Hamia kwenye habari

Je, Mungu Alitumia Mageuzi Kuumba Aina Mbalimbali za Uhai?

Je, Mungu Alitumia Mageuzi Kuumba Aina Mbalimbali za Uhai?

Jibu la Biblia

 Hapana. Biblia inasema waziwazi kwamba Mungu aliumba wanadamu na pia “aina” tofauti-tofauti za wanyama na mimea. a (Mwanzo 1:12, 21, 25, 27; Ufunuo 4:11) Inasema kwamba familia yote ya wanadamu ilitokana na wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa. (Mwanzo 3:20; 4:1) Simulizi la Biblia haliungi mkono nadharia ya kwamba Mungu alitumia mageuzi kutokeza aina mbalimbali za uhai. Nyakati nyingine wazo hilo husemekana kuwa ni nadharia ya wanaoamini kwamba kuna Mungu lakini wanaoamini pia katika mageuzi. Hata hivyo, ukweli wa mambo ni kwamba hakuna chochote katika Biblia kinachopingana na mambo ambayo wanasayansi wamejionea kwamba mabadiliko hutokea katika aina mbalimbali za viumbe.

 Je, Mungu alitumia mageuzi?

 Wanaoamini kwamba kuna Mungu lakini uhai ulitokana na mageuzi wana mawazo ya aina mbalimbali. Kulingana na Encyclopædia Britannica, wanaendeleza wazo la kwamba “uteuzi wa kiasili ni mojawapo ya njia ambazo Mungu hutumia kuongoza ulimwengu wa asili.”

 Kuamini kwamba kuna Mungu lakini uhai ulitokana na mageuzi kunaweza kutokeza mawazo yafuatayo:

  •   Viumbe vyote vilitokana na vyanzo vilevile wakati uliopita.

  •   Aina moja ya uhai inaweza kutokeza aina nyingine tofauti kabisa ya uhai kupitia mageuzi.

  •   Kwa njia fulani Mungu ndiye anayesababisha michakato hiyo yote.

 Je, mageuzi yanapatana na Biblia?

 Kuamini kwamba kuna Mungu lakini uhai ulitokana na mageuzi kunadokeza kwamba simulizi la Biblia kuhusu uumbaji lililo kwenye Mwanzo si sahihi kabisa. Hata hivyo, Yesu alirejelea simulizi la Mwanzo kuwa jambo hakika la kihistoria. (Mwanzo 1:26, 27; 2:18-24; Mathayo 19:4-6) Biblia inasema kwamba kabla ya kuja duniani, Yesu aliishi mbinguni pamoja na Mungu na alimsaidia Mungu kutokeza “vitu vyote.” (Yohana 1:3) Hivyo, wazo la kwamba Mungu alitumia mageuzi kutokeza aina mbalimbali za uhai halipatani na mafundisho ya Biblia.

 Namna gani kuhusu uwezo wa mimea na wanyama kubadilika?

 Biblia haielezi ni mabadiliko kadiri gani yanayoweza kutokea katika viumbe vya aina moja. Wala haipingi ukweli wa kwamba aina tofauti-tofauti za wanyama na mimea iliyoumbwa na Mungu inaweza kubadilika kadiri inavyozaliana au kujipatanisha na mazingira mapya. Ingawa watu fulani huona mabadiliko hayo kuwa aina fulani ya mageuzi, hakuna uhai mpya unaotokezwa.

a Biblia inatumia neno “aina,” ambalo lina maana pana zaidi kuliko neno “spishi” linalotumiwa na wanasayansi. Mara nyingi, wanasayansi wanaposema kwamba mageuzi yametokeza aina mpya ya kiumbe, kwa kawaida huwa ni mabadiliko tu katika aina ileile ya kiumbe, kama neno linalotumiwa katika simulizi la Mwanzo linavyomaanisha.