Hamia kwenye habari

Majengo ya ofisi ya tawi ya Chelmsford, Uingereza. Picha ndogo: Ndugu Kenneth Cook, Jr., akitoa hotuba ya wakfu

MEI 27, 2024
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Kuwekwa Wakfu kwa Ofisi ya Tawi ya Uingereza—Wageni Walialikwa Kutoka Nchi 60 Tofauti

Kuwekwa Wakfu kwa Ofisi ya Tawi ya Uingereza—Wageni Walialikwa Kutoka Nchi 60 Tofauti

Mei 18, 2024, majengo ya ofisi ya tawi yaliyo Chelmsford, Uingereza, yaliwekwa wakfu wakati wa hotuba iliyotolewa na Ndugu Kenneth Cook, Jr., mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Jumla ya ndugu na dada 1,518 walihudhuria programu hiyo ya wakfu na wakaketi kwenye kumbi nne za ofisi ya tawi. Washiriki mbalimbali wa Baraza Linaloongoza na wasaidizi wa halmashauri za Baraza Linaloongoza walikuwepo. Ndugu na dada wengine 10,085 waliunganishwa kwenye programu hiyo kupitia video mtandaoni wakiwa kwenye Majumba ya Makusanyiko na vituo vya elimu ya Biblia katika maeneo mbalimbali ya Ireland na Uingereza. Jumla ya wote walioshiriki katika kazi ya ujenzi wa ofisi hiyo mpya ya tawi ilikuwa 11,000, hata hivyo, ni ndugu na dada 3,000 kati yao waliohudhuria programu hiyo.

Ndugu na dada wakiwa katika Jumba la Kusanyiko la Pennine lililo Rotherham, Uingereza, wakisikiliza kwa makini hotuba ya wakfu

Siku iliyofuata, jumla ya ndugu na dada 172,834 walifurahia programu ya pekee ya kiroho ambayo ilipeperushwa kwa njia ya video mtandaoni kwa makutaniko 1,821 katika eneo lote la ofisi ya tawi.

Juma moja kabla ya programu hiyo ya wakfu, wageni walioalikwa walipata fursa ya kutembelea majengo hayo ya ofisi ya tawi. Mipango ilifanywa ili kuwasaidia wageni kujifunza kuhusu kazi zinazofanywa Betheli ili kuunga mkono kazi ya Ufalme katika eneo la ofisi hiyo ya tawi na ulimwenguni pote. Kwa mfano, Timu ya Video ilionyesha hatua zote zinazohusika katika kutayarisha sinema inayotegemea Biblia na wageni walialikwa kutazama onyesho moja lilipokuwa likiendelea kurekodiwa.

Kushoto: Dada akitayarisha viburudisho. Kulia: Timu ya Video ikionyesha jinsi video za tengenezo letu zinavyotayarishwa

Ndugu na dada wakiangalia Mwanzi wa Koreshi walipotembelea Jumba la Makumbusho la London, Uingereza

Kwa kuongezea utendaji huo, ndugu na dada wengi walifurahia matembezi na elimu waliyoipata nje ya eneo la Betheli. Hilo lilitia ndani safari za kwenda kwenye maeneo ya kihistoria yaliyo katika jiji la London na jimbo la Kent ili kujifunza zaidi kuhusu historia ya Biblia nchini Uingereza.

Ndugu Richard Cook, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Uingereza, alisema hivi baada ya juma hilo lililokuwa na utendaji mwingi: “Ilipendeza sana kuona undugu wa kimataifa ukikusanyika pamoja kwa ajili ya pindi hiyo ya pekee. Tulistaajabu kuona jinsi Yehova alivyotusaidia kushinda changamoto mbalimbali na hatimaye tukafaulu kuandaa tukio hilo ambalo lilitukuza jina lake.”

‘Tunashangilia kwa shangwe kubwa’ pamoja na ndugu na dada zetu katika eneo la ofisi ya tawi ya Uingereza kwamba ofisi hiyo maridadi ya tawi imewekwa wakfu kwa Mungu wetu, Yehova.​—Nehemia 12:43.