Hamia kwenye habari

SEPTEMBA 3, 2020
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Kusanyiko la Eneo la 2020—Kusanyiko la Kwanza Kufanywa Duniani Pote Kupitia Video Mtandaoni

Kusanyiko la Eneo la 2020—Kusanyiko la Kwanza Kufanywa Duniani Pote Kupitia Video Mtandaoni

Katika miezi ya Julai na Agosti 2020, mamilioni ya ndugu na dada zetu, pamoja na watu wanaopendezwa walitazama programu ya kusanyiko la eneo la 2020.

Mashahidi wa Yehova walitazamia kwa hamu kufanya kusanyiko la Eneo la “Shangilieni Sikuzote”! katika Majumba ya Kusanyiko, maeneo ya makusanyiko, au katika viwanja vya michezo katika nchi 240. Ili kulinda afya ya wale ambao wangehudhuria kusanyiko hilo, Baraza Linaloongoza liliamua kwamba kusanyiko la eneo lifanywe duniani pote kupitia video mtandaoni. Hii ni mara ya kwanza kwa tengenezo tangu mwaka wa 1897, kutofanya kusanyiko lenye wahudhuriaji waliokusanyika pamoja.

Kenneth Cook, Jr., mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alisema: “Kusanyiko la eneo lilipofutwa, lengo letu lilikuwa kufanya kusanyiko ambalo kila mtu angeweza kuhudhuria katika kipindi kilekile. Tulijua kwamba programu hiyo ilipaswa kutayarishwa katika lugha nyingi ndani ya kipindi kisichozidi miezi minne. Kwa kawaida kazi hiyo huchukua mwaka mmoja au zaidi kuanzia matayarisho mpaka kuikamilisha. Julai 6, 2020, tulifurahi sana kuona sehemu ya kwanza ya kusanyiko hilo mtandaoni katika lugha 400 hivi. Tunatazamia kwamba programu hiyo itapatikana katika lugha 511!”

Dada yetu mmoja ambaye ni mzazi anayelea watoto wake watatu peke yake, alisema hivi kuhusu programu hiyo: “Ingawa tunakosa kuwa pamoja na ndugu na dada zetu, watoto wetu wamenufaika sana. Kutazama programu hiyo kwa sehemu fupi, kumewasaidia sana kukazia fikira. Tulisimamisha video walipohitaji kupumzika. Hakuna anayepitwa na chochote. Sehemu ya Ijumaa ilikazia kwamba watoto ni kama mishale ambayo inapaswa kulengwa ili wapate maisha yenye furaha na yanayoridhisha kwa kumtumikia Yehova. Kusanyiko hili linanisaidia kutimiza jambo hilo.”—Zaburi 127:4

Kusanyiko hilo la eneo lililofanywa kupitia video mtandaoni, liliwavutia waandishi wa habari duniani pote. Kwa mfano, Robert Hendriks, ambaye ni msimamizi wa Dawati la Habari za Umma nchini Marekani, alisema hivi: “Waandishi wa habari wengi wameandika habari kuhusu kusanyiko lililofanywa kupitia video mtandaoni. Habari zao zilizungumzia jinsi tengenezo letu limekuwa likitumia teknolojia kuonyesha programu ya kusanyiko ili kuwalinda washiriki wake.”

Kusanyiko la eneo la 2020 la “Shangilieni Sikuzote”! limetuonyesha katika njia mpya inayosisimua sana jinsi Yehova alivyo Mfundishaji wetu Mkuu.—Isaya 30:20.