Kitabu cha Pili cha Wafalme 24:1-20

  • Uasi na kifo cha Yehoyakimu (1-7)

  • Yehoyakini, mfalme wa Yuda (8, 9)

  • Uhamisho wa kwanza wa kwenda Babiloni (10-17)

  • Sedekia, mfalme wa Yuda; uasi wake (18-20)

24  Katika siku za utawala wa Yehoyakimu, Mfalme Nebukadneza+ wa Babiloni alikuja kumshambulia, Yehoyakimu akawa mtumishi wake kwa miaka mitatu. Hata hivyo, alimgeuka na kumwasi.  Kisha Yehova akaanza kutuma makundi ya wavamizi ya Wakaldayo,+ Wasiria, Wamoabu, na Waamoni yaende kumshambulia. Aliendelea kutuma makundi hayo yawavamie watu wa Yuda ili kuwaangamiza, kulingana na neno la Yehova+ alilosema kupitia watumishi wake manabii.  Hakika watu wa Yuda walipatwa na mambo hayo kwa agizo la Yehova, ili kuwaondoa mbele za macho yake+ kwa sababu ya dhambi zote ambazo Manase alitenda,+  na pia kwa sababu ya damu isiyo na hatia aliyomwaga,+ kwa maana alijaza Yerusalemu damu isiyo na hatia na Yehova hakutaka kumsamehe.+  Na mambo mengine katika historia ya Yehoyakimu, mambo yote aliyotenda, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda?+  Kisha Yehoyakimu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake;+ na Yehoyakini mwanawe akawa mfalme baada yake.  Mfalme wa Misri hakutoka tena kamwe katika nchi yake, kwa maana mfalme wa Babiloni alichukua vitu vyote vilivyokuwa vya mfalme wa Misri,+ kuanzia Korongo* la Misri+ mpaka Mto Efrati.+  Yehoyakini+ alikuwa na umri wa miaka 18 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miezi mitatu huko Yerusalemu.+ Mama yake aliitwa Nehushta binti ya Elnathani wa Yerusalemu.  Yehoyakini aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova, alitenda mambo yote ambayo baba yake alitenda. 10  Wakati huo watumishi wa Mfalme Nebukadneza wa Babiloni walipanda kwenda kushambulia Yerusalemu, wakalizingira jiji hilo.+ 11  Mfalme Nebukadneza wa Babiloni alikuja wakati watumishi wake walipokuwa wakilizingira jiji hilo. 12  Mfalme Yehoyakini wa Yuda akatoka nje kwenda kukutana na mfalme wa Babiloni,+ akiwa pamoja na mama yake, watumishi wake, wakuu wake, na maofisa wa makao yake;+ na mfalme wa Babiloni akamchukua mateka katika mwaka wa nane wa utawala wake.+ 13  Kisha akachukua hazina zote za nyumba ya Yehova na hazina za nyumba ya mfalme.*+ Alivikata vipandevipande vyombo vyote vya dhahabu ambavyo Sulemani mfalme wa Israeli alitengeneza katika hekalu la Yehova.+ Hilo lilitendeka kama Yehova alivyokuwa ametabiri. 14  Akawapeleka uhamishoni watu wote wa Yerusalemu, wakuu wote,+ mashujaa wote hodari, na kila fundi na mfua chuma*+—aliwapeleka uhamishoni watu 10,000. Hakuna yeyote aliyebaki isipokuwa watu maskini kabisa nchini.+ 15  Basi akampeleka Yehoyakini+ uhamishoni Babiloni;+ alimpeleka pia mama ya mfalme, wake za mfalme, maofisa wa makao yake, na viongozi wa nchi, akawapeleka uhamishoni Babiloni kutoka Yerusalemu. 16  Pia mfalme wa Babiloni aliwapeleka uhamishoni Babiloni mashujaa wote, 7,000, na vilevile mafundi na wahunzi* 1,000, wote walikuwa wanaume mashujaa waliozoezwa kupigana vita. 17  Mfalme wa Babiloni alimweka Matania, mjomba wa Yehoyakini,+ kuwa mfalme baada yake na kubadili jina lake kuwa Sedekia.+ 18  Sedekia alikuwa na umri wa miaka 21 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 11 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Hamutali+ binti ya Yeremia kutoka Libna. 19  Sedekia aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova, alitenda mambo yote ambayo Yehoyakimu alitenda.+ 20  Mambo hayo yalitukia Yerusalemu na Yuda kwa sababu ya hasira ya Yehova, mpaka alipowatupa mbali kutoka mbele zake.+ Na Sedekia akamwasi mfalme wa Babiloni.+

Maelezo ya Chini

Angalia Kamusi.
Au “jumba la mfalme.”
Au labda, “mjenzi wa maboma ya ulinzi.”
Au labda, “wajenzi wa maboma ya ulinzi.”