Mwanzo 22:1-24

  • Abrahamu aambiwa amtoe Isaka (1-19)

    • Uzao wa Abrahamu utaleta baraka (15-18)

  • Familia ya Rebeka (20-24)

22  Sasa baada ya mambo hayo Mungu wa kweli akamjaribu+ Abrahamu, akamwambia: “Abrahamu!” akajibu: “Mimi hapa!”  Kisha Mungu akamwambia: “Tafadhali, mchukue mwana wako, mwana wako wa pekee unayempenda sana,+ Isaka,+ usafiri kwenda katika nchi ya Moria+ nawe umtoe kuwa dhabihu ya kuteketezwa juu ya mlima mmoja nitakaokuonyesha.”  Kwa hiyo Abrahamu akaamka asubuhi na mapema, akaweka matandiko juu ya punda wake na kuchukua wawili kati ya watumishi wake pamoja na Isaka mwanawe. Akapasua kuni kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa, kisha akafunga safari kwenda mahali ambapo Mungu wa kweli alimwonyesha.  Siku ya tatu, Abrahamu aliinua macho, akapaona mahali hapo kwa mbali.  Sasa Abrahamu akawaambia watumishi wake: “Ninyi kaeni hapa pamoja na punda, lakini mimi na mvulana huyu tutaenda kule ili kuabudu, halafu tutarudi.”  Kwa hiyo Abrahamu akachukua kuni kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa na kumtwika Isaka mwanawe. Halafu akabeba moto na kisu* mikononi, na wote wawili wakaendelea kutembea pamoja.  Kisha Isaka akamwambia Abrahamu baba yake: “Baba!” Akajibu: “Naam, mwanangu!” Halafu Isaka akauliza: “Hapa kuna moto na kuni, lakini yuko wapi kondoo kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa?”  Abrahamu akajibu: “Mwanangu, Mungu mwenyewe ataandaa kondoo kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa.”+ Na wote wawili wakaendelea kutembea.  Mwishowe wakafika mahali ambapo Mungu wa kweli alikuwa amemwonyesha, Abrahamu akajenga madhabahu hapo na kupanga kuni juu yake. Akamfunga Isaka mwanawe mikono na miguu na kumlaza kwenye madhabahu juu ya zile kuni.+ 10  Kisha Abrahamu akaunyoosha mkono wake na kuchukua kisu* ili amuue mwanawe.+ 11  Lakini malaika wa Yehova akamwita kutoka mbinguni: “Abrahamu, Abrahamu!” naye akajibu: “Mimi hapa!” 12  Kisha akasema: “Usimdhuru mvulana huyo, wala usimtendee lolote, kwa maana sasa ninajua kwamba unamwogopa Mungu kwa sababu hukuninyima+ mwana wako, mwana wako wa pekee.” 13  Ndipo Abrahamu akainua macho yake, na hapo karibu mbele yake kulikuwa na kondoo dume aliyenaswa kwa pembe zake kichakani. Kwa hiyo Abrahamu akaenda na kumchukua kondoo dume huyo na kumtoa dhabihu ya kuteketezwa badala ya mwanawe. 14  Naye Abrahamu akapaita mahali hapo Yehova-yire.* Ndiyo sababu mpaka leo inasemwa: “Katika mlima wa Yehova itaandaliwa.”+ 15  Na malaika wa Yehova akamwita Abrahamu mara ya pili kutoka mbinguni, 16  akamwambia: “‘Naapa kwa nafsi yangu,’ asema Yehova,+ ‘kwamba kwa kuwa umetenda jambo hili nawe hujaninyima mwana wako, mwana wako wa pekee,+ 17  hakika nitakubariki, nami hakika nitaufanya uzao* wako uwe mwingi kama nyota za mbinguni na kama chembe za mchanga kwenye ufuo wa bahari,+ na uzao* wako utamiliki lango la* maadui wake.+ 18  Na kupitia uzao wako*+ mataifa yote ya dunia yatajipatia baraka kwa sababu umeisikiliza sauti yangu.’”+ 19  Baada ya hayo Abrahamu akarudi kwa watumishi wake, wakaondoka wote pamoja na kurudi Beer-sheba;+ na Abrahamu akaendelea kuishi Beer-sheba. 20  Baadaye Abrahamu akaambiwa: “Tazama, Milka amemzalia pia Nahori ndugu yako+ wana hawa: 21  Usi mzaliwa wake wa kwanza, Buzi ndugu yake, Kemueli baba ya Aramu, 22  Kesedi, Hazo, Pildashi, Yidlafu, na Bethueli.”+ 23  Bethueli akamzaa Rebeka.+ Milka alimzalia Nahori ndugu ya Abrahamu wana hao wanane. 24  Suria wake, aliyeitwa Reuma, alimzalia pia wana hawa: Teba, Gahamu, Tahashi, na Maaka.

Maelezo ya Chini

Au “kisu cha kuchinjia.”
Au “kisu cha kuchinjia.”
Maana yake “Yehova Ataandaa; Yehova Atahakikisha Jambo Hilo.”
Tnn., “mbegu.”
Tnn., “mbegu.”
Au “majiji ya.”
Tnn., “mbegu yako.”