Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Ni Kosa Kufanya Ngono Kati ya Watu wa Jinsia Moja?

Je, Ni Kosa Kufanya Ngono Kati ya Watu wa Jinsia Moja?

 “Nilipokuwa nikikua, jambo moja ambalo lilinihangaisha sana ni hisia zangu za kuvutiwa kingono na watu wa jinsia yangu. Nilifikiri hisia hizo zitapita, lakini bado zinaendelea kunisumbua.”​—David, mwenye umri wa miaka 23.

 David ni Mkristo ambaye anataka kumpendeza Mungu. Je, anaweza kumpendeza Mungu ikiwa anavutiwa kingono na watu wa jinsia yake? Mungu anahisije kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja?

 Biblia inasema nini?

 Mtazamo kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja unatofautiana kati ya jamii moja na nyingine na unaweza kubadilika kulingana na wakati. Hata hivyo, Wakristo hawaongozwi na maoni yanayoungwa mkono na watu wengi au “kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho.” (Waefeso 4:​14) Badala yake, maoni yao kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja (na mwenendo mwingine wowote) yanategemea viwango vya Biblia.

 Viwango vya Biblia kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja viko wazi. Neno la Mungu linasema:

  •  “Usilale na mwanamume kama vile unavyolala na mwanamke.”​—Mambo ya Walawi 18:22.

  •  “Kupatana na tamaa za mioyo yao, Mungu aliwaacha katika hamu za ngono yenye kufedhehesha, kwa maana wanawake wao walibadili matumizi yao wenyewe ya asili kuwa yale yaliyo kinyume cha asili.”​—Waroma 1:​24, 26.

  •  “Msipotoshwe. Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume wanaowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume wanaolala na wanaume, wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi hawataurithi ufalme wa Mungu.”​—1 Wakorintho 6:​9, 10.

 Bila shaka, viwango vya Mungu vinawahusu watu wote, iwe wana tamaa ya kufanya ngono na watu wa jinsia moja au jinsia tofauti. Ukweli ni kwamba, kila mtu anapaswa kujizuia anaposhawishiwa kujihusisha katika mwenendo usiompendeza Mungu.​—Wakolosai 3:5.

 Je, hilo linamaanisha . . . ?

 Je, hilo linamaanisha kwamba Biblia inachochea chuki dhidi ya mashoga?

 Hapana. Kwa kweli, Biblia haiungi mkono chuki dhidi ya mtu yeyote, awe ni shoga au si shoga. Badala yake, inatuambia “tufuatilie amani pamoja na watu wote,” licha ya mtindo wao wa maisha. (Waebrania 12:14) Kwa hiyo ni kosa kuwanyanyasa, kuwatendea kwa ukatili, au kuwatesa kwa njia yoyote watu wanaofanya ngono na watu wa jinsia yao.

 Je hilo linamaanisha Wakristo wanapaswa kupinga sheria zinazoruhusu ndoa za watu wa jinsia moja?

 Biblia inaonyesha kwamba viwango vya Mungu kuhusu ndoa ni muungano wa mwanamume mmoja na mwanamke mmoja. (Mathayo 19:​4-6) Hata hivyo, mijadala ya sheria za wanadamu kuhusu ndoa za jinsia moja inahusiana na mambo ya kisiasa na si ya kimaadili. Biblia inawahimiza Wakristo wasiunge mkono upande wowote wa kisiasa. (Yohana 18:36) Kwa hiyo, hawaungi mkono wala kupinga sheria za serikali zinazohusiana na ndoa za watu wa jinsia moja au matendo ya ngono kati ya watu wa jinsia moja.

 Lakini vipi ikiwa . . . ?

 Lakini vipi ikiwa mtu ni shoga? Je, anaweza kubadilika?

 Ndiyo. Baadhi ya watu katika karne ya kwanza walikuwa hivyo! Baada ya kueleza kwamba wale wanaofanya ngono na watu wa jinsia yao hawataurithi Ufalme wa Mungu, Biblia inasema hivi: “Wengine wenu mlikuwa hivyo.”​—1 Wakorintho 6:​11.

 Je, hilo linamaanisha kwamba, watu walioacha mazoea ya kufanya ngono na watu wa jinsia yao hawakuwahi kuhisi kana kwamba wanatamani maisha yao ya zamani? La. Biblia inasema hivi: “Mjivike utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya.” (Wakolosai 3:​10) Mabadiliko ni jambo la kuendelea.

 Lakini vipi ikiwa mtu anataka kufuata viwango vya Mungu lakini bado ana tamaa ya ngono ya jinsia moja?

 Kama tu ilivyo na tamaa ya aina yoyote, mtu anaweza kuamua kutotenda kupatana na tamaa hiyo. Jinsi gani? Biblia inasema hivi: “Endeleeni kutembea kwa roho nanyi hamtatenda tamaa ya kimwili hata kidogo.”​—Wagalatia 5:​16.

 Ona kwamba mstari huo hausemi kwamba mtu hatakuwa na tamaa ya kimwili. Badala yake, akiwa na ratiba nzuri ya kufanya mambo ya kiroho kama vile kusoma Biblia na kusali, atapata nguvu za kupinga tamaa hizo.

 David, aliyetajwa mwanzoni, alitambua ukweli wa jambo hilo​—hasa baada ya kuzungumza na wazazi wake Wakristo kuhusu mahangaiko yake. Anasema hivi: “Nilihisi kana kwamba nimeondolewa mzigo mzito sana. Huenda ningefurahia zaidi miaka yangu ya utineja ikiwa ningezungumza nao mapema.”

 Kwa kweli, tunapata furaha nyingi sana tunapofuata viwango vya Yehova. Tuna hakika kwamba maagizo ya Yehova “ni manyoofu, huufanya moyo ushangilie,” na kwamba “katika kuyashika kuna thawabu kubwa.”​—Zaburi 19:​8, 11.