Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

ENDELEA KUKESHA!

Janga la Wakimbizi—Mamilioni Wakimbia Kutoka Ukrainia

Janga la Wakimbizi—Mamilioni Wakimbia Kutoka Ukrainia

 Februari 24, 2022, Urusi ilivamia nchi ya Ukrainia na kutokeza janga kubwa sana la wakimbizi wanaokimbia vita hivyo. a

 “Kulikuwa na makombora na milipuko. Yalikuwa mambo yenye kutisha sana hivi kwamba siwezi kueleza. Tuliposikia kwamba magari-moshi yalikuwa yakiwatoa watu nchini, tuliamua kuondoka. Tulilazimika kuacha kila kitu kwa sababu mtu angeweza kubeba mfuko mmoja tu. Tulibeba tu hati, dawa, maji, na vyakula vidogo. Tuliacha kila kitu na kwenda kwenye kituo cha gari-moshi huku makombora yakiendelea kuanguka.”​—Nataliia, kutoka Kharkiv, Ukrainia.

 “Hadi dakika ya mwisho, tuliamini kwamba hakungekuwa na vita. Nilisikia milipuko katika maeneo fulani ya jiji, na madirisha yalikuwa yakitetemeka. Niliamua kuondoka, na kuchukua vitu vichache tu muhimu. Niliondoka saa 2:00 asubuhi na kupanda gari-moshi hadi Lviv, kisha nikapanda basi hadi Poland.”​—Nadija, kutoka Kharkiv, Ukrainia.

Katika makala hii

 Ni nini chanzo halisi cha janga hili la wakimbizi?

 Janga la wakimbizi wa Ukrainia limetokezwa na uvamizi wa jeshi la Urusi. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba kuna sababu kubwa hata zaidi inayotokeza majanga ya wakimbizi:

  •   Serikali za wanadamu zimeshindwa kuwapa wanadamu kile ambacho wanahitaji hasa. Mara nyingi, watu walio madarakani hutumia mamlaka yao kuwakandamiza wengine.​—Mhubiri 4:1; 8:9.

  •   Shetani Ibilisi, “mtawala wa ulimwengu,” anatokeza uvutano mwovu juu ya wanadamu hivi kwamba Biblia inasema hivi: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.”​—Yohana 14:30; 1 Yohana 5:19.

  •   Mbali na matatizo ambayo yamewasumbua wanadamu kwa karne nyingi, sasa tunaishi katika kipindi cha wakati kilichotabiriwa katika Biblia: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Siku hizo zingetambuliwa kutokana na vita, misiba ya asili, upungufu wa chakula, na magonjwa—matatizo ambayo huwalazimisha watu kukimbia na kuacha makao yao.​—Luka 21:10, 11.

 Wakimbizi wanaweza kupata wapi tumaini?

 Biblia inafunua kwamba Muumba wetu, Yehova, b ni Mungu ambaye anawapenda na kuwahurumia wakimbizi na watu waliolazimika kuacha makao yao. (Kumbukumbu la Torati 10:18) Anaahidi kwamba atatumia serikali yake ya mbinguni, inayoitwa Ufalme wa Mungu, kutatua matatizo ya wakimbizi. Serikali hiyo itachukua mahali pa serikali za wanadamu. (Danieli 2:44; Mathayo 6:10) Yehova atatumia Ufalme wake kumwondoa Shetani Ibilisi. (Waroma 16:20) Ufalme huo utakuwa serikali ya ulimwenguni pote, itakayoondoa migawanyiko iliyotokezwa na mipaka ya kitaifa. Wanadamu wote watafanyiza familia ya ulimwenguni pote yenye umoja. Hakuna mtu atakayehitaji kukimbia kutoka nyumbani kwake tena, kwa kuwa Biblia inaahidi hivi: “Wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, na hakuna yeyote atakayewaogopesha, kwa maana kinywa cha Yehova wa majeshi kimesema hayo.”​—Mika 4:4.

 Ni Ufalme wa Mungu tu unaoweza kuandaa suluhisho la kudumu kwa tatizo la wakimbizi tunaloona leo. Yehova atatumia Ufalme wake kuondoa matatizo yanayowalazimisha watu kuwa wakimbizi. Fikiria mifano michache:

  •   Vita. “[Yehova] anakomesha vita katika dunia yote.” (Zaburi 46:9) Ili kuona jinsi Mungu atakavyokomesha vita, soma makala yenye kichwa “Amani Duniani—Itapatikanaje?

  •   Ukandamizaji na jeuri. “[Yehova] atawaokoa kutoka katika ukandamizaji na ukatili.” (Zaburi 72:14) Ili kuelewa jinsi watu wanavyoweza kubadili mitazamo isiyofaa ambayo imekuwepo kwa muda mrefu, soma mfululizo wa makala yenye kichwa “Jinsi ya Kushinda Chuki.”

  •   Umaskini. “[Yehova] atamwokoa maskini anayelilia msaada.” (Zaburi 72:12) Ili kuona jinsi ambavyo Mungu atatatua chanzo cha umaskini, soma makala yenye kichwa “Je, Inawezekana Kuwa na Mfumo wa Kiuchumi Wenye Usawa?

  •   Ukosefu wa chakula. “Kutakuwa na nafaka nyingi duniani.” (Zaburi 72:16) Ili kujifunza jinsi Mungu atakavyohakikisha kwamba hakuna mtu anayelala njaa, ona makala yenye kichwa “Ulimwengu Usio na Njaa.”

 Je, Biblia inaweza kuwasaidia wakimbizi leo?

 Ndiyo. Mbali na kuwapa wakimbizi tumaini hakika la wakati ujao, Biblia inaweza kuwasaidia kukabiliana na changamoto wanazokabili sasa hivi.

 Kanuni ya Biblia: “Mjinga huamini kila neno, lakini mwerevu hutafakari kila hatua.”​—Methali 14:15.

 Maana: Tarajia hatari unazoweza kukabili na jinsi ya kujilinda. Jihadhari na wahalifu wanaowavizia na kuwatumia vibaya wakimbizi kwa kuwa wanajua hawajihisi salama na hawafahamu eneo ambalo wamekimbilia.

 Kanuni ya Biblia: “Tukiwa na chakula na mavazi, tutaridhika na vitu hivyo.”​—1 Timotheo 6:8.

 Maana: Epuka kukazia fikira vitu vya kimwili. Unaporidhika na vitu vya msingi, utakuwa na furaha zaidi.

 Kanuni ya Biblia: “Basi, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima ninyi pia mwatendee vivyo hivyo.”​—Mathayo 7:12.

 Maana: Uwe na subira na fadhili. Sifa hizo zitakusaidia kuwafanya watu wakuheshimu na kukukubali.

 Kanuni ya Biblia: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu.”​—Waroma 12:17.

 Maana: Usiruhusu hasira ikufanye ulipize kisasi unapotendewa kwa njia isiyofaa. Hilo litafanya mambo yawe mabaya zaidi.

 Kanuni ya Biblia: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.”​—Wafilipi 4:13.

 Maana: Mfanye Mungu awe sehemu muhimu ya maisha yako na usali kwake. Anaweza kukuimarisha ukabiliane na hali.

 Kanuni ya Biblia: “Msihangaike kuhusiana na jambo lolote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani, mjulisheni Mungu maombi yenu; na amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.”​—Wafilipi 4:6, 7.

 Maana: Mwombe Mungu akupe amani ya akili na moyoni unapokuwa katika hali yoyote ile. Ona makala yenye kichwa “Wafilipi 4:6, 7—‘Msihangaike Kuhusiana na Jambo Lolote.’

a Siku moja baada ya uvamizi huo, Tume ya Umoja wa Mataifa Inayoshughulikia Wakimbizi (UNHCR) ilisema kwamba hiyo ndiyo hali ya dharura zaidi katika shambulizi hilo. Ndani ya siku 12 tu, zaidi ya wakimbizi milioni mbili walikuwa wamekimbilia nchi jirani, huku watu milioni moja ambao bado wako nchini Ukrainia wamelazimika kuacha makao yao.

b Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?