Hamia kwenye habari

DESEMBA 1, 2020
PAPUA NEW GUINEA

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Yatolewa Katika Kihiri Motu

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Yatolewa Katika Kihiri Motu

Ndugu Kegawale Biyama, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Papua New Guinea, alitoa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha ya Kihiri Motu. Programu hiyo ilirekodiwa mapema katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova iliyopo eneo la Port Moresby na kisha kurushwa kwa watazamaji Novemba 28, 2020. Watu zaidi ya 7,000 walitazama programu hiyo.

Papua New Guinea ni nchi yenye lugha nyingi zaidi zinazozungumzwa kuliko nchi nyingine yoyote duniani, kukiwa na lugha 840 hivi zinazozungumzwa. Kihiri Motu ni mojawapo ya lugha tatu rasmi zinazozungumzwa nchini humo. Inakadiriwa kwamba watu 140,000 wanazungumza lugha hiyo.

Ndugu Kukuna Jack, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi, alisema hivi: “Wanaozungumza Kihiri Motu wamekuwa wakisubiria Biblia hii kwa muda mrefu. Tunajua kwamba wataipenda sana Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kwa kuwa ni rahisi kuielewa.”

Kikundi cha watafsiri sita kilitumia miaka kumi kutafsiri Biblia hiyo. Mtafsiri mmoja alisema hivi: “Bila shaka wasomaji wa Biblia hii watafurahia kuona jina la Mungu kuanzia kitabu cha Mwanzo hadi Ufunuo. Tunamshukuru Yehova kwa kutupatia zawadi hii!”

Tunapokumbuka kazi yote iliyofanywa ili kutokeza tafsiri hiyo mpya, tunaunga mkono maneno ya nabii Isaya aliyesema hivi: “Ee Yehova, utatupatia amani, kwa sababu kila kitu ambacho tumefanya ni wewe uliyetutimizia.”—Isaya 26:12.