MACHI 8, 2022
UKRAINIA
RIPOTI YA 1 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia
Maisha yamekuwa magumu sana kwa ndugu na dada zetu katika majiji ya Mariupol, Kharkiv, Hostomel, na miji mingine ya Ukrainia kadiri makombora yanavyozidi kuangushwa. Kwa zaidi ya juma moja, baadhi ya akina ndugu hawajaweza kutoka kwenye vyumba vya chini ya ardhi au sehemu nyingine ambazo wanajificha. Wamebaki na chakula kidogo. Hakuna huduma za umeme, Intaneti, na huduma za simu kwa hiyo imekuwa vigumu kuwasiliana na ndugu na dada wengine.
Inasikitisha kwamba Ndugu Dmytro Rozdorskyi, mzee wa Kutaniko huko Myrnohrad mwenye umri wa miaka 28, alikufa kutokana na majeraha aliyopata baada ya kukanyaga bomu lililotegwa ardhini. Tunasali kwa ajili ya wale ambao wamepoteza wapendwa wao katika kifo na kwa ajili ya ndugu na dada zetu walio katika maeneo yanayoshambuliwa vikali kwa mabomu.—2 Wathesalonike 3:1.
Kufikia Machi 7, 2022, hizi ndizo takwimu zilizotufikia kutoka Ukrainia:
Athari Ambazo Ndugu na Dada Zetu Wamepata
Wahubiri 2 wamekufa
Wahubiri 8 wamejeruhiwa
Wahubiri 20,617 wameacha makao yako na kwenda sehemu zilizo salama zaidi nchini
Nyumba 25 ziliharibiwa kabisa
Nyumba 29 zilipata uharibifu mkubwa
Nyumba 173 zilipata uharibifu mdogo
Majumba 5 ya Ufalme yameharibiwa
Jitihada za Kutoa Msaada
Halmashauri 27 za Kutoa Msaada zinashughulikia hali nchini Ukrainia
Wahubiri 6,548 walisaidiwa moja kwa moja na halmashauri hizo kupata makao salama zaidi
Wahubiri 7,008 wamekimbilia nchi nyingine na wanasaidiwa na waamini wenzetu
Jumba 1 la Kusanyiko na Majumba 30 hivi yaliyo magharibi ya Ukrainia, katika maeneo kama vile Chernevtsi, Ivano-Frankivsk, Lviv, na katika maeneo ya Transcarpathian yameandaliwa kwa ajili ya kupokea wakimbizi