Kwa Waebrania 1:1-14

  • Mungu azungumza kupitia Mwana wake (1-4)

  • Mwana ni mkuu kuliko malaika (5-14)

1  Zamani za kale, Mungu alizungumza na mababu zetu kupitia manabii katika pindi nyingi na kwa njia nyingi.+  Lakini sasa mwishoni mwa siku hizi amezungumza nasi kupitia Mwana,+ aliyemweka rasmi kuwa mrithi wa vitu vyote,+ na kupitia kwake aliifanya mifumo ya mambo.*+  Yeye ndiye mng’ao wa utukufu wa Mungu+ na mfano kamili wa utu wake,+ naye hutegemeza vitu vyote kwa neno la nguvu zake. Na baada ya kuzitakasa dhambi zetu,+ aliketi kwenye mkono wa kuume wa Ukuu huko juu.+  Kwa hiyo amekuwa bora kuliko malaika,+ kwa maana amerithi jina bora kabisa kuliko lao.+  Kwa mfano, Mungu aliwahi kumwambia nani kati ya malaika: “Wewe ni mwanangu; leo nimekuwa baba yako”?+ Na tena: “Nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu”?+  Lakini anapomleta tena Mzaliwa wake wa kwanza+ katika dunia inayokaliwa, anasema: “Malaika wote wa Mungu na wamsujudie.”*  Pia, anasema kuhusu malaika: “Huwafanya malaika wake kuwa roho, na wahudumu wake*+ kuwa mwali wa moto.”+  Lakini kumhusu Mwana, anasema: “Mungu ni kiti chako cha ufalme+ milele na milele, na fimbo ya Ufalme wako ni fimbo ya unyoofu.*  Ulipenda uadilifu, nawe ukachukia uasi sheria. Ndiyo sababu Mungu, Mungu wako, amekutia mafuta+ kwa mafuta ya kushangilia kuliko wenzako.”+ 10  Na: “Hapo mwanzoni, Ee Bwana, uliiweka misingi ya dunia, na mbingu ni kazi za mikono yako. 11  Hizo zitaangamia, lakini wewe utadumu; na zote zitachakaa kama vazi, 12  nawe utazikunja kama kanzu, kama vazi, nazo zitabadilishwa. Lakini wewe ni yuleyule, na miaka yako haitafikia mwisho kamwe.”+ 13  Lakini amewahi kumwambia malaika yupi hivi: “Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwaweke maadui wako kuwa kiti cha miguu yako”?+ 14  Je, wao wote si roho kwa ajili ya utumishi mtakatifu,*+ waliotumwa kuhudumu kwa ajili ya wale watakaorithi wokovu?

Maelezo ya Chini

Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Au “wamwinamie.”
Au “watumishi wake wa watu wote.”
Au “haki.”
Au “utumishi wa watu wote.”