Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Sababu Gani Tunapaswa ‘Kuendelea Kukesha’?

Sababu Gani Tunapaswa ‘Kuendelea Kukesha’?

‘Hamujue ni siku gani Bwana yenu atakuja.’MATHAYO 24:42.

NYIMBO: 136, 129

1. Toa mufano wenye kuonyesha sababu gani tunapaswa kuwa waangalifu juu ya wakati na mambo yenye kufanyika nafasi kwenye tunapatikana. (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

MUKUSANYIKO unakaribia kuanza. Musimamizi anapanda kwenye jukwaa na anakaribisha watu wote. Muziki unakaribia kuanza. Wasikilizaji wanajua kama ni wakati wa kukaa kwenye nafasi zao. Wanapenda kusikiliza muziki muzuri, na wanangojea kwa hamu kusikiliza hotuba mbalimbali zenye zitatolewa. Lakini pengine kuko watu fulani wenye hawafuate musimamizi kwa uangalifu ao hawatambue kama muziki umekwisha kuanza. Kwa hiyo, hawatambue kama mukusanyiko umeanza na wanaendelea kutembea-tembea ao kuzungumuza na marafiki wao. Hali hiyo inaonyesha jambo lenye linaweza kutokea ikiwa hatuko waangalifu juu ya wakati ao mambo yenye kufanyika nafasi kwenye tunapatikana. Hali hiyo inatufundisha jambo la maana sana kwa sababu hivi karibuni tukio kubwa sana litaanza, na tunapaswa kujitayarisha kwa ajili ya tukio hilo. Ni tukio gani?

2. Sababu gani Yesu aliambia wanafunzi wake ‘waendelee kukesha’?

2 Yesu Kristo alionya wanafunzi wake kama ni lazima kuendelea kukesha na kuwa tayari kwa ajili ya ‘umalizio wa mufumo wa mambo.’ Aliwaambia hivi: ‘Muendelee kukesha, kwa maana hamujue wakati uliowekwa ni gani.’ Kisha hapo, aliwaambia mara nyingi hivi: ‘Muendelee kukesha.’ (Mathayo 24:3; soma Marko 13:32-37.) Habari yenye Mathayo aliandika inaonyesha pia kama Yesu aliwaonya wanafunzi wake juu ya jambo hilo. Aliwaambia hivi: ‘Kwa hiyo, muendelee kukesha kwa sababu hamujue ni siku gani Bwana yenu atakuja.’ Na tena aliwaonya hivi: ‘Mukuwe tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa musiyofikiria.’ Kisha alisema tena hivi: ‘Muendelee kukesha kwa sababu hamuijue ile siku wala saa.’—Mathayo 24:42-44; 25:13.

3. Sababu gani tunapaswa kufuata kwa uangalifu onyo la Yesu?

3 Mashahidi wa Yehova wanafuata kwa uangalifu onyo lenye Yesu alitoa. Tunajua kama tunaishi katika “wakati wa mwisho” na kama ‘ziki [taabu] kubwa’ itaanza hivi karibuni! (Danieli 12:4; Mathayo 24:21) Kama vile Yesu alitabiri, watumishi wa Yehova wanaendelea kuhubiri habari njema ya Ufalme katika dunia yote. Wakati huohuo, tunaona vita, magonjwa, matetemeko ya inchi, na njaa katika maeneo mengi. Kuko muvurugo zaidi katika dini nyingi, kuvunja sheria na jeuri vinaongezeka zaidi kuliko zamani. (Mathayo 24:7, 11, 12, 14; Luka 21:11) Tunangojea sasa kwa hamu wakati Yesu atakuja ili kutimiza kusudi la Baba yake.—Marko 13:26, 27.

SIKU HIYO INAKARIBIA SANA!

4. (a) Sababu gani tunaweza kuamini kama Yesu anajua sasa wakati vita ya Har-Magedoni itaanza? (b) Hata kama hatujue wakati ziki kubwa itaanza, tunaweza kuwa hakika na jambo gani?

4 Wakati tunaenda kwenye mukusanyiko fulani, tunajua ni wakati gani kila sehemu itaanza. Lakini, hatuwezi kujua hata kidogo siku gani ziki kubwa itaanza. Wakati Yesu alikuwa duniani, alisema hivi: ‘Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mutu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.’ (Mathayo 24:36) Kwa kweli, kwa sababu Yesu ndiye ataongoza vita ya Har-Magedoni, inawezekana kabisa anajua sasa ni wakati gani vita hiyo itaanza. (Ufunuo 19:11-16) Lakini, sisi hatujue tarehe ao wakati mwisho utakuja. Ndiyo sababu ni jambo la maana sana tuendelee kukesha. Yehova amepanga kabisa wakati wenye ziki kubwa itaanza, na kila siku yenye kupita ziki hiyo inaendelea kukaribia zaidi na zaidi. ‘Haitachelewa!’ (Soma Habakuki 2:1-3.) Sababu gani tunaweza kuwa hakika kabisa na jambo hilo?

Yehova amepanga kabisa wakati wenye ziki kubwa itaanza

5. Toa mufano wenye kuonyesha kama sikuzote Yehova anatimiza unabii wake kwa wakati wake.

5 Sikuzote Yehova anatimiza unabii wake kwa wakati wake! Kwa mufano, fikiria siku yenye alikomboa watu wake kutoka Misri. Ilikuwa tarehe 14 Mwezi wa Nisani katika mwaka wa 1513 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. Kisha Musa aliandika hivi juu ya siku hiyo: ‘Na ikakuwa kwamba mwishoni mwa ile miaka 430, naam [ndiyo], ikakuwa kwamba siku hiyohiyo majeshi yote ya Yehova yakatoka katika inchi ya Misri.’ (Kutoka 12:40-42) Tarehe 14 Mwezi wa Nisani katika mwaka wa 1943 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, kisha kupita tu miaka 430 mbele Waisraeli wakombolewe, ahadi ya Yehova ya kubariki uzao wa Abrahamu ilianza kutimia. (Wagalatia 3:17, 18) Kisha wakati fulani, Yehova alimuambia Abrahamu hivi: ‘Ujue hakika kwamba uzao wako utakuwa mukaaji mugeni katika nchi isiyokuwa yao, nao watawatumikia watu wale, nao watawatesa kwa miaka mia ine.’ (Mwanzo 15:13; Matendo 7:6) Miaka 400 ilianza kuhesabiwa katika mwaka wa 1913 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, wakati Ishmaeli alianza kumutendea Isaka mubaya. Miaka hiyo iliisha wakati Yehova aliwakomboa Waisraeli kutoka Misri. (Mwanzo 21:8-10; Wagalatia 4:22-29) Ndiyo, mamia ya miaka mbele ya tukio hilo, Yehova aliweka kabisa siku yenye angewakomboa watu wake!

6. Sababu tunaweza kuwa hakika kama Yehova ataokoa watu wake?

6 Yoshua alikuwa kati ya Waisraeli wenye walikombolewa kutoka Misri. Kisha miaka mingi, alikumbusha Waisraeli hivi: ‘Nanyi munajua vema kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.’ (Yoshua 23:2, 14) Yehova ameahidi kama ataokoa watumishi wake wakati wa ziki kubwa na kuwapatia uzima wa milele katika dunia mupya. Na tunaweza kuwa hakika kama atatimiza kabisa ahadi hiyo. Kwa hiyo, ikiwa tunapenda kuishi katika dunia mupya, tunapaswa kuendelea kukesha.

ENDELEA KUKESHA ILI UOKOKE

7, 8. (a) Zamani mulinzi alikuwa na kazi gani, na hilo linatufundisha nini? (b) Ikiwa walinzi wanalala usingizi kwenye kazi, hilo linaweza kuwa na matokeo gani? Toa mufano.

7 Mufano wa walinzi wenye walikuwa wanalinda miji zamani unaweza kutufundisha jambo fulani. Miji mingi kati ya miji hiyo, kama vile Yerusalemu, ilizungukwa na kuta ndefu ili kuzuia maadui kuingia ndani ya muji. Walinzi walisimama juu ya kuta hizo, na kufanya hivyo kungewasaidia waone maeneo yote yenye kuzunguka muji huo. Walinzi wengine walisimama kwenye milango ya muji. Wanaume hao walipaswa kuendelea kukesha usiku na muchana, na ikiwa waliona maadui wanakuja, walipaswa kuonya watu wenye kuwa ndani ya muji. (Isaya 62:6) Walijua kama lilikuwa jambo la maana sana kuendelea kukesha na kuchunguza kwa uangalifu mambo yenye yalikuwa yanafanyika. Ikiwa hawangekesha, watu wengi wangekufa.—Ezekieli 33:6.

8 Yosefu, mwanahistoria mwenye aliandika habari juu ya Wayahudi, alieleza namna Waroma waliweza kuingia katika Yerusalemu mwaka wa 70 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Walinzi wenye walikuwa wanachunga sehemu fulani ya muji huo walilala usingizi. Kwa hiyo, askari Waroma waliingia katika muji. Walienda kwenye hekalu, wakaliunguza, na kuharibu sehemu zingine zote za muji wa Yerusalemu. Hiyo ilikuwa sehemu ya mwisho ya ziki kubwa sana yenye haijafikiaka taifa la Wayahudi.

9. Leo, watu wengi hawatambue jambo gani?

9 Leo, serikali nyingi zinachunga mipaka ya inchi zao kwa kutumia askari na njia za ulinzi zenye kutumia teknolojia ya sasa kabisa. Serikali hizo zinakesha ili kuona kila mutu ao kila kitu chenye kinaweza kuvuruga usalama wa inchi yao. Lakini, hazitambue kama kuko serikali ya mbinguni yenye kuongozwa na Yesu Kristo yenye kuwa na nguvu zaidi. Hivi karibuni, serikali hiyo itapigana vita na serikali zote zenye kuwa katika dunia. (Isaya 9:6, 7; 56:10; Danieli 2:44) Tunangojea kwa hamu siku hiyo ikuje na tunapenda kuwa tayari kwa ajili ya siku hiyo. Kwa hiyo, tunafuata kwa uangalifu unabii wa Biblia na tunaendelea kumutumikia Yehova kwa uaminifu.—Zaburi 130:6.

USIKENGEUSHWE

10, 11. (a) Tunapaswa kuwa waangalifu juu ya jambo gani, na sababu gani? (b) Ni nini inakusadikisha kama Shetani amechochea watu wazarau unabii wa Biblia?

10 Fikiria mulinzi fulani mwenye amekesha usiku muzima. Wakati usiku unakaribia kucha, ni vigumu aendelee kukesha kwa sababu ni mwenye kuchoka sana. Vilevile, tunaishi katika siku za mwisho za ulimwengu huu. Na kwa sababu tunaendelea kukaribia mwisho, itakuwa vigumu sana kwetu kuendelea kukesha. Litakuwa jambo lenye kuhuzunisha sana ikiwa hatuendelee kukesha! Tuzungumuzie basi mambo tatu yenye yanaweza kutuzuia tuendelee kukesha.

11 Shetani anadanganya watu. Yeye ndiye ‘mutawala wa ulimwengu huu.’ Muda mufupi tu mbele ya kifo chake, Yesu alikumbusha wanafunzi wake mara tatu juu ya jambo hilo. (Yohana 12:31; 14:30; 16:11) Shetani ametumia dini za uongo ili kudanganya watu. Ndiyo sababu leo watu wengi wanazarau unabii wa Biblia wenye kuonyesha wazi kama mwisho wa ulimwengu huu unakaribia sana. (Sefania 1:14) Kwa kweli, Shetani “amezipofusha akili za wasioamini.” (2 Wakorintho 4:3-6) Kwa hiyo, wakati tunajikaza kuambia watu kama mwisho wa ulimwengu unakaribia sana na kama Kristo anatawala, wengi wao hawapendi kutusikiliza. Mara nyingi wanasema, “Sipendezwe.”

12. Sababu gani hatupaswe kumuacha Shetani atudanganye?

12 Watu wengi hawapendezwe na unabii wa Biblia; lakini, hatupaswe kuacha jambo hilo lituvunje moyo. Tunajua sababu gani tunapaswa kuendelea kukesha. Mutume Paulo aliwaambia ndugu zake hivi: ‘Ninyi wenyewe munajua vema kabisa kwamba siku ya Yehova inakuja.’ Aliongezea hivi: “Sawasawa kabisa kama mwizi usiku.” (Soma 1 Wathesalonike 5:1-6.) Yesu alituonya hivi: ‘Muendelee kuwa tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa musiyoitazamia.’ (Luka 12:39, 40) Hivi karibuni, Shetani atadanganya watu kwa kuwachochea wafikiri kama kuko “amani na usalama” katika dunia. Kisha, siku ya Yehova itakuja mara moja, na watashituka. Halafu sisi? Ikiwa tunapenda kuwa tayari kwa ajili ya siku hiyo na hatupendi kudanganywa kama watu wengine, tunapaswa ‘kukaa macho na kutunza akili zetu.’ Ndiyo sababu tunapaswa kusoma Neno la Mungu kila siku na kufikiri sana juu ya mambo yenye Yehova anatuambia.

13. Namna gani roho ya ulimwengu inachochea watu, na namna gani tunaweza kuepuka hatari hiyo?

13 Roho ya ulimwengu inachochea mawazo ya watu. Leo, watu wengi wanawaza kama hawana lazima ya kumujua Mungu. (Mathayo 5:3) Kwa hiyo, wanatumia nguvu na wakati mwingi ili kutafuta vitu vingi vya kimwili vyenye ulimwengu huu unatoa. (1 Yohana 2:16) Pia, kuliko zamani, leo kuko mambo mengi mbalimbali ya kujifurahisha yenye yanapendeza watu na kuwachochea wapende kujifurahisha sana na watimize kila tamaa yenye wako nayo. (2 Timotheo 3:4) Mambo hayo yanakengeusha watu kufanya mambo ya maana zaidi, na hawafikirie urafiki wao pamoja na Mungu. Ndiyo sababu Paulo aliwakumbusha Wakristo kama walipaswa ‘kuamuka kutoka katika usingizi’ kwa kuepuka kutumia maisha yao tu ili kutimiza tamaa zao.—Waroma 13:11-14.

Tunapenda roho ya Mungu ichochee mawazo yetu, hapana roho ya ulimwengu

14. Andiko la Luka 21:34, 35 linatutolea onyo gani?

14 Tunapenda roho ya Mungu ichochee mawazo yetu, hapana roho ya ulimwengu. Yehova anatumia roho takatifu yake ili kutusaidia tuelewe muzuri mambo yenye yatatokea hivi karibuni. (1 Wakorintho 2:12) [1] (Soma maelezo kwenye mwisho wa habari hii.) Lakini tunapaswa kuwa waangalifu. Hata mambo ya kawaida yenye tunafanya katika maisha yanaweza kutukengeusha kumutumikia Yehova. (Soma Luka 21:34, 35.) Watu wengine wanaweza kusema kama tuko wapumbavu kwa sababu tunaamini kama tunaishi katika siku za mwisho za ulimwengu huu. (2 Petro 3:3-7) Lakini hatupaswe kuwaacha watuvunje moyo. Tuko na ushuhuda wenye kuonyesha wazi kama mwisho utakuja hivi karibuni. Ikiwa tunapenda roho ya Mungu ituchochee, tunapaswa kuhuzuria mikutano kwa ukawaida pamoja na ndugu na dada.

Unafanya nguvu zako zote ili ‘uendelee kukesha’? (Picha hii inapatana na fungu la 11-16)

15. Ni jambo gani lilipata Petro, Yakobo, na Yohana, na namna gani jambo hilo linaweza kutupata sisi pia?

15 Uzaifu wetu unafanya ikuwe vigumu tuendelee kukesha. Yesu alielewa kama wanadamu hawakamilike na wako na uzaifu. Fikiria jambo lenye lilitokea usiku wenye ulitangulia kifo chake. Yesu alikuwa mukamilifu, lakini alijua kama ili aendelee kuwa muaminifu, alipaswa kumuomba Baba yake amusaidie. Yesu aliambia mutume Petro, Yakobo, na Yohana waendelee kukesha wakati yeye alikuwa anasali. Lakini mitume hawakuelewa kama lilikuwa jambo la maana sana waendelee kukesha. Walikuwa wenye kuchoka, na walilala usingizi. Yesu pia alikuwa mwenye kuchoka, lakini aliendelea kukesha na kusali kwa Baba yake. Mitume pia walipaswa kusali wakati huo.—Marko 14:32-41.

16. Kulingana na Luka 21:36, namna gani Yesu alitushauria ‘kuendelea kukesha’?

16 Ni nini itatusaidia ‘tuendelee kukesha’ na kuwa tayari kwa ajili ya siku ya Yehova? Tunapaswa kuwa na tamaa kubwa ya kuendelea kufanya mambo yenye kuwa sawa. Lakini kuko mambo mengine ya kufanya. Siku kidogo mbele ya kifo chake, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kama walipaswa kuendelee kumuomba Yehova awasaidie. (Soma Luka 21:36.) Ili tuendelee kukesha katika wakati huu wa mwisho, sisi pia tunapaswa kusali kwa Yehova kila wakati.—1 Petro 4:7.

ENDELEA KUKESHA

17. Namna gani tunaweza kuhakikisha kama tuko tayari kwa ajili ya mambo yenye yatatokea hivi karibuni?

17 Yesu alisema kama mwisho utakuja ‘katika saa musiyofikiria.’ (Mathayo 24:44) Kwa hiyo, tunapaswa kuwa tayari kila wakati. Huu si wakati wa kutafuta maisha yenye ulimwengu wa Shetani unaonyesha kuwa yataleta furaha. Hiyo ni ndoto tu. Lakini, kupitia Biblia, Yehova na Yesu wametuambia namna tunaweza kuendelea kukesha. Kwa hiyo, tukaze basi uangalifu wetu juu ya unabii mbalimbali wa Biblia na namna unaendelea kutimia. Na tuendelee kumukaribia Yehova zaidi na kutia Ufalme wake pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu. Ikiwa tunafanya hivyo, tutakuwa tayari wakati mwisho utakuja. (Ufunuo 22:20) Tutaokolewa ikiwa tunafanya hivyo!

^ [1] (fungu la 14) Soma sura ya 21 katika kitabu Ufalme wa Mungu Unatawala!