Hamia kwenye habari

Dakt. Gabriele Hammermann, msimamizi wa Eneo la Kambi ya Mateso ya Dachau, akionyesha picha ya bamba la kumkumbuka Max Eckert alipotoa hotuba.

JULAI 9, 2018
UJERUMANI

Sasa Anajulikana: Max Eckert Akumbukwa Katika Maadhimisho Yaliyofanywa Kwenye Kambi ya Mateso ya Dachau

Sasa Anajulikana: Max Eckert Akumbukwa Katika Maadhimisho Yaliyofanywa Kwenye Kambi ya Mateso ya Dachau

Katika maadhimisho yaliyofanywa Mei 7, 2018 kwenye Eneo la Kambi ya Mateso ya Dachau, watu 200 hivi walionyeshwa bamba la kumkumbuka Ndugu Max Eckert ambaye alifungwa katika kambi ya Dachau kwa miaka zaidi ya miwili kabla ya kupelekwa kwenye kambi ya mateso ya Mauthausen yenye sifa mbaya nchini Austria. Hakurudi nyumbani. Ingawa Ndugu Eckert alikufa bila kujulikana na wengi, sasa anatambuliwa na wote kuwa mwanamume mwenye imani isiyotikisika.

Picha ya karibuni ya kambi ya mateso ya zamani ya Dachau ambako Max Eckert alifungwa kabla ya kupelekwa Mauthausen.

Kambi ya mateso ya Mauthausen ambako Max Eckert alikufa.

Rekodi zinaonyesha utimilifu wa Ndugu Eckert. Yeye na mkewe walitozwa faini mwaka wa 1935 hivi kwa kuwaeleza wengine imani yao. Baadaye alifutwa kazi kwa kukataa kubeba bendera yenye swastika. Mwaka wa 1937, alikuwa mmoja kati ya Mashahidi wa Yehova jasiri 600 hivi waliopelekwa kwenye kambi ya Dachau. Zaidi ya miaka miwili baadaye, alihamishiwa kwenye kambi ya Mauthausen ambako wafungwa 90,000 hivi walikufa kwa sababu ya hali ngumu sana. Februari 21, 1940, mke wa Ndugu Eckert alipata telegramu iliyosema tu: “Mume alikufa leo katika kambi. Kwa habari zaidi ongea na polisi.” Alikuwa na umri wa miaka 43.

Alipotoa hotuba yake katika maadhimisho hayo, Dakt. Gabriele Hammermann, msimamizi wa Eneo la Kambi ya Mateso ya Dachau, alisema hivi: “Wanafunzi wa Biblia [kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo] waliteswa kwa sababu imani yao haikuwaruhusu kuwa washiriki wa mashirika ya Wanazi, kumpigia Hitler saluti, au kushiriki katika utumishi wa kijeshi.” Alisema hivi pia: “Wafungwa wa zamani [walizungumzia] mtazamo wa Wanafunzi wa Biblia kwa heshima kubwa na hasa [walikazia] ushikamanifu wao na utayari wa kusaidia.”

Ndugu Wolfram Slupina, msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani, alikubali kwamba wengi waliohudhuria hawakumfahamu Ndugu Eckert, na kusema kwamba: “Hata hatuna picha ya Max Eckert.” Lakini akaendelea kusema kwamba bamba hilo limefaulu “kutambua ushikamanifu ambao [Ndugu Eckert] alionyesha na imani ya kidini yenye nguvu, hakukubali kuridhiana hata alipokabili kifo.”

Bila shaka, Yehova anakumbuka imani na utimilifu wa Max Eckert, pamoja na Mashahidi wa Yehova wote ambao wamekufa kwa sababu ya imani yao.—Waebrania 6:10.