Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Kutafsiri Programu ya Kusanyiko la Eneo la 2020 “Shangilieni Sikuzote”!

Kutafsiri Programu ya Kusanyiko la Eneo la 2020 “Shangilieni Sikuzote”!

JULAI 10, 2020

 Kwa mara ya kwanza kabisa, mnamo Julai na Agosti 2020, ndugu ulimwenguni pote watatazama programu ileile ya kusanyiko la eneo wakati uleule. Ili hilo liwezekane, rekodi za programu hiyo zilihitaji kutafsiriwa katika lugha zaidi ya 500. Kwa kawaida, mradi kama huo ungehitaji kupangwa na kushughulikiwa kwa mwaka mzima au zaidi. Lakini kwa sababu ya hali zinazotokana na ugonjwa wa virusi vya corona, watafsiri wa Kusanyiko la Eneo la 2020 lenye kichwa “Shangilieni Sikuzote!” walikuwa na muda usiozidi miezi minne kukamilisha kazi hiyo.

 Idara ya Huduma za Tafsiri na Idara ya Ununuzi ya Ulimwenguni Pote zilizo katika Makao Makuu ya Ulimwenguni Pote ya Mashahidi wa Yehova zilisaidia kutimiza mradi huo mkubwa. Idara ya Huduma za Tafsiri ilitambua kwamba vikundi vingi vya utafsiri vilihitaji vifaa vya ziada kufanya kazi hiyo, hasa maikrofoni za hali ya juu. Idara ya Ununuzi ya Ulimwenguni Pote ilifanya mipango ya kununua maikrofoni 1,000 na kuzisafirisha katika maeneo 200 tofauti.

 Ili kuokoa pesa, maikrofoni hizo zilinunuliwa kwa jumla, zikasafirishwa hadi sehemu moja, kisha zikapakiwa upya ili kusafirishwa sehemu mbalimbali ulimwenguni pote. Kwa kununua maikrofoni nyingi kwa wakati mmoja, kila moja iligharimu wastani wa dola 170 za Marekani, kutia ndani gharama za usafirishaji, na kufanya hivyo kuliokoa zaidi ya asilimia 20 ya gharama ya kununua mojamoja.

 Idara ya Ununuzi ya Ulimwenguni Pote ilihitaji kufanya ununuzi wote huo ndani ya mwezi wa Aprili na Mei 2020—wakati ambapo biashara nyingi hazingeweza kufanya kazi kama kawaida kwa sababu ya ugonjwa wa virusi vya corona. Hata hivyo, kufikia mwishoni mwa Mei, vifaa vilikuwa vimefika katika ofisi nyingi za utafsiri, ofisi za tawi, na maeneo mengine ambapo kazi ya kutafsiri inafanyiwa.

 Jay Swinney, mwangalizi wa Idara ya Ununuzi ya Ulimwenguni Pote anasema hivi: “Kulikuwa na ushirikiano mzuri kati ya idara za Betheli na wafanyabiashara wanaohusika wakati wa mradi wote huu. Ni roho ya Yehova tu inayoweza kuunganisha jitihada zetu ili kutimiza mahitaji ya kitheokrasi kwa muda mfupi hivyo na kwa gharama ndogo.”

 Nicholas Ahladis, anafanya kazi katika Idara ya Huduma za Tafsiri, anasema hivi: “Watafsiri ambao walikuwa wamewekewa vizuizi vya kutotoka nyumbani walitiwa moyo sana kupata vifaa hivyo. Licha ya kwamba hawangeweza kuchangamana na wengine katika vikundi vyao vya kutafsiri, wangeweza kufanya kazi pamoja ili kutafsiri na kurekodi hotuba, drama, na nyimbo katika lugha zaidi ya 500.”

 Huo ni mradi mmoja kati ya miradi mingi iliyotimizwa ili kutokeza Kusanyiko la Eneo la 2020 lenye kichwa “Shangilieni Sikuzote”! kwa ajili ya ndugu na dada ulimwenguni pote. Michango yenu ya ukarimu kupitia donate.pr418.com na kupitia njia nyingine zilisaidia kununua vifaa hivyo muhimu.