Hamia kwenye habari

Kushoto: Machi 8, 1947, mamia ya ndugu na dada wakiwa wamekusanyika kwenye Ukumbi wa Mji wa Wellington kwa ajili ya kusanyiko la pekee. Kulia: Nje ya ofisi za Betheli huko 69 Kent Terrace, Wellington, New Zealand

MACHI 7, 2022
NEW ZEALAND

Miaka 75 ya “Kuithibitisha Kisheria Habari Njema” Nchini New Zealand

Miaka 75 ya “Kuithibitisha Kisheria Habari Njema” Nchini New Zealand

Kufikia Machi 2022, Mashahidi wa Yehova watakuwa wameandikishwa kisheria kwa miaka 75 nchini New Zealand. Machi 7, 1947, Ndugu Nathan H. Knorr, Milton Henschel, na Charles Clayton, aliyekuwa mmishonari wa kwanza kuhitimu Shule ya Gileadi nchini New Zealand, walitembelea Bunge la New Zealand. Maofisa wa serikali waliwapa ndugu hao hati za kuwaandikisha kisheria Mashahidi wa Yehova. Leo, kazi ya kuhubiri inazidi kusonga mbele, na kuna wahubiri 14,500 wenye bidii nchini humo.

Ujumbe wa Ufalme ulifika kwa mara ya kwanza nchini New Zealand katika mwaka wa 1898. Idadi ya wahubiri iliongezeka upesi. Kanisa Katoliki lilikasirishwa na jinsi machapisho yetu yalivyofundisha kweli iliyo katika Biblia, kwa hiyo, walichochea watu kuwachukia Mashahidi wa Yehova. Oktoba 24, 1940, serikali ilipiga marufuku utendaji wetu. Lakini, Mei 8, 1941 Bunge lilibadili marufuku hiyo na kuwaruhusu akina ndugu wakutane na kuendelea na huduma. Hata hivyo, waliruhusiwa tu kutumia Biblia, na si machapisho. Machi 29, 1945, marufuku hiyo ilifutwa rasmi na idadi ya wahubiri ikaanza kuongeza tena. Miaka miwili tu baadaye, idadi ya wahubiri wa Ufalme iliongezeka kwa asilimia 40 na hivyo kukawa na kilele kipya cha ndugu na dada 659 wanaotangaza habari njema.

Kushoto hadi kulia: Ndugu Charles Clayton, Milton Henschel, na Nathan H. Knorr wakiwa nje ya Bunge mwaka wa 1947, baada ya kupokea hati za kuwaandikisha kisheria Mashahidi wa Yehova

Mwaka wa 1947, Ndugu Knorr aliamua kutembelea New Zealand wakati wa ziara yake ya utumishi ya ulimwenguni pote. Wakati wa ziara hiyo ndipo alipotembelea Bunge.

Baada ya Mashahidi wa Yehova kuandikishwa, ofisi ya tawi ilifunguliwa katika jiji la Wellington ili kusaidia katika kusimamia kazi ya kuhubiri. Ndugu Robert Lazenby aliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa kwanza wa ofisi ya tawi.

Ndugu Knorr aliandika hivi baadaye katika ripoti kuhusu ofisi mpya ya tawi na idadi inayozidi kuongeza nchini New Zealand: “Wote wako tayari kufanya kazi ya kutegemeza ofisi ya tawi na kufuata mwelekezo wake.”

Machi 8-9, 1947, Ndugu Knorr na Ndugu Henschel walitoa hotuba katika kusanyiko la pekee lilifanywa katika Ukumbi wa Mji wa Wellington. Kipindi cha alasiri kilifanywa katika chuo cha kiufundi kilichokuwa karibu. Ndugu na dada 500 hivi walihudhuria.

Dada Beryl Todd, ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 17, anakumbuka: “Kabla ya hapo sikuwa nimehudhuria kusanyiko kubwa kama hilo, na tulisisimuka kwamba Ndugu Knorr alikuwepo.” Clyde Canty alibatizwa siku hiyo katika kidimbwi cha umma kilichokuwa karibu, na baadaye alitumikia akiwa mratibu wa ofisi ya tawi ya New Zealand.

Machi 10, 1947, watu wengine 300 walikusanyika huko Auckland ili kusikiliza hotuba zilizotolewa na Ndugu Knorr, Ndugu Henschel, na Ndugu Lazenby. Ndugu Knorr alisema kwamba anaona kuna uwezekano wa kuwa na ongezeko wakati ujao nchini New Zealand. Alisema hivi: “Nina uhakika kwamba kutakuwa na ongezeko. Eneo hili lina uwezo wa kuwa na ongezeko kubwa.”

Maneno ya Ndugu Knorr yalithibitika kuwa ya kweli. Kulikuwa na ongezeko la asilimia 18 nchini New Zealand katika miaka minane iliyofuata. Kufikia mwaka wa 1955, kulikuwa na wahubiri 2,519. Mwaka wa 1989, kulikuwa na wahubiri 10,000 nchini humo.

Tunamshukuru Yehova kwa kuwasaidia ndugu zetu kuthibitisha kisheria habari njema nchini New Zealand.​—Wafilipi 1:7.