Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Kwa Nini Ukatae Kufinyangwa na Vyombo vya Habari?​—Sehemu ya 1: Kwa Wasichana

Kwa Nini Ukatae Kufinyangwa na Vyombo vya Habari?​—Sehemu ya 1: Kwa Wasichana

 Vyombo vya habari huendeleza mawazo na mitazamo gani?

 Tazama maneno haya, kisha ujibu maswali yafuatayo.

Safu ya 1

Safu ya 2

Wasio wakomavu

Wanaowajibika

Waasi

Wanaotii Sheria

Wenye Maadili Mapotovu

Walio Safi Kiadili

Wasio na Busara

Wanaotenda kwa Hekima

Wenye Porojo

Wenye Busara

Waongo

Wanyoofu

  1.   Ni maneno gani yanayofafanua vizuri jinsi unavyowaona wasichana wanaoonyeshwa katika sinema, televisheni, na magazeti?

  2.   Ni maneno gani yanayofafanua jinsi ambavyo wewe ungependa watu wakuone?

 Inaelekea kwamba ulipata majibu ya swali la kwanza katika safu ya 1 na majibu ya swali la pili katika safu ya 2. Ikiwa ndivyo, hilo linamaanisha kwamba ungependa kuwa bora zaidi ya tineja “wa kawaida” anayeonyeshwa katika vyombo vya habari​—na si wewe peke yako unayehisi hivyo! Fikiria ni kwa nini.

 “Sinema huonyesha msichana tineja wa kawaida akiwa mwasi na mfidhuli. Hilo hufanya sote tuonekane kuwa watu wasiotumainika, wanaozingatia hadhi yao katika jamii na wanaofanya mambo madogo yaonekane kuwa makubwa kupita kiasi.”​—Erin

 “Wasichana matineja wanaoonyeshwa kwenye sinema na televisheni wanapenda kujionyesha mbele ya watu na wanahangaikia sana sura, mavazi, umaarufu, na wavulana.”​—Natalie

 “Mara nyingi msichana ‘kamili’ hunywa pombe, hulala na wavulana, na anaasi wazazi wake. Ikiwa msichana anayeonyeshwa hafanyi mambo hayo, basi anaonwa kuwa mtakatifu sana au mshamba kuhusu mambo ya ngono.”​—Maria

 Jiulize hivi: ‘Je, mavazi, matendo, na maneno yangu yanaonyesha jinsi nilivyo kikweli, au ninaiga tu mawazo na mitazamo inayoendelezwa katika vyombo vya habari?’

 Mambo unayopaswa kujua

  •   Wengi wanaofikiri kwamba wameanzisha mtindo wao wenyewe kwa kweli wanaiga tu mitindo inayoendelezwa na vyombo vya habari. Mwanamke kijana anayeitwa Karen anasema hivi: “Mimi huona jinsi dada yangu mdogo anavyojiendesha. Ni kana kwamba hangaiko lake kuu ni mavazi na wavulana. Yeye ni mwerevu, na ninajua kwamba anapendezwa na mambo mengine, lakini yeye huyapuuza tu kwa sababu anafikiri kwamba hiyo ndiyo njia pekee ya kufanana na ‘wale wasichana wengine wote.’ Na ana miaka 12 tu!”

     Biblia inasema hivi: “Acheni kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo.”​—Waroma 12:2.

  •   Si wasichana wote ambao wangependa kuiga mawazo na mitazamo inayoendelezwa na vyombo vya habari. Alexis, mwenye umri wa miaka 15 anasema hivi: “Katika vyombo vya habari, wasichana huonyeshwa wakiwa wanajifikiria kupita kiasi, washenzi, na wenye mwelekeo wa kufanya mambo ya kitoto, lakini nafikiri wengi wetu tunataka kuwa na tabia bora zaidi. Tuna mambo mengine ya kufanya maishani kuliko kuwaza tu kuhusu mvulana mwenye sura nzuri.”

     Biblia inasema hivi: ‘Watu wakomavu hutumia nguvu zao za ufahamu zilizozoezwa ili kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’​—Waebrania 5:14.

  •   Kuiga mawazo na mitazamo inayoendelezwa katika vyombo vya habari huwanufaisha wafanya-biashara​—si wasichana matineja. Viwanda vikubwa, kutia ndani viwanda vya uchapishaji, vya mitindo, vya teknolojia, na vya burudani, vimetambua kwamba vinaweza kupata faida kubwa vikiwalenga hasa vijana kabla hawajawa matineja. Kitabu 12 Going on 29, cha Kiingereza, kinasema hivi: “Matangazo ya kibiashara yanawaonyesha vijana walio chini ya umri wa utineja kwamba ikiwa hawana mavazi, vito, vipodozi, na vifaa vya kisasa vya kielektroni, hawatakuwa maarufu. Vijana hao huona kila mara matangazo ya kibiashara yenye kuvutia, hata kabla hawajaelewa wanashawishiwa kufanya nini.”

     Biblia inasema hivi: “Kila kitu kilicho katika ulimwengu​—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani​—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.”​—1 Yohana 2:​16.

 Jambo la kufikiria: Ni nani anayefaidika zaidi unapofikiria kupita kiasi kuhusu mitindo maarufu na ya kisasa zaidi ya mavazi? Ni nani hasa anayefaidika ikiwa lazima ununue simu ya karibuni zaidi ili uwe maarufu kati ya rafiki zako? Je, wafanya-biashara wanakuhangaikia wewe au wanajihangaikia wenyewe?

 Mambo unayoweza kufanya?

  •   Jifunze kuchanganua mawazo na mitazamo unayoona katika vyombo vya habari. Unapoendelea kukua, unasitawisha uwezo wa kutoona mambo kijuu-juu tu. Tumia utambuzi kufikiria jinsi mawazo na mitazamo inayoendelezwa na vyombo vya habari inavyoweza kukuathiri. Alana, mwenye umri wa miaka 14 anasema hivi: “Kwa kawaida, vyombo vya habari huonyesha kwamba msichana tineja anapaswa kujipaka vipodozi vingi na kuvaa nguo fupi sana, na matineja wengi hawatambui kwamba hilo huwafanya waonekane kuwa wamekata tamaa badala ya kupendeza.”

  •   Jiwekee viwango vitakavyokusaidia kuwa mtu bora. Kwa mfano, fikiria sifa zilizokuvutia mwanzoni mwa makala hii​—sifa ambazo ungependa kuwa nazo. Kwa nini usianze sasa kuzisitawisha au kuziboresha? Biblia inasema hivi: “Mjivike utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba”​—si kulingana na mitindo inayopendekezwa na vyombo vya habari.​—Wakolosai 3:​10.

  •   Tafuta vielelezo vinavyofaa. Unaweza kuwapata katika familia yako, kama vile mama au shangazi yako. Wengine wanaweza kuwa wanawake unaowafahamu au marafiki waliokomaa. Mashahidi wa Yehova wana pendeleo la kuwa na wanawake wengi Wakristo waliokomaa katika kutaniko la Kikristo.​—Tito 2:​3-5.

 Pendekezo: Tumia kitabu Igeni Imani Yao ili ujifunze kuhusu mifano bora ambayo wanawake wanaweza kuiga iliyo katika Biblia, inayotia ndani Ruthu, Hana, Abigaili, Esta, Maria, na Martha. Kitabu Igeni Imani Yao kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova na kinapatikana katika www.pr418.com/sw.