Hamia kwenye habari

Mazungumzo ya Biblia yenye kutia moyo pamoja na ndugu na dada ambao wamekimbia makao yao

MEI 23, 2022
UKRAINIA

RIPOTI YA 8 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

Ndugu Zetu Wanafanya Ziara Nyingi Zaidi za Uchungaji Kadiri Vita Vinavyoendelea

RIPOTI YA 8 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

Huku hali zikiendelea kuwa ngumu zaidi nchini Ukrainia, ofisi ya tawi ya Ukrainia imeongeza jitihada za kufanya ziara za uchungaji ili kuwafariji ndugu na dada waliolazimika kukimbilia sehemu nyingine nchini. Ndugu na dada zetu waliotembelewa wamenufaika na mpango huo. Mshiriki mmoja wa Halmashauri ya Tawi aliwatembelea ndugu na dada waliokimbia makao yao na ambao kwa sasa wanaishi magharibi mwa Ukrainia. Katika ziara hiyo, dada mmoja ambaye anakaa kwa muda pamoja na wengine 30 hivi katika Jumba la Ufalme lililo kwenye jiji la Uzhgorod alisema hivi: “Nilihisi kana kwamba Yehova alikuwa akinikumbatia kwa upendo.”

Ndugu hao wanajitahidi sana kuwafanyia ziara za uchungaji washiriki 100 hivi wa Halmashauri 27 za Kutoa Msaada. Ihor, mshiriki wa Halmashauri moja ya Kutoa Msaada, anasema hivi: “Nilipopewa mgawo wa kutumikia kwenye Halmashauri ya Kutoa Msaada, tayari mimi na mke wangu tulikuwa tumekimba makao yetu na tulikuwa tunaishi kwenye nyumba nyingine. Tulipozidiwa na uchovu, mshiriki mmoja wa Halmashauri ya Tawi, ambaye pia ana shughuli nyingi sana alitenga muda, akatutembelea na kutusikiliza kwa makini. Tulihisi anatujali kikweli.” Ihor anaendelea kusema hivi: “Tunapojipata katika hali ambayo sisi tunakuwa kama watoto, yaani, hatuna uwezo wa kudhibiti hali tunayokabili, hatuna suluhisho na tunachoweza kufanya tu ni kusali Yehova aongoze mambo, mara nyingi tunaona mkono wake ukitenda kwa niaba yetu.”

Kwa sasa hii ndio hali ya Majumba ya Ufalme yaliyo katika eneo ambalo vita vinaendelea, Majumba 4 yameharibiwa kabisa, Majumba 8 yamepata uharibifu mkubwa, na Majumba 33 yamepata uharibifu mdogo.

Jumba la Ufalme lililo karibu na Kyiv, lilivyokuwa mwaka wa 2019 (kushoto) na lilivyo sasa (kulia)

Kufikia Mei 17, 2022, hizi ndizo takwimu zilizotufikia kutoka Ukrainia. Takwimu hizo zinategemea ripoti za uhakika tulizopata kutoka kwa ndugu walio katika maeneo hayo. Hata hivyo, huenda idadi halisi ikawa kubwa zaidi, kwa sababu ni vigumu kudumisha mawasiliano mazuri katika maeneo yote nchini.

Athari Ambazo Ndugu na Dada Zetu Wamepata

  • Wahubiri 37 wamekufa

  • Wahubiri 74 wamejeruhiwa

  • Wahubiri 45,253 wameacha makao yao na kwenda sehemu zilizo salama zaidi nchini

  • Nyumba 418 zimeharibiwa kabisa

  • Nyumba 466 zimepata uharibifu mkubwa

  • Nyumba 1,213 zimepata uharibifu mdogo

  • Majumba 4 ya Ufalme yameharibiwa kabisa

  • Majumba 8 ya Ufalme yamepata uharibifu mkubwa

  • Majumba 33 ya Ufalme yamepata uharibifu mdogo

Jitihada za Kutoa Msaada

  • Halmashauri 27 za Kutoa Msaada zinashughulikia hali nchini Ukrainia

  • Wahubiri 48,806 wamesaidiwa moja kwa moja na halmashauri hizo kupata makao salama zaidi

  • Wahubiri 21,786 wamekimbilia nchi nyingine na wanasaidiwa na waamini wenzetu