisha mawazo na maisha yao. Kazi ya kuhubiri ndiyo kazi ya maana zaidi na yenye kuleta furaha zaidi. Inasaidia wale wenye wamekuwa marafiki wa Mungu wapate uzima wa milele.—2 Wakorintho 5:20.

8. Watu fulani wamesema nini juu ya furaha yenye wanapata kwa kufanya kazi pamoja na Yehova?

8 Wakati tunasaidia wengine wamujue Mungu, tunajua kwamba tunamupendeza Yehova na kwamba anafurahia bidii yenye tunafanya ili kumutumikia. Jambo hilo linatuletea furaha pia. (Soma 1 Wakorintho 15:58.) Marco, mwenye kuishi Italia, anasema hivi: “Niko na furaha kubwa sana kwa sababu ninajua kwamba ninafanya yangu yote ili kumutumikia Yehova, lakini situmikie mutu fulani mwenye anaweza kusahau haraka kazi yote yenye nilimufanyia.” Vilevile, ndugu Franco, mwenye kutumikia Italia, anasema hivi: “Kupitia Neno lake na mambo mengine yenye Yehova anatutolea, anatukumbusha kila siku kwamba anatupenda na kwamba mambo yote yenye tunafanya katika kazi yake ni ya maana sana, hata kama tunaweza kuona kuwa bidii yetu haina maana yoyote. Ndiyo sababu kufanya kazi pamoja na Mungu kunaniletea furaha na kunafanya maisha yangu ikuwe yenye maana.”

KUMUTUMIKIA MUNGU KUNATUSAIDIA TUMUKARIBIE NA TUKARIBIE WENGINE

9. Yehova na Yesu walikuwa na urafiki wa namna gani, na sababu gani?

9 Wakati tunafanya kazi pamoja na wale wenye tunapenda, tunakuwa karibu nao. Tunafikia kuwajua muzuri zaidi na sifa zao. Tunajua miradi yao na namna wanajikaza kuifikia. Yesu alifanya kazi pamoja na Yehova kwa miaka mingi sana. Kwa hiyo, upendo wao ukakuwa wenye nguvu sana, na hakuna kitu chenye kingeweza kuharibu urafiki wao. Yesu alionyesha kwamba urafiki wao ulikuwa wa sana wakati alisema hivi: “Mimi na Baba ni kitu kimoja.” (Yohana 10:30) Walikuwa na umoja wa kweli kabisa, na waliungana mukono kabisa wakati walifanya kazi pamoja.

Kazi ya kuhubiri inatia nguvu imani yetu kwa sababu inatukumbusha ahadi za Mungu na kanuni zake zenye upendo

10. Sababu gani kazi ya kuhubiri inatusaidia tumukaribie Mungu na tukaribie ndugu na dada zetu?

10 Yesu alimuomba Yehova awalinde wanafunzi wake. Sababu gani? Alisali hivi: ‘Ili wakuwe kitu kimoja kama vile sisi tulivyo.’ (Yohana 17:11) Wakati tunatumikisha kanuni za Mungu na kufanya kazi ya kuhubiri, tunajua muzuri zaidi sifa zake zenye kupendeza sana. Tunaelewa sababu gani ni jambo la hekima kumutegemea na kufuata muongozo wake. Na wakati tunamukaribia Mungu, yeye pia anatukaribia. (Soma Yakobo 4:8.) Tunakaribia pia ndugu na dada zetu kwa sababu tunapata magumu ileile na furaha ileile, na kwa sababu tuko na miradi moja. Tunafanya kazi pamoja, tunafurahi pamoja, na tunavumilia pamoja. Dada Octavia, mwenye kuishi Angleterre, anasema hivi: “Kufanya kazi pamoja na Yehova kunanisaidia nikaribie wengine.” Anaeleza kwamba ni kwa sababu sasa yeye na marafiki wake wako na miradi ileile na wanatumia maisha yao ili kumutumikia Yehova. Kwa kweli, sisi pia tunajisikia hivyo. Wakati tunaona namna ndugu na dada zetu wanajikaza kumupendeza Yehova, hilo linatuchochea tuwakaribie.

11. Katika dunia mupya, sababu gani tutamukaribia Yehova na ndugu na dada zetu zaidi?

11 Leo, tunapenda Mungu na ndugu na dada zetu; lakini upendo huo utakuwa nguvu zaidi katika dunia mupya. Fikiria kazi zote zenye kufurahisha zenye tutafanya wakati unaokuja! Tutakaribisha wale wenye watafufuliwa na kuwafundisha juu ya Yehova. Tutakuwa pia na kazi ya kufanya dunia ikuwe paradiso. Tutafurahi kabisa kufanya kazi pamoja na kufikia ukamilifu hatua kwa hatua katika utawala wa Kristo. Wanadamu wote watakaribiana na kumukaribia zaidi Yehova, kwa sababu atatimiza kabisa tamaa ya kila kitu chenye kuwa na uzima.—Zaburi 145:16.

KUFANYA KAZI PAMOJA NA MUNGU KUNATULINDA

12 Tunapenda kulinda urafiki wetu pamoja na Yehova. Tunaishi katika ulimwengu wa Shetani na hatukamilike; kwa hiyo, inaweza kuwa mwepesi kwetu kuanza kufikiri na kutenda kama watu wa ulimwengu huu. Ni kama vile tunaogelea katika mutoni wenye kutuongoza ngambo yenye hatupendi kuenda. Tunapaswa kutumia nguvu zetu zote ili tuogelee na kuenda ngambo yenye tunapenda. Vilevile, tunapaswa kujikaza sana ili tuepuke kuchochewa na ulimwengu wa Shetani. Kwa hiyo, namna gani kazi ya kuhubiri inatulinda? Wakati tunazungumuza na wengine juu ya Yehova na Biblia, tunakazia akili yetu juu ya mambo ya maana na mema, hatukazie akili yetu juu ya mambo yenye inaweza kuregeza imani yetu. (Wafilipi 4:8) Kazi ya kuhubiri inatia nguvu imani yetu kwa sababu inatukumbusha ahadi za Mungu na kanuni zake zenye upendo. Inatusaidia pia tuendelee kuwa na sifa zenye tuko nazo lazima ili tujilinde na Shetani na ulimwengu wake.—Soma Waefeso 6:14-17.

Wakati tunaendelea kuhubiri, kujifunza, na kutumikia wengine katika kutaniko kwa bidii, tunajilinda kwa sababu hatuna wakati wa kuhangaikia sana magumu yetu wenyewe

13. Shahidi moja mwenye kuishi Australia anajisikia namna gani juu ya kazi ya kuhubiri?

13 Wakati tunaendelea kuhubiri, kujifunza, na kutumikia wengine katika kutaniko kwa bidii, tunajilinda kwa sababu hatuna wakati wa kuhangaikia sana magumu yetu wenyewe. Joel, mwenye kuishi Australia, anasema hivi: “Kazi ya kuhubiri inanisaidia nielewe muzuri hali ya maisha. Inanikumbusha magumu yenye watu wanapambana nayo na faida zenye nimepata kwa kutumikisha kanuni za Biblia katika maisha yangu. Kazi ya kuhubiri inanisaidia niendelee kujikaza kuwa munyenyekevu; inanipatia nafasi ya kumutegemea Yehova na ndugu na dada zangu.”

14. Kuhubiri kwa bidii kunaonyesha namna gani kwamba tuko na roho ya Mungu?

14 Kazi ya kuhubiri inatuhakikishia kabisa kwamba tuko na roho ya Mungu. Kwa mufano: Fikiria kwamba kazi yako ni kupatia watu wa eneo lako mukate. Haulipiwe mushahara, lakini unapaswa kujilipia garama zako wewe mwenyewe. Pia, watu wengi hawapendi mukate huo, na wengine wamekuchukia kwa sababu unawaletea mukate huo. Utaendelea kufanya kazi hiyo? Unaweza kuvunjika moyo haraka, na pengine unaweza kuacha kufanya kazi hiyo. Lakini, kila mwaka wengi kati yetu tunaendelea kufanya kazi ya kuhubiri, hata kama kazi hiyo inatuomba tutumie wakati na feza zetu, na hata kama watu wanatucheka ao kutukasirikia. Hilo linaonyesha kwamba roho ya Mungu inaendelea kutusaidia.

KUFANYA KAZI PAMOJA NA MUNGU KUNAONYESHA KWAMBA TUNAMUPENDA YEYE NA WENGINE

15. Namna gani kazi ya kuhubiri habari njema inapatana na kusudi la Mungu kwa wanadamu?

15 Kazi ya kuhubiri inapatana namna gani na kusudi la Yehova kwa wanadamu? Kusudi la Mungu lilikuwa kwamba wanadamu waishi milele, na kusudi hilo halikubadilika wakati Adamu alifanya zambi. (Isaya 55:11) Mungu alifanya mupango ili kutukomboa kutoka katika utumwa wa zambi na kifo. Namna gani? Yesu alikuja katika dunia ili kutoa uzima wake. Lakini, wanadamu wanapaswa kumutii Mungu ili zabihu hiyo iwaletee faida. Kwa hiyo, Yesu alifundisha watu wajue mambo yenye Mungu anapenda wafanye, na aliamuru wanafunzi wake wafanye kazi hiyo. Leo, wakati tunahubiri na kusaidia wengine wakuwe marafiki wa Mungu, tunatumika moja kwa moja na Mungu katika mupango wake wenye upendo wa kuokoa wanadamu kutoka katika zambi na kifo.

16. Kazi yetu ya kuhubiri inapatana namna gani na amri kubwa za Mungu?

16 Wakati tunasaidia wengine waanze kutembea katika njia ya uzima wa milele, tunaonyesha kwamba tunawapenda na kwamba tunamupenda Yehova. “Mapenzi yake ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:4) Wakati Mufarisayo moja alimuuliza Yesu amri kubwa ya Mungu ni gani, Yesu alisema hivi: “‘Lazima umupende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri iliyo kubwa na ya kwanza. Ya pili, kama hiyo, ni hii: ‘Umupende jirani yako kama wewe mwenyewe.’” (Mathayo 22:37-39) Tunatii amri hizo wakati tunahubiri habari njema.—Soma Matendo 10:42.

17. Unaona namna gani pendeleo la kuhubiri habari njema?

17 Tumebarikiwa sana! Yehova ametupatia kazi yenye kutuletea furaha, yenye kutusaidia tumukaribie yeye na ndugu na dada zetu, na yenye kutusaidia tulinde urafiki wetu pamoja naye. Inatupatia pia nafasi ya kuonyesha upendo wetu kwa Mungu na kwa wengine. Yehova ana mamilioni ya watumishi katika dunia yote, na watumishi hao wote wanapambana na hali mbalimbali. Lakini, iwe sisi ni vijana ao wazee, tajiri ao maskini, wenye kuwa na nguvu ao wazaifu, tunafanya yote tunaweza ili kutangazia wengine mambo yenye tunaamini. Tunajisikia kama vile Chantel wa Ufaransa, mwenye alisema hivi: “Mutu mwenye nguvu zaidi sana katika ulimwengu wote, Muumbaji wa vitu vyote, Mungu mwenye furaha, ananiambia: ‘Uende! Useme! Useme juu yangu, useme kwa moyo wote. Ninakupatia nguvu zangu, Neno langu Biblia, musaada wa malaika, wafanyakazi wenzako katika dunia, mazoezi yenye kuendelea, na maagizo mazuri kwa wakati wenye kufaa.’ Ni pendeleo kubwa sana kufanya mambo yenye Yehova anatuomba na kufanya kazi pamoja na Mungu wetu!”