Hamia kwenye habari

OKTOBA 25, 2021
ZAMBIA

Biblia Imetolewa Katika Lugha ya Lunda

Biblia Imetolewa Katika Lugha ya Lunda

Oktoba 16, 2021, Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa katika Kilunda katika muundo wa kidijitali wakati wa programu ya pekee iliyopeperushwa kwa wahubiri katika nchi tatu za Afrika. Nakala zilizochapishwa zitapatikana mwanzoni mwa Februari 2022.

Ndugu Emmanuel Chiposa, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Zambia alitoa Biblia hiyo katika hotuba iliyorekodiwa mapema. Ilipeperushwa kwa wasikilizaji nchini Angola, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, na Zambia.

Watu wanaozungumza Kilunda ni wakulima wa mahindi, mihogo, na viazi vitamu. Nchini Zambia, wanaishi karibu na chanzo cha Mto Zambezi unaojulikana sana, ambao ndio mto wa nne kwa ukubwa barani Afrika baada ya Mto Nile, Mto Kongo, na Mto Niger. Mashahidi wa Yehova walianza kuwahubiria watu wanaozungumza Kilunda katika miaka ya 1930 na wakaanza kutafsiri machapisho katika Kilunda mwaka wa 2003.

Septemba 2019, kikundi cha watafsiri wa Kilunda kilihamia ofisi mpya ya utafsiri. Hilo limesaidia kazi kwa kuwawezesha kupata Intaneti inayotegemeka, kutia ndani mambo mengine mengi.

Ofisi mpya ya utafsiri iliyojengwa katika eneo la Mwinilunga, Zambia

Kwa miaka kadhaa, wahubiri walilazimika kutumia Biblia za bei ghali ambazo zilitumia ya lugha ya kale na ambazo hazikupatikana kwa urahisi. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kilunda ni ya wazi na rahisi kueleweka. Kwa mfano, badala ya kutumia neno la umoja “uzao” kwenye Mwanzo 3:15, Biblia zilizopatikana awali katika Kilunda zilitumia neno la wingi. Hilo lilifanya iwe vigumu kwa wahubiri kueleza kwamba unabii huo ulimhusu hasa Yesu. Hata hivyo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kilunda inatumia neno sahihi la umoja.

Watafsiri wamefurahishwa sana na kutolewa kwa Biblia hiyo mpya. Mmoja wao alisema hivi: “Nina uhakika kwamba watu watakaposoma tafsiri hii, watahisi kwamba wamevutwa kwa Muumba wao, Yehova.”

Kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kilunda ni uthibitisho wa ziada kwamba Yehova anawajali watu wa mataifa yote. Biblia hii itawasaidia watu wa Yehova kuendelea kueneza ujumbe wa Ufalme mpaka “kwenye miisho ya dunia inayokaliwa.”​—Waroma 10:18.