Hamia kwenye habari

MACHI 21, 2023
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

JW.ORG Yatimiza Miaka 10—Sehemu ya 3

Kuendeleza Huduma

JW.ORG Yatimiza Miaka 10—Sehemu ya 3

Katika mfululizo huu, makala zilizotangulia zilieleza jinsi jw.org imetumiwa kutoa machapisho yetu ya kielektroni na video na pia kutoa ripoti za habari kuhusu undugu wetu wa ulimwenguni pote. Makala hii ya mwisho ya mfululizo huu itafafanua jinsi jw.org imetumiwa kuendeleza kazi ya kuhubiri.

Lugha Mbalimbali: Tovuti iliyoundwa upya ilipotolewa Agosti 2012, ukurasa wa mwanzo ulipatikana katika lugha 139. Kufikia Agosti 2014, mwaka ambao kulikuwa na kampeni ya trakti ya kutangaza tovuti yetu, idadi iliongezeka hadi kufikia lugha 500. Kwa kupendeza, hiyo ilitia ndani lugha 22 za ishara. Leo, kuna habari zinazopatikana kwenye tovuti yetu katika lugha zaidi ya 1,070 kutia ndani lugha zaidi ya 100 za ishara.

Makala Zinazotolewa kwa Wakati Unaofaa: Oktoba 2019, ukurasa wa mwanzo wa jw.org uliundwa upya ili kuonyesha makala kuu yenye picha kubwa ya kuwavutia wasomaji, na makala nyingine tatu zilizoangaziwa. Muundo huo unakazia kwa matokeo zaidi habari iliyo kwenye tovuti kuhusiana na huduma. Baadaye, idara ya Uandikaji na ya Uchoraji zilipanga kuwe na njia ya haraka ya kutokeza makala na picha kwa ajili ya ukurasa wa mwanzo ili kuhakikisha kwamba ukurasa huo unakuwa na makala na habari za karibuni za matukio ya ulimwengu. Kwa mfano, ukurasa wa mwanzo umekuwa na makala zilizohusu janga la COVID-19 na pia kuhusu vita kati ya Urusi na Ukrainia na tatizo la wakimbizi linalosababishwa na vita hivyo.

Tovuti Inayowasaidia Watu Kupata Habari Kutuhusu: Tovuti ya jw.org inawasaidia watu wanaopendezwa kupata habari sahihi mtandaoni kuhusu tengenezo letu na kazi yetu. Pia, inawasaidia watu kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova ikiwa wangependa kujifunza mengi zaidi. Mwanamke mmoja ambaye ni kiziwi alijifunza na Mashahidi wa Yehova alipokuwa tineja lakini alipohama akapoteza mawasiliano. Alitaka kuanza kujifunza tena lakini hakuna aliyekuwa amemtembelea katika makao yake mapya. Alikumbuka tovuti ya jw.org na akajaza ombi kupitia mtandao. Katika kipindi cha siku chache tu, alitembelewa na mapainia wa pekee. Hakuanza tena funzo lake tu, bali pia alianza kuhudhuria mikutano. Sasa yeye amebatizwa na anawafunza watoto wake watatu kumhusu Yehova. Anasema hivi: “Ninamshukuru Yehova kwa tovuti hii kwa sababu ikiwa nisingejaza fomu kwenye mtandao, ingenibidi kungoja hadi wakati ambapo ningekutana na Shahidi.”

Kazi ya kuhubiri inapoendelea kufanywa haraka zaidi, inatia moyo kujua kwamba tengenezo la Yehova litaendelea kuandaa vifaa vyenye matokeo vinavyowasaidia watu wanaopendezwa.​—Isaya 60:22.

  • Idadi ya video zinazopakuliwa kila mwezi

  • Idadi ya watu wanaoitembelea kila mwezi

  • Kutolewa kwa nembo mpya ya jw.org, Machi 2013

  • Tovuti inaanza kupatikana katika lugha za ishara, Julai 2014

  • Ukurasa wa mwanzo unaundwa upya ili kuvutia zaidi umma, Oktoba 2019

  • Kutolewa kwa kitabu Furahia Maisha Milele! Januari 2022