Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Vijana, Mutie Nguvu Imani Yenu

Vijana, Mutie Nguvu Imani Yenu

‘Imani ni . . . usibitisho [uhakikisho] ulio wazi wa mambo halisi [ya kweli-kweli] ingawa hayaonekane.’—WAEBRANIA 11:1.

NYIMBO: 41, 69

1, 2. Wakati fulani, vijana wenye kumutumikia Yehova wanaweza kujiuliza nini, na Biblia inatoa shauri gani?

 DADA mumoja katika inchi ya Uingereza aliambiwa na mwanafunzi mwenzake hivi: “Mutu mwenye akili sana kama wewe hawezi kuamini Mungu.” Ndugu mumoja katika inchi ya Ujerumani aliandika hivi: “Walimu wangu waliona habari za uumbaji zenye kuzungumuziwa katika Biblia kuwa ni hadisi za kuwazia tu. Na wanaona kuwa ni jambo la kawaida wanafunzi waamini fundisho la mageuzi.” Dada mumoja katika inchi ya Ufaransa alisema hivi: “Walimu kwenye masomo yetu wanashangaa kuona kama kuko wanafunzi wenye wangali wanaamini Biblia.”

2 Leo, watu wengi hawaamini kama ni Mungu ndiye alituumba. Ikiwa wewe ni kijana mwenye kumutumikia Yehova ao uko unajifunza juu yake, wakati fulani unaweza kujiuliza namna unaweza kuonyesha kama yeye ndiye Muumbaji wetu. Biblia inatusaidia kuwaza sana juu mambo yenye tunasikia ao tunasoma na kufikiri pamoja na wengine juu ya mambo hayo. Neno la Mungu linasema hivi: “Uwezo wa kufikiri utakutunza.” Namna gani? Uwezo huo utakusaidia kupinga mawazo ya uongo na kutia nguvu imani yako kwa Yehova.—Soma Methali 2:10-12.

3. Tutazungumuzia nini katika habari hii?

3 Ili tukuwe na imani yenye nguvu kwa Yehova, tunapaswa kumujua muzuri. (1 Timotheo 2:4) Kwa hiyo, wakati unasoma Biblia na vichapo vyetu, ni muzuri usimamishe usomaji na kufikiri juu ya mambo yenye unasoma. Ujikaze kuelewa mambo hayo. (Mathayo 13:23) Ikiwa unajifunza kwa njia hiyo, utaona mambo mengi yenye kuhakikisha kama Yehova ndiye Muumbaji wetu na kama Biblia ilitoka kwake. (Waebrania 11:1) Tuone basi namna gani tunaweza kufanya hivyo.

NAMNA UNAWEZA KUTIA NGUVU IMANI YAKO

4. Ni katika njia gani kuamini mageuzi kunafanana na kuamini uumbaji? Sisi wote tunapaswa kufanya nini?

4 Mutu fulani anaweza kukuambia hivi: “Ninaamini mageuzi kwa sababu wanasayansi wamesema kuwa ni kweli. Namna gani unaweza kuamini Mungu ikiwa hakuna mutu amekwisha kumuona?” Watu wengi wanawaza hivyo. Ni kweli, hakuna mutu kati yetu mwenye amekwisha kuona Mungu ao kuona wakati alikuwa anaumba kitu fulani. (Yohana 1:18) Sasa, tuseme nini juu ya watu wenye kuamini mageuzi? Wao pia wanaamini mambo yenye hawawezi kuona. Hakuna mwanasayansi ao mwanadamu mwengine yeyote mwenye ameona aina fulani ya uzima inageuka kuwa aina ingine. Kwa mufano hakuna mutu hata mumoja mwenye amekwisha kuona sokwe (chimpanzé) anageuka kuwa mutu. (Ayubu 38:1, 4) Kwa hiyo, sisi wote tunapaswa kuchunguza ukweli wa mambo, kufikiri kwa uangalifu juu ya mambo hayo, na kuamua kulingana na yale yanaonyesha kabisa. Watu wengi wamechunguza uumbaji na ‘wameelewa’ kama kuna Mungu. ‘Wameona waziwazi’ kama yeye ndiye Muumbaji, ni mwenye nguvu, na ana sifa nyingi za muzuri.—Waroma 1:20.

Vyombo vyetu vyenye kutusaidia kutafuta habari vinaweza kukusaidia ufasirie wengine mambo yenye unaamini (Picha hii inapatana na fungu la 5)

5. Ni vyombo gani vyenye vinaweza kutusaidia tujifunze mengi juu ya uumbaji?

5 Wakati tunaangalia na kufikiri sana juu ya uumbaji, tunaweza kuona kama kila kitu kiliumbwa kwa njia yenye kushangaza. “Kwa imani tunatambua” kama kuna Muumbaji, hata kama hatuwezi kumuona. Tunatambua kama ana sifa za muzuri na hekima kubwa. (Waebrania 11:3, 27) Tunaweza kujifunza mengi juu ya vitu vyenye aliumba wakati tunasoma mambo yenye wanasayansi wamevumbua. Tunaweza kupata habari fulani juu ya mambo hayo katika vyombo vyetu vya kutusaidia kutafuta habari kama vile video Maajabu ya Uumbaji Yanafunua Utukufu wa Mungu, broshua Uhai—Ulitokana na Muumba? na Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai, na kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? Katika gazeti Amuka! mara nyingi kuna sehemu za kuuliza maulizo wanasayansi na watu wengine wenye wanafasiria sababu gani sasa wanaamini Mungu. Na habari zenye kichwa “Kitu Hiki Kilijifanya Chenyewe?” zinatoa maelezo fulani juu ya wanyama na vitu vingine katika uumbaji na pia mifano yenye kuonyesha namna wanasayansi wamejaribu kuiga vitu hivyo.

6. Namna gani vichapo vyetu vinaweza kukusaidia?

6 Juu ya broshua hizo mbili zenye tunataja, ndugu mumoja wa miaka 19 katika inchi ya Amerika alisema hivi: “Broshua hizo zimekuwa za maana sana kwangu. Nimejifunza broshua hizo mara nyingi.” Dada mumoja katika inchi ya Ufaransa aliandika hivi: “Habari zenye kichwa ‘Kitu Hiki Kilijifanya Chenyewe?’ zinanishangaza! Habari hizo zinaonyesha kama mafundi wakubwa sana wanaweza kuiga vitu vya uumbaji, lakini hakuna hata siku moja watafikia kufanya vitu vya ajabu sana kama hivyo.” Wazazi wa mutoto mumoja mwanamuke wa miaka 15 katika Afrika Kusini walisema hivi: “‘Sehemu ya Kuuliza Maulizo’ ndiyo habari ya kwanza yenye mutoto wetu anasoma katika gazeti Amuka!” Vichapo hivyo vinaweza kukusaidia pia uone mambo yenye kuhakikisha kama kuna Muumbaji, na utajua mafundisho ya uongo na kuyapinga. Imani yako itakuwa yenye nguvu sana, na utakuwa kama muti wenye mizizi mirefu na wenye hauwezi kuanguka katika upepo mukali.—Yeremia 17:5-8.

UAMINI MAFUNDISHO YA BIBLIA

7. Sababu gani Mungu anapenda utumie nguvu zako za kufikiri?

7 Ni mubaya kuuliza maulizo kama vile, ‘Sababu gani ninaamini mafundisho ya Biblia?’ Hapana kabisa. Yehova hapendi uamini jambo fulani kwa sababu tu wengine wanaamini jambo hilo. Anapenda utumie ‘nguvu zako za kufikiri’ ili uelewe Biblia na uone mambo yenye kuhakikisha kama ilitoka kwa Mungu. Ikiwa unaendelea kuelewa mambo Biblia inasema, imani yako itakuwa yenye nguvu zaidi. (Soma Waroma 12:1, 2; 1 Timotheo 2:4.) Njia moja ya kukusaidia uelewe Biblia ni kujifunza habari fulani zenye unapenda kuelewa muzuri.

8, 9. (a) Watu fulani wanafurahia kujifunza habari gani? (b) Watu fulani walipata faida gani wakati walifikiri sana juu ya mambo yenye walisoma?

8 Watu fulani wanafurahia kujifunza unabii mbalimbali wa Biblia. Ao wanaweza kupenda kulinganisha habari za Biblia na mambo yenye wanahistoria, wanasayansi, ao wale wenye kuchimbua vitu vya zamani wanasema. Kwa mufano, fikiria andiko la Mwanzo 3:15. Yehova alitoa unabii huo wa maana sana kisha tu Adamu na Eva kumuasi na kukataa njia yake ya kutawala. Unabii huo ni wa kwanza kati ya unabii mbalimbali wa Biblia wenye unatusaidia kuelewa namna Ufalme wa Mungu utaonyesha kama njia ya Mungu ya kutawala ndiyo ya muzuri zaidi, na namna Ufalme huo utamaliza mateso yote. Namna gani unaweza kujifunza andiko la Mwanzo 3:15? Unaweza kufanya liste ya maandiko ya Biblia yenye kutoa maelezo mengi zaidi juu ya namna unabii huo utatimizwa. Kisha, unaweza kutafuta kujua wakati maandiko hayo yaliandikwa na kuyapanga muzuri. Bila kukawia, utatambua kama wale waandikaji wa Biblia hawakuishi wakati mumoja lakini kila muandikaji aliandika jambo fulani lenye linasaidia kuelewa muzuri zaidi unabii huo. Hilo linaweza kukusaidia uone kama waliongozwa na roho takatifu ya Mungu.—2 Petro 1:21.

9 Ndugu mumoja katika inchi ya Ujerumani alifikiria namna kila kitabu cha Biblia kinatoa maelezo juu ya Ufalme wa Mungu. Alisema hivi: “Ni hivyo, hata kama Biblia iliandikwa na wanaume 40 hivi. Na wengi kati yao hawakuishi wakati mumoja na hawakujuana.” Dada mumoja katika inchi ya Australia alikuwa anajifunza habari moja katika Munara wa Mulinzi na alielewa namna sikukuu ya Pasaka inapatana na andiko la Mwanzo 3:15 na Masiya. [1] (Soma maelezo kwenye mwisho wa habari hii.) Aliandika hivi: “Kujifunza habari hiyo kulinisaidia kuona waziwazi kama Yehova ni Mungu wa ajabu sana. Nilishangaa sana kuona kama mupango huo ulifanywa juu ya Waisraeli na ukatimia juu ya Yesu. Nilipaswa kusimama na kufikiri sana juu ya namna unabii huo juu ya chakula cha Pasaka ulikuwa wa kushangaza sana!” Sababu gani dada huyo alishangaa hivyo? Aliwaza sana juu ya mambo yenye alisoma na aliyaelewa. Hilo lilimusaidia kutia nguvu imani yake na kumukaribia Yehova zaidi.—Mathayo 13:23.

10. Waandikaji wa Biblia waliandika bila kuficha kitu chochote, namna gani hilo linafanya tukuwe na imani yenye nguvu katika Biblia?

10 Fikiria pia namna waandikaji wa Biblia waliandika habari bila kuficha kitu chochote. Walisema kweli sikuzote na hawakuogopa kufanya hivyo. Mara nyingi, waandikaji wa wakati huo walikuwa wanaandika tu mambo ya muzuri juu ya taifa lao na viongozi wao. Lakini manabii wa Yehova hawakuandika tu mambo ya muzuri, waliandika pia mambo ya mubaya yenye watu wa Israeli na wafalme wao walifanya. (2 Mambo ya Nyakati 16:9, 10; 24:18-22) Waliandika hata makosa yao na ya watumishi wengine wa Mungu. (2 Samweli 12:1-14; Marko 14:50) Ndugu mumoja kijana katika inchi ya Uingereza alisema hivi: “Watu wenye kufanya hivyo ni wadogo sana. Hilo linatuhakikishia kabisa kama Biblia ilitoka kwa Mungu.”

11. Namna gani muongozo wenye tunapata katika Biblia unafanya tuamini kama Biblia ilitoka kwa Mungu?

11 Wakati watu wanaacha Biblia iongoze maisha yao, wanaona kama inawasaidia kabisa. Hilo linafanya waamini kama Biblia ilitoka kwa Mungu. (Soma Zaburi 19:7-11.) Dada mumoja kijana katika inchi ya Japani aliandika hivi: “Wakati familia yangu ilitumikisha mafundisho ya Biblia, tulikuwa na furaha kabisa. Tulikuwa na amani, umoja, na upendo.” Biblia imesaidia watu wengi waone kama mambo fulani yenye walikuwa wanaamini ni ya uongo. (Zaburi 115:3-8) Inasaidia watu wamutegemee Yehova, Mungu mweza-yote, na inaahidi maisha ya muzuri wakati unaokuja. Lakini, watu fulani wenye kusema kama hakuna Mungu wanafanya kabisa uumbaji kuwa mungu wao. Wengine wanasema kama wanadamu wanaweza kufanya watu wakuwe na maisha ya muzuri wakati unaokuja, lakini wakati tunachunguza mambo yenye wamefanya mupaka leo, tunaona kama hawana uwezo wa kumaliza magumu yenye kuwa katika dunia.—Zaburi 146:3, 4.

NAMNA YA KUFIKIRI NA WATU

12, 13. Namna gani tunaweza kuzungumuza na watu juu ya uumbaji ao juu ya Biblia?

12 Wakati unazungumuza na watu juu ya uumbaji ao juu ya Biblia, utafute kwanza kujua mambo yenye wanaamini kabisa. Ukumbuke kama watu fulani wenye kuamini mageuzi wanaamini pia kama kuna Mungu. Wanasema kama alitumia mageuzi ili kuumba vitu vyote vyenye kuwa na uzima. Wengine wanaamini kama fundisho la mageuzi linapaswa kuwa la kweli kwa sababu linafundishwa kwenye masomo. Na wengine wanaacha kuamini Mungu kwa sababu dini imewavunja moyo. Kwa hiyo, uliza kwanza mutu mambo yenye anaamini na sababu gani anaamini mambo hayo. Kisha umusikilize kwa uangalifu. Kama unafanya hivyo, anaweza kuwa tayari zaidi kukusikiliza.—Tito 3:2.

Kwa heshima, uulize watu mambo yenye wanaamini, na kisha uwasikilize kwa uangalifu

13 Ikiwa mutu fulani anasema kama uko mupumbavu kwa sababu unaamini kama kuna Muumbaji, unaweza kumujibu namna gani? Umuombe kwa heshima atoe mawazo yake juu ya namna uzima ulianza. Unaweza kusema kama ikiwa uzima uligeuka-geuka, kitu cha kwanza chenye kilikuwa na uzima kilipaswa kuwa na uwezo wa kutokeza vitu vingine vyenye kukifanana. Profesa mumoja wa kemia (chimie) alisema kama kiumbe cha kwanza kilipaswa kuwa na lazima ya mambo kama vile, (1) kitu fulani kama ngozi ili kukilinda, (2) uwezo wa kupata nguvu na kuitumia, (3) habari za kuchunguza namna kinatokea na kukomaa, na (4) uwezo wa kufanya kopi za habari hizo. Aliongeza hivi: “Hata aina nyepesi sana ya uzima ni yenye kushangaza sana.”

14. Ni mawazo gani mepesi unaweza kutumia wakati unazungumuza na watu juu ya uumbaji?

14 Wakati unazungumuza na watu juu ya uumbaji, unaweza kutumia mawazo haya mepesi yenye mutume Paulo alitumia. Aliandika hivi: ‘Kila nyumba inajengwa na mutu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.’ (Waebrania 3:4) Kwa kweli, kila nyumba iko na mutu fulani mwenye alifanya plan na kuijenga. Kwa hiyo, viumbe vyenye kuwa na uzima, vyenye kuwa vya ajabu sana kuliko nyumba, vinapaswa kuwa vilifanywa na mutu fulani. Unaweza pia kutumia vichapo vyetu. Dada mumoja alizungumuza na kijana fulani mwenye hakuamini kama kuna Mungu. Dada huyo alimupatia broshua mbili zenye tumekwisha kutaja katika habari hii, na kisha juma moja, kijana huyo alisema hivi: “Sasa ninaamini Mungu.” Kijana huyo alianza kujifunza Biblia na kisha akakuwa Shahidi wa Yehova.

15, 16. Tunapaswa kufanya nini mbele ya kufasiria mutu kama Biblia ilitoka kwa Mungu? Na tunapaswa kukumbuka nini sikuzote?

15 Namna gani unaweza kufikiri na mutu mwenye kuwa na mashaka juu ya Biblia? Kama vile tumekwisha kuona, umuulize kwanza mambo yenye anaamini. Pia, ujikaze kujua mambo yenye kumupendeza. (Methali 18:13) Ikiwa anapendezwa na sayansi, umutolee mifano ya Biblia yenye kuonyesha kama habari zenye inasema juu ya mambo ya sayansi ni za kweli sikuzote. Ikiwa anapendezwa na historia, unaweza kutaja tukio fulani lenye kuonyeshwa katika vitabu vya historia na umuonyeshe namna Biblia ilitabiri tukio hilo miaka mingi mbele lifanyike. Watu wengine wanaweza kukusikiliza ikiwa unawaonyesha jambo fulani katika Biblia lenye linaweza kufanya maisha yao kuwa ya muzuri, kwa mufano shauri fulani lenye kupatikana katika Mahubiri ya Yesu ya Mulimani.

16 Kumbuka kama hatupendi kubishana na watu. Tunapenda wafurahie kuzungumza na sisi na wajifunze Biblia. Kwa hiyo, uwaulize maulizo kwa heshima, na kisha uwasikilize kwa uangalifu. Wakati unazungumuza na mutu fulani juu ya mambo yenye unaamini, ukuwe na adabu, zaidi sana ikiwa mutu huyo ni mukubwa kuliko wewe. Kama unaheshimia wengine, wao pia wanaweza kukuheshimia. Na watashangaa kuona kama umefikiria kwa uzito mambo yenye unaamini hata kama ungali kijana. Kwa kweli, ikiwa mutu fulani anapenda tu kubishana na wewe ao kukuzarau, haiko lazima umujibie.—Methali 26:4.

VUMBUA MAFUNDISHO YA BIBLIA NA UTIE NGUVU IMANI YAKO

17, 18. (a) Ni nini inaweza kukusaidia utie nguvu imani yako katika Biblia? (b) Katika habari yenye kufuata, tutazungumuzia ulizo gani?

17 Tunaweza kujua mafundisho ya musingi ya Biblia, lakini tuko na lazima ya mambo mengi zaidi ili tukuwe na imani yenye nguvu. Tunapaswa kutafuta na kuvumbua mafundisho mazito yenye kuwa ndani, kama vile tunatafuta utajiri wenye kufichwa. (Methali 2:3-6) Moja kati ya njia za muzuri zaidi za kutia nguvu imani yako ni kusoma Biblia yote nzima. Pengine unaweza kupima kuisoma katika mwaka moja. Kufanya hivyo kulisaidia mwangalizi mumoja wa muzunguko amukaribie Yehova zaidi wakati alikuwa kijana. Alisema hivi: “Jambo moja lenye lilinisaidia kuona kama Biblia ni Neno la Mungu ni wakati niliisoma yote nzima. Nilifikia kuelewa hadisi za Biblia zenye nilijifunza wakati nilikuwa mutoto.” Pia, utumie vyombo vyenye kutusaidia kutafuta habari katika luga yako ili kuelewa mambo yenye unasoma. Unaweza kutumia Watchtower Library kwenye DVD, Watchtower—MAKTABA KWENYE INTERNETE, Index des Publications Watch Tower, ao Musaada wa Kutafuta Habari kwa Ajili ya Mashahidi wa Yehova.

18 Wazazi, ninyi ndio munastahili kufundisha watoto wenu juu ya Yehova, kuliko mutu mwengine yeyote. Kwa hiyo, namna gani munaweza kuwasaidia wakuwe na imani yenye nguvu kwake? Habari yenye kufuata itazungumuzia njia fulani za kufanya hivyo.

^ [1] (fungu la 9) Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 12, 2013.