Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Mwanzo 1:1​—“Hapo Mwanzo Mungu Aliumba Mbingu na Dunia”

Mwanzo 1:1​—“Hapo Mwanzo Mungu Aliumba Mbingu na Dunia”

 “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.”—Mwanzo 1:1, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.”—Mwanzo 1:1, Union Version.

Maana ya Mwanzo 1:1

 Mstari huo wa kwanza katika Biblia unataja kweli mbili muhimu. Kwanza, “mbingu na dunia,” au ulimwengu unaoonekana, ulikuwa na mwanzo. Pili, mbingu na dunia ziliumbwa na Mungu.—Ufunuo 4:11.

 Biblia haitaji ni lini Mungu aliumba ulimwengu, wala haisemi jinsi alivyoumba. Lakini inaeleza kwamba aliumba ulimwengu kwa kutumia “nguvu zake nyingi zenye msukumo na nguvu zake zenye kuogopesha.”—Isaya 40:26.

 Neno “aliumba” limetafsiriwa kutokana na kitenzi cha Kiebrania ambacho kinatumiwa tu kufafanua kazi ambayo Mungu anafanya. a Katika Biblia, Yehova b Mungu ndiye tu anayefafanuliwa kuwa Muumba.—Isaya 42:5; 45:18.

Muktadha wa Mwanzo 1:1

 Mstari huu wa kwanza wa kitabu cha Mwanzo unatoa utangulizi wa simulizi la uumbaji linalopatikana katika Mwanzo sura ya 1 na 2. Kuanzia Mwanzo 1:1 hadi 2:4, Biblia inasimulia kifupi hatua ambazo Mungu alichukua alipokuwa akiumba dunia na vitu vyote vilivyo hai duniani, kutia ndani mwanamume na mwanamke wa kwanza. Baada ya muhtasari huo, Biblia inatoa maelezo zaidi kuhusu kuumbwa kwa mwanamume na mwanamke.—Mwanzo 2:7-25.

 Simulizi la Mwanzo linaelezea kwamba kazi ya Mungu ya kuumba ilifanywa hatua kwa hatua katika kipindi cha “siku” sita. Hizo hazikuwa siku halisi zenye saa 24, bali ni vipindi vya wakati vyenye urefu ambao haujatajwa. Neno “siku” linaweza kutumiwa kuhusiana na vipindi vya wakati ambavyo si vya saa 24. Hilo linaonekana kwenye Mwanzo 2:4, ambapo neno “siku” linatumiwa kama kisawe cha neno “wakati” na kujumlisha shughuli zote za Mungu za uumbaji katika siku sita zilizotangulia kana kwamba zilifanywa kwa “siku” moja.”

Maoni Yasiyo Sahihi Kuhusu Mwanzo 1:1

 Maoni yasiyo sahihi: Mungu aliumba ulimwengu unaoonekana miaka elfu kumi hivi iliyopita.

 Ukweli: Biblia haisemi ulimwengu uliumbwa lini. Maneno yaliyo kwenye Mwanzo 1:1 hayapingani na makadirio ya kisasa kwamba ulimwengu umekuwepo kwa mabilioni ya miaka. c

 Maoni yasiyo sahihi: Andiko la Mwanzo 1:1 linaonyesha kwamba Mungu ni Utatu kwa sababu neno la Kiebrania Mungu limeandikwa kwa wingi katika mstari huo.

 Ukweli: Jina la cheo “Mungu” linatafsiriwa kutokana na neno la Kiebrania ’Elo·himʹ, ambalo linaandikwa kwa wingi, ili kuonyesha ukuu au heshima, bali si idadi ya watu. Kitabu New Catholic Encyclopedia kinasema kwamba neno la wingi ’Elo·himʹ lililotumiwa kwenye Mwanzo 1:1 “sikuzote huambatana na kitenzi kinachoonyesha kitu kimoja na hivyo kuonyesha kwamba, kama vile mfalme alivyotumia neno sisi, wingi huu unamaanisha heshima, bali si idadi.”—Toleo la Pili, Buku la 6, ukurasa wa 272.

Soma Mwanzo sura ya 1 pamoja na ufafanuzi wa maelezo ya chini na marejeo ya pambizoni.

a Biblia ya HCSB Study Bible inasema: “Katika hali ya kutenda kitenzi cha Kiebrania bara’, kinachomaanisha ‘kuumba,’ hakitumiwi kuhusiana na kitendo kinachofanywa na mwanadamu. Basi kitenzi bara’ kinahusu kazi inayofanywa na Mungu peke yake.”— Ukurasa wa 7.

b Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu.—Zaburi 83:18.

c Kuhusu kipindi cha wakati ambacho kimetafsiriwa “hapo mwanzo” kutoka kwa Kiebrania, kitabu The Expositor’s Bible Commentary kinasema: “Maneno hayo hayaonyeshi urefu au muda wa kipindi hicho.”—Toleo Lililorekebishwa, Buku la I, ukurasa wa 51.